Thursday, May 16, 2013

SINDI....NA LAURA PETTIE(15)

15

Wakati jua la alfajiri likichomoza Sindi Nalela alikuwa shambani pamoja na mama yake. Kazi za kutifua ardhi ilikuwa ikiendelea kwa kasi huku kila mmoja akiwa kimya na Sindi akionekana mwenye uso mzito uliojaa mawazo.

Mama Sindi akasimama wima na kulisimamisha jembe  mbele yake. Akamatazama Sindi alivyokuwa akikazana kulima pasipo hata kupumzika.
‘Hivi lini mwanangu utaukubali kweli?’ akamsemesha Sindi ambaye hakugeuka wala hakuonyesha ishara yoyote kuwa alikuwa amemsikia mama yake



‘Sindi!’ Mama yake akamuita kwa sauti ya juu kidogo na Sindi akapunguza taratibu kasi ya kulima na hatimaye akaacha kabisa na kusimama wima naye akiegesha jembe mbele yake. hakumtazama mama yake usoni.

‘unajiumiza bure Sindi….umenuna tangu juzi huongei na mtu ndani…. utadhani sisi ndio tuliopokea mahari…’ mama yake akamlalamikia
Sindi akashusha pumzi kwa nguvu kidogo kiasi cha mabega yake kuonekanayakinyanyuka na kushuka, kisha akamgeukia mama yake

‘sijisikii kuzungumzia haya mambo..’ akajibu kwa mkato akitupa jembe pembeni na kuchapua hatua ndefu ndefu kuufuata mti uliokuwa umbali mfupi toka eneo la shamba. Akatandua khanga aliyokuwa ameitundika hapo mtini kabla ya kuanza kulima na kujifunga kiunoni  kisha akaokota ndala  zake alizozivulia hapo na  kuzibana kwapa la kushoto. Akashika njia na kuondoka akimuacha mama yake anamsemesha kilugha kwa sauti ya kulaumu. hakugeuka!

Alitembea taratibu akikwanyua vitawi kwa mkono wake wa kulia na kuvirusha hewani. Alipolimaliza pori, akaona watu wakikimbia kuelekea uelekeo mmoja. Zile mbio ziliashiria tafrani mahali.

Akasimama kwanza na kukodoa macho ya mshangao, naye akitamani kukimbia pamoja nao na asijue kilichokuwa kinawakimbiza. Akatafuta wa kumuuliza na asimuone kila mmoja alikuwa na haraka ya kufika uko walikokuwa wanakimbilia.

Sindi akanyoosha shingo na kutazama kule walikokuwa wanaelekea watu. Hakuna cha kumstua pia. Akaaamua kuchanganya miguu kuufuata ule uelekeo. Hata mbili tatu akamuona Alma akitokea kule waliokuwepo watu na kuja huku walikotokea. Akafarijika!

‘kuna nini uko?’ akamuuliza Alma alyeonekana kuwa na haraka kupitiliza
‘Twende kwanza..’ Alma akamshika mkono na kumpigisha kona kali, sindi akaunga mchakamchaka usio rasmi akiwa na Alma. Wakakimbia mpaka njia iliyokuwa inaelekea zahanati na Sindi akasimama akihema na kuinama kushika magoti

‘Kuna nini kwanza?’ akauliza kwa ukali huku pumzi zilizotoka zikikosa usawa na zile zilizoingia
‘Namfuata mama’ Alma akajibu akijiandaa kuanza kukimbia tena pasipo kujali kama Sindi angemfuata nyuma au lah.

‘ngoja kwanza…’ Sindi akamzuia  ‘ kuna nini?’ akauliza akimeza mate kwa juhudi kubwa kutokana na kule kuhema kulikombana.
‘Mama Nyanza ameanguka na kuzimia…’

‘Nini?’ Sindi akajikuta anasimama wima ghafla na kule kuhema kukikata bila kutarajia
‘Mama nani…imekuwaje kwanza?’ Sindi sasa akamfuata Alma kwa kasi pengine akitamani ambebe juu juu na kukimbia naye kuelekea uko zahanati. Alma akampa ishara ya kutulia kwanza na wakianza tena kukimbia kuifuata zahanati ambayo kwa pale walipokuwa  ilikuwa imebaki mara tatu ya mwendo waliokwisha kimbia.
Mama Nyanza alikuwa katikati ya watu wakimpepea na wengine wakisema awahishwe zahanati huku wengine wakitaka mama Alma angojwe palepale kuepusha gharama kubwa ambazo hakuna hata mmoja aliyetaka kuzibeba kwa wakati ule.

Uamuzi wa kumngoja mama Alma ukapita na kukawa na hekaheka sasa ya kumpa huduma ya kwanza na watu wakiongea hili na lile kuhusiana na kilichotokea. Wakati mama Nyanza akiwa chini ya uangalizi wa majirani zake. Nyanza Mugilagila alikuwa mjini.

Ndani ya siku mbili alishapata mnunuzi wa kile kibanda cha mama yake na kwa roho moja, alichukua hati ya kiwanja na kuondoka nayo akimuachia mama yakenujumbe kuwa ameiuza nyumba na kiwanja kwa laki tisa na kwamba laki tano angelipa mahari na zinazobaki angefanyia harusi na kwamba angemjengea nyumba nyingine nzuri zaidi.

Mama Nyanza hakuamini alichokisoma asubuhi hii, alihisi mchomo wa moyo, hamaki na hasira ndani yake. Alikuwa ameihangaikia hiyo nyumba ya vyumba viwili kwa takribani miaka karibu sita. Akijinyima apate sehemu ambayo angepaita kwake mara baada ya ndugu wa marehemu mumewe kumkatili kwa kuzoa mali zote alizotafuta na mumewe,

Leo hii Nyanza alikuwa ameitoa rehani sababu ya mwanamke.Alikuwa ameipoteza nguvu yake kwa jambo ambalo kwake halikuwa na maana yoyote. Pale alipokuwa amesimama aliona pakizunguka, ardhi ikinyanyuka na kushuka. Akatoka nje akiyumba an akupaza sauti kumuita Nyanza japo alijua hakuwepo pale wala karibu na pale.

Mama wa watu akaanguka nje ya fensi ya nyumba aliyokuwa anaishi na kupoteza fahamu. Watu waliokuwa wakitoka shambani ndio waliomuona na kumuondoa, wakimkimbiza kwa mwenyekiti kuomba msaada.

Mpaka mama Alma, nesi maarufu pale kijijini, alipofika na kumkagua mama Nyanza, Sindi bado alikuwa hajajua kilichotokea. na kule mjini Nyanza aliamua kulala na kuanza safri ya kurudi kijijini kesho yake.

Usiku wa siku ile, Nyanza alitulia nyumba ya kulala wageni, akizitazama zile pesa kwa tabasamu. Laki tisa! kwake zilikuwa kama milioni tisa taslimu. Alizifunga vizuri na kuziweka chini ya mto wa kulalia. Akajikunyata kitandani, ndani ya shuka. Uso ukiwa na nuru ya matumaini pasipo kujua balaa alilomletea mama yake.
888888888888888888888888

Wakati Nyanza akihisi ahueni moyoni usiku ule, Sindi alikuwa na Maria pamoja na Alma chumbani wa Sindi. Alma alikuwa amejilaza kitandani kitandani miguu yake kuanzia magotini ikijikunja na kuchezeshwa hewani, akiwa amelalia tumbo na kutumia viwiko vya mikono yake kujiinusha kidogo juu akiwatazama Maria na Sindi waliokuwa wanasukana. Sindi alikuwa kitandani na Maria alikuwa ameketi sakafuni, mabega yake yakipita katikati ya miguu ya Sindi akisukwa.

‘Milioni mbili?’ Alma aliuliza,  Maria akageuza kichwa na kumtazama sindi ambaye alijikuta akicheka kwanza.
‘Hamjasikia au hamjanielewa?’ Sindi akawauliza
‘kha! hebu kwanza…’ Maria akajigeuza mzima mzima na sasa akawa anawatazama rafikize hawa wawili kwa awamu kisha akamgandishia Sindi macho.

‘kwa hiyo mahari ya Mzee Dunia inarudishwa  halafu?’ Alama akauliza kwa shauku
‘nataka nikakae mjini kwa muda mpaka hali itulie ndio nitarudi’ Sindi akajieleza alakini ikawa kama vile ametumia lugha isiyoeleweka

‘nini?’ Alma na Maria wakauliza kwa pamoja kama watu walioambizana na Alma akijiinusha na kuketi vizuri.
‘Jamani kipi msichoelewa?’ Sindi akawashangaa
‘Hapo pa kwenda mjini…hebu rudisha sinema nyuma kidogo tuone vizuri….steringi anavyoenda mjini’ Maria akatania na kufanya wote watatu wacheke na kugongesha viganja vyao.

Sindi akafanya utani wa kuchezesha vidole kama mtu alieshika remote control ya tv na kufanya kicheko kizuke upya
‘Kwamba tukisharudisha mahari….hapa ndani hapatakalika si ndio… kuna kubanwa hela umetoa wapi na nini na nini…. sasa mimi nitatrokea mjini kwanza…’ Sindi akawa anajieleza huku wenzake wakimskiliza kwa makini mno. Alma akadakia
‘Kuna mahali pa kufikia…sio mjini ukang’ae macho ste…’ hakumalizia
‘tulia nimalizie basi…’ Sindi naye akamdaka akamziba Alma mdomo
‘….kuna mtu atanipokea na atanipa mahali pa kuishi mpaka hapo Jerry atakapo kuja mjini’ akamalizia ana kuwatazama wenzake kwa awamu. Maria akajikohoza kwa muda na kufanya wenzake waanze kucheka tena

‘Mmmh Nyanza anajua haya?’ Maria akauliza
‘ Ningemweleza saa ngapi na mtu ameondoka sijui hata yuko wapi?’ Sindi akajitetea
‘…zaidi ya kujua atakubali tuuende mjini na Jerry wakati walishachapana ngumi…we toroka zako kimya kimya shosti…ukisema umshirikishe Nyanza balaa lake unalijuaAlma akatoa ushauri ambao hata kabla hajaumalizia Maria alikuwa meshaukubali kiasi ya kunyoosha kiganja chake hewani kuomba kugongewa tano na Alma.

‘Sadaktaaa….namuunga mikono na miguu’ Maria alinyanyua miguu hewani na kuichanua. Sindi na Alma wakacheka na Sindi akamchapa kibao miguu ili airudishe chini miguu yake.

‘Sasa akija akanikuta nimeishia atanielewaje?’ Sindi akaleta wasiwasi wake
‘unajua anarudi lini…mtu hakukuaga…mtu hana hata senti ya kumrudishia Mzee Dunia bado tu unamfikiria….mi mapenzi yenu haya ya moyo kwa moyo siyawezi…dunia moyo mwenzake pesa’ Maria akamnanga Sindi

‘Utamwachia hata kiujumbe mradi tu usimtaje Jerry wa watu tu…..vinginevyo utamuokota tena pori lingine’ Alma akaonya akipiga piga piga miguu yake kufukuza mbu.
‘ mmmh jamani…’ Sindi aliusitia ule ushauri
‘mmh nini sasa?.... halafu sasa huyu Jerry ndio inakuwaje mkishasaidiana kuikimbia ndoa ya hii…. maana cha bure duniani pumzi tu….’ Maria akata uhakika
‘nimeshakwambia tumepishana kuwa marafiki tu…ana wake na mimi nina wangu jamani’ Sindi akatetea

‘Na ndio atoe milioni mbili za kukopa wapi sijui uko ili amuokoe msichana na msichana huyo ni rafiki tu….hadithi za mitume bado zipo duniani wallah….’
‘yetu macho….ila tu muombe sana Mungu huyu kaka asikuuze madanguroni uko maana mwenzangu upeo wa macho yako umeishi shinyanga mjini duka la pembejeo…huko Dar kuna maduka haswaa’ Alma akamkoga shoga yake

‘We nawe ulifika lini dar ukayaona hayo maduka….’ maria akamshushua
‘Umesahau nilienda kwenye harusi ya mama mdogo?’ akatamba Alma
‘Yaani kuingia mjini na Coaster la shinyanga basi ndio mkazunguka mjini kote kuona maduka….’ Maria akamponda

‘Wivu tu….bora wenzio tumeosha hata macho duka la pembejeo…. we ukitoka mbali sana pale zahanati’ Alma akarudisha dongo na maria akasimama na kumvamia Alma akimfinya na Alma akimvutia Sindi kwake kujikinga na dhoruba za maria. Ukatawala utani wa kufinyana na kukingana, wakasahau mjadala wao na mwisho wa siku wakalala pamoja pale chumbani kwa Sindi.
88888888888888888888888

Sindi Nalela alishafanya uamuzi wa kuikimbia ndoa yake na Mzee Dunia. asubuhi hii aliamkia kwa mama Nyanza, wakati huo Nyanza alikuwa bado hajarejea
Hali ya mama Nyanza haikuwa njema hata kidogo. hakuwa na nguvu za kunyanyuka, alionekana kama mtu aliyetaka kupooza kuanzia kiunoni huku mwili ukimtetemeka. Sindi alipoingia kumtazama na kumuachia barua ambayo alitaka imfikie Nyanza. Alishapata uhakika toka kwa rafiki wa Nyanza kuwa angerejea siku hiyo na muda ambao angerejea, Mama Nyanza alimtazama kwa jicho kali sana

‘Shikamoo mama’ akasalimia akipiga goti la heshima
‘Mchawi mkubwa wewe! …toka nyumbani kwangu…toka nje mchawi wewe’ Mama Nyanza alimkaripia na Sindi akamtazama kwa huruma akitafuta maneno ya kumwambia na kukosa.
‘ nina ujumbe wa Nyanza’ Sindi akamudu kusema shida yake
‘Binti!...naomba utoke’ Mama Nyanza alisema akitetemeka na machozi yakimjaa macboni
‘Lakini mama….’

‘toka nje…’ Mama Nyanza alifoka tena akichukua kikombe cha bai kilichokuwa karibu yake kumrushia Sindi, kwa hasira akahaha kutafuta kingine cha kumrushia na kule kuhaha kukamfanya aanguke kama mzigo toka pale kitandani alipokuwa amelala. Hakuwa na uwezo wa kunyanyuka  na Sindi aliachama kwa mshangao baada ya kugundua hali ya mama Nyanza.

Akamkimbilia ili amanyanyue lakini mama nyanza alimnasa vibao na kumtaka asimguse na ishie zake. Akamrushia maneno ya ghadhabu na kumtukana kwa hasira kiasi cha Sindi kuona asingeeleweka hata kidogo. Akaiweka bahasha ile juu ya meza huku machozi yakimtoka.
‘Mama angalau nifikishie huu ujumbe kwa Nyanza…nakuomba mama’ aliongea huku akipokea matusi toka kwa Mama Nyanza ambaye bado alikuwa pale chini akiongea huku machozi yakimtoka.

Sindi akaondoka pale ndani akilia, akaenda kuonana na Jerry kule anakofundishia ambako ndiko alikopewa pesa za safari pamoja na za mahari. Sindi akarudi kwao na kuziweka zile fedha kwenye mfuko pamoja na barua ndani. akaviweka mahali ambapo lazimababa yake angepagusa. Kwenye kabati lenye redio.

Alma na Maria walishamtangulizia nguo zake eneo la mbali, wakiogopa kupita barabarani ambako kila mtu angewaona. Walikatisha porini na kwenda kumngoja Sindi mbali kidogo. Alipomaliza maandalizi yake. Sindi alifunga mlango na kutoka kama mtua nayeenda kuchota maji. Akaipita nyumba ya akina Nyanza ana kusimama kidogo kuitazama. akaipita nyumba ya Mzee Dunia ambako kulikuwa na dalili zote za kuanza kwa maandalizi ya harusi yake. Akafumba macho na kukaza njia, akatembea na kutembea mpaka alipowafikia akina Alma.

Huku nyuma Nyanza alirejea nyumbani lakini hali aliyomkuta nayo mama yake ilimuacha hoi, ilimharibia furaha yake. Akalia sana akimtaka mama yake anyanyuke na kutembea. Mama yake alikuwa kimya pasipo kumsemesha, alikuwa akimtazama tu pasipo hata kumkaripia. Machozi yake yaliongea kuhusu hasira zake na hali yake wakati ule. ile Barua aliyoiacha Sindi ilikuwa chini yam to wa kulalia aliokuwa ameuegemea mama Nyanza. hakuwa ameifungua ila barua, aliamua tu kutompatia Nyanza kwa hasira alizokuwa nayo

ndani ya ile barua kulikuwa na ujumbe…

Mpenzi wangu Nyanza,
naomba upatapo ujumbe huu uje haraka kilimamoto kule porini, nina mengi ya kukwambia na kukueleza. Kwa wazazi wangu nimetoroka ila kwako siwezi, nataka kukuaga, nataka kukwambia nitakuwa wapi na unifuate vipi, nataka kukuachia hata pesa kidogo za chakula na kumsaidia mama. Imebidi niondoke kuikwepa ndoa ambayo ingetutenganisha milele. Nakupenda sana sana sana sana na nimefanya hivi kwa ajili yako kwani najua huna uwezo wa kumrudishia Mzee Dunia mahari yake.
                        Nitakusubiri!
                             Wako
                                    Sindi Nalela

Sindi na wenzake walimsubiri Nyanza mno. Mpaka giza lilikaribia kuingia. nyanza hakutokea. Sindi aliketi chini akilia, alilia sana na kuwapa marafiki zake kazi ya kumbembeleza. Akaagana nao huku nao wakilia. Akatembea akielekea pori dogo ambalo angelivuka na kungoja usafiri. aligeuka mara kadhaa kuwatazama rafiki zake ambao walikuwa wamesimama wakilia na kumtazama anavyoshia.
Walipogeuka na kuanza kuondoka Sindi naye aligeuka na kujitahidi kuondoka bila kuangalia nyuma.

Sindi akatoroka kijijini kwao! Nyanza akiwa hana taarifa zozote. Akawa anajipanga kuamkia kwa Mzee Nalela kupinga ndoa ya Sindi na kurudisha mahari ya Sindi iliyotolewa na Mzee Dunia. Asijue kilichokuwa kinatokea uko kwa Mzee Nalela kwa wakati huo

…… ITAKUWAJE?.....ENDELEA KUFUATILIA!! NIPE MAONI YAKO

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger