Thursday, August 1, 2013

MGENI WANGU:....MHADHIRI WA SAUT BW. ROBERT MKOSAMALI

Leo mgeni wangu ni Mhadhiri wa chuo kikuu cha St. Augustine University of Tanzania, bwana Robert Mkosamali. Pasi kupoteza muda karibu utiririke na mtiririko wa maswali  toka kwa Blogger wako Laura Pettie…. Karibu sana!
MHADHIRI WA SAUT
BW. ROBERT MKOSAMALI

Laura Pettie Blog: Kwa maneno matatu tu, unamwelezeaje Robert Mkosamali?
Robert Mkosamali:     Haahaaa! Ninaweza kumwelezea Robert J. Mkosamali kama mtu simple, straight forward na hardworking!

Laura Pettie Blog:  Kitu gani kilikuvutia kujiunga na tasnia ya habari? Is there any motivational story behind?
Robert Mkosamali:      Kitu kilichonivutia kuingia katika tasnia ya habari ni umaskini uliokithiri wa watanzania hasa wale wanaoishi katika mikoa ya pembezoni. Mikoa hii mbali ya kuwa katika hali ngumu ya maisha ilikosa waandishi wa habari ambao wangeweza kuelezea matatizo ya watu walio ndani ya mikoa hiyo na hivyo kuifanya serikali iweze kuchukua hatua.

Nakumbuka miaka ya 1993 kulikuwa na mfumko wa wakimbizi mkoani Kigoma lakini kwa bahati mbaya maisha ya watu wa Kigoma yalionekana kuwa duni kuliko hata yale ya wakimbizi kutokana na mashirika mengi ya kimataifa ........





na ya ndani kuelekeza nguvu nyingi kuwasaidia wakimbizi ilhali wenyeji wakitumia rasilimali zao chache kuwahudumia wakimbizi hao kwa takribani miezi mitatu kabla ya kuingia kwa mashirika ya kimataifa. 

Kungekuwa na waandishi wa habari wakati huo nchi ingefahamu ni kwa kiasi gani wenyeji wenye hali duni sana  nao walihitaji msaada kama hao wakimbizi. Hii ndio ilikuwa motivation yangu kuingia katika tasnia hii ya habari.

Laura Pettie Blog:       Ni kwa miaka mingapi umekuwa mhadhiri wa chuo cha SAUT na unafundisha kozi gani?
Robert Mkosamali:      Nimekitumikia chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino kwa miaka 14 sasa nikifundisha kozi mbalimbali kama vile news writing and reporting, introduction to computers na kwa sasa ninashughulikia zaidi masomo ya utangazaji kwa njia ya radio yaani radio broadcasting.

Laura Pettie Blog:       Kama si kuwa mhadhiri, unadhani ungekuwa unajishughulisha na nini sasa?
Robert Mkosamali:      Kama si kuwa mhadhiri nadhani ningejikita katika utabibu wa binadamu. Naona tasnia hii bado ina mahitaji makubwa ya watumishi waliobobea na mahitaji ya watu ni makubwa sana. Watu wanapoteza maisha kwa sababu ya kukosa huduma nzuri hasa vijijini. Hii ilikuwa ndoto yangu tangu nikiwa nasoma o-level na ilikuwa ni moja ya mambo yaliyonifanya kufanya vizuri katika masomo ya sayansi.

Laura Pettie Blog:       Kuna madai ya wahadhiri wa kiume kudai rushwa ya ngono toka kwa wanafunzi wa kike vyuoni. Unalizungumziaje hili suala?
Robert Mkosamali:      Rushwa ya ngono imekuwa si suala linaloongelewa tu katika vyuo vikuu lakini hata maeneo ya ajira mpya wahitimu wa kike wanapata matatizo makubwa katika kupata ajira mpaka pale wanapokubali kutoa rushwa ya ngono.
Suala la rushwa la ngono vyuoni linadidimiza maadili ya taifa, linawafanya wanawake kuwa wanyonge na kuwaondolea hali ya kujiamini……linashusha hadhi ya elimu nchini kwani linawafanya watu wenye uwezo na kujiheshimu kuonekana hawana uwezo kielimu na kuwapa wale wahitimu wa kike wenye kukubali suala la rushwa ya ngono lakini hawana uwezo kimasomo waonekane kuwa wana uwezo wa kielimu lakini kiutendaji hawana uwezo wowote.

Ni suala baya ambalo linapaswa kupigwa vita mno…..Ni tatizo la kitaifa na litaendelea kulitafuna taifa kama hatua thabiti hazitachukuliwa kuliondoa tatizo hili.

Laura Pettie Blog:       Hivi Karibuni kumekuwa na malalamiko/ dhihaka na shutuma dhidi ya wanahabari mnaozalisha vyuoni. Wengi wanatuhumiwa kukosa maadili ya kazi/ upeo na weledi mkubwa kuhusiana na majukumu yao. Unalizungumziaje hili tatizo na unadhani linaletwa na nini?
Robert Mkosamali:      Tatizo la kukosekana kwa maadili na weledi kwa wahitimu wengi wanaozalishwa na vyuo vingi Tanzania unatokana na sababu nyingi.

Kwanza, ni kukosekana kwa msukumo wa serikali kuifanya tasnia ya habari nchini kuheshimiwa. Sera ya mpya ya habari imechukuwa imechukuwa muda mwingi kuandaliwa na kupitishwa na serikali na hivyo kuwafanya waandishi walio wengi kutoipenda tasnia hii kwani inaonekana inawaneemesha wenye taasisi ya habari zaidi kuliko wale wanaovitumikia. Hali hii inawapunguzia wanafunzi umakini wa kuipenda na kuitumikia tasnia hii kwa maadili na weledi wa hali ya juu.

Pili, tasnia ya habari imeingiliwa na watu wasiokuwa waandishi. Hivi sana kumekuwa na majina mbalimbali mfano waandishi wa habari makanjanja nk. Wamiliki wa taasisi za vyombo vya habari wanawaajiri watu wasiokuwa na sifa zinazotakiwa na hivyo kuwaharibia wale wenye mafunzo ya uandishi wa habari. Inawezekana wanaochafua maadili na weledi wa uandishi wa habari ni wale wasiokuwa na mafunzo ya maadili uandishi wa habari.

Tatu, ni kukosekana kwa waalimu waliobobea katika masuala ya uandishi wa habari na vifaa vya kujifunza kwa vitendo uandishi wa habari. Vyuo vingi vinapata shida ya kuwa na wanafunzi wengi wasioweza kuwahudumia kwani kuna uhaba wa walimu wa kufundisha masomo husika. Pengine mwalimu anaweza kuwa mzuri kwa nadharia lakini mafunzo kwa vitendo kwake ikawa ni shida hii inawasababishia wanafunzi kuwa na maandilizi hafifu na wanapoingia sokoni wanaonekana hawawezi kitu.

Nne, kukosekana na ushirikiano duni kati ya vyuo na taasisi za habari nchini. Ni wanafunzi wachache wanaoweza kupata nafasi ya kupata mafunzo kwa vitendo katika taasisi za habari nchini. Wakati mwingine wale wanaopata nafasi wanakosa 'mentors' ndani ya taasisi hizo za habari na kuwafanya wanafunzi hao kupoteza muda wao kufanya yale yasioyotegemewa.

Tano, tasnia ya habari kwa sasa inakumbwa na mabadiliko makubwa yanayosababishwa na mabadiliko ya technologia. Leo msukumo wa habari umekuwa katika "New media" na inasikitisha kuwa ni vyuo vichache sana Tanzania vinatia msukumo kuwafundisha watu kutumia "new media" au mitandao ya kijamii nchini. Tuanhitaji mabadiliko katika tasnia ya habari kuwawezesha vijana wetu kuwa na maadilili na weledi uliotukuka.

Sita, Tasnia ya habari imekuwa si sehemu salama kwa waandishi. Mauaji na vitisho vimeongezeka kwa kasi na kuwafanya waandishi makini toka vyuoni kukimbilia tasnia nyingine kwa ajili ya hofu ya usalama wao. Wachache wasiokuwa na jinsi wanaonekana kubaki na kuendelea kuitumikia tasnia hii.

Hizi ni baadhi tu ya sababu zinazobabisha kukosekana kwa weledi na maadili kwa wahitimu walio wengi wanaozalishwa na vyuo leo hii.

Laura Pettie Blog: Kiingereza kimekuwa kikitiliwa mkazo zaidi katika masomo ya uandishi wa habari mf. kuwepo kwa somo la communication skills. Ni kwanini hakuna somo la Kiswahili ili kuwajengea wanahabari umahiri katika matumizi ya lugha ya taifa ya Kiswahili kwa ufasaha? ikizingatiwa asilimia 80 ya vyombo vya habari nchini vinatumia lugha ya Kiswahili kuwasilisha taarifa zao.
Robert Mkosamali:      Lugha si kitu. Ukiwa na weledi unaweza kufanyakazi kwa kutumia lugha yoyote! Mwandishi anapaswa kujua lugha mbalimbali ili kumuwezesha 'audience wake kujua yanayojiri duniani. Fikiria leo anakuja waziri mmoja wa ufaransa na mwandishi hajui kifaransa atawezaje kumhoji waziri huyo ili kupata habari kwa ajili ya 'audience' yake.

Dunia ya leo inatutaka tuwe "multilingua" ili kuweza ku"interact" vizuri na watu na kupata habari toka vyombo vingine vya kigeni kwa lugha mbalimbali ili tuweze kuwahudumia walaji wa habari zetu kwa weledi wa hali ya juu. Kutumia kiswahili peke yake kutawafanya watanzania kuwa watu wanaoweza kuhudumia soko la ndani na kushindwa kuajirika katika soko la dunia. Tunahitaji kubadilisha mitazamo yetu ya ndani na kuwa na mawazo mapana zaidi yenye kutufanya kuona mbali.

Laura Pettie Blog:       Unaizungumziaje tasnia ya habari kwa ujumla nchini Tanzania. Je inakidhi matwaka ya jamii kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni?
Robert Mkosamali:      Kwa kiasi fulani tasnia ya habari imeweza kukidhi matakwa ya jamii kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni. Tatizo kubwa linaloikumba tasnia hii Tanzania na Afrika kwa ujumla ni aina ya mafunzo tuyatowayo kwa waandishi wetu. Leo mwandishi anajua habari kubwa ni siasa pekee wakati kuna habari nyingi ambazo zinapendwa na watu pia.

Tatizo hili linatokana na kutokuwepo na specilized training in journalism vyuoni. Tungependa kuona kuna watu waliobobea katika nyanja za kimataifa, nyanja za uchumi, nyanja za utalii, nyanja za usalama, na hata nyanja za utamaduni. Waandishi walio wengi ni wale "wanaoweza kuandika kila kitu" "Jack of all trades but masters of none".
Tunapaswa kurudi nyuma na kufikiri tunawezaje kuwaandaa vijana wetu as specialized journalist kama ni mtu wa masuala ya Bunge basi anajua taratibu za bunge na anaweza kuibua masuala yaliyofichika bungeni. Mtu kama huyu atawezakuwa na "jicho la tatu" la kuona yale watu wengine wasiokuwa wataalamu katika eneo lake kuweza kuyaona. Kwa jinsi hiyo tutaweza kusema mahitaji ya watu yanatimizwa kwa kiwango kikubwa.

Lakini hili litawezekana iwapo mfumo wa umiliki wa taasisi za habari na utawala ndani ya taasisi hizo utaacha kuyapa kipaumbele maslahi ya watu binafsi na kujikita katika kujatumikia maslahi mapana ya umma.

Laura Pettie Blog:       Katika jamii yoyote yapo makundi ya watu wenye mahitaji maalumu. Watu hawa kama vipofu, walemavu wa ngozi, jamii ya viziwi na kadhalika ni watu wenye haki ya kupata habari na elimu husika. Je unadhani vyombo vya habari nchini na taasisi za elimu kama vyuo vinakidhi mahitaji ya hawa watu kuanzia kupata elimu ya chuo inahusiana na masuala ya habari hadi kupokea habari? Na katika miaka yako ya uhadhiri umeshawahi kufundisha wanafunzi wenye mahitaji maalumu chuoni?
Robert Mkosamali:      Kama ilivyo katika jamii yetu watu wenye mahitaji maalumu wamekuwa hawapewi kipaumbele. Angalia mifumo yetu ya kijamii, angalia vyombo vyetu vya usafiri nk, havitoi huduma maalumu kwa watu kama hao. Hali kama hii pia ipo katika vyuo vyetu. Tuna wanafunzi wasioona, wasiosikia, wenye ulemavu wa ngozi lakini hakuna huduma maalumu zinazotolewa kwao hata kujenga uelewa wa jamii juu ya uwepo wa watu hao na kutafuta namna bora ya kuweza kuwahudumia.

Hali hii inajitokeza pia katika vyombo vya habari. Hakuna sheria, sera au mwongozo wowote unaozitaka taasisi za habari hasa za runinga kuwaajiri watu wenye uwezo wa kutafsiri alama kwa ajili ya watu wasiosikia. Au kuwepo magazeti yanayoandikwa kwa lugha ya wasioona kuweza kuelewa taifa linakwendaje ili nao wawezekufanya maamuzi sahihi kutokana na taarifa wanazozipata.

Katika miaka yangu kama mhadhiri hapa chuo kikuu cha mtakatifu Augustino nimepata kuwafundisha vijana wasiosikia na wenye ulemavu ya ngozi. Kitu kikubwa nilichogundua ni kuwa watu hawa wana uwezo mkubwa wa akili hata zaidi ya watu wenye kusikia na kuona pale ambapo tunawapa attention ya kutosha. Nilimfundisha mwanafuzi mmoja mwenye tatizo la kusikia na nilishangazwa sana na uwezo wake darasani. Nilipaswa kutumia multimedia approach kumfundisha broadcasting na kwa jinsi hiyo aliweza kufanya vizuri.

Laura Pettie Blog:       Wasomi wengi ikiwemo wahadhiri wameonyesha mwamko wa kujiingiza katika chaguzi za kisiasa. Je wewe umewahi kufikiri kujiunga na siasa?... Kwanini?
Robert Mkosamali:      Kwa kweli sijawahi kufikiria kujiunga na siasa na si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Sababu inayonifanya nisijiunge na siasa ni kuwa naona siasa za leo ni za ubabe na zisizojali mahitaji ya watu wa chini. Tunasoma,  kusikia na kuona ndani ya vyombo vya habari kukosekana kwa dawa hospitalini na watoto wanakufa, maliasili ya Taifa inatoweka na vijana wanangamia kwa dawa za kulevya. Ni kazi ya siasa safi kujenga maisha yenye matumaini kwa watu.

Uchumi umekuwa neema kwa wanasiasa na si kwa watu wa kawaida. Tunawezaje kuitumia siasa kuboresha maisha ya watu? Tunahitaji viongozi wenye dhamira ya kweli ya kuyabadili maisha ya watu na si wale wenye nia ya kujineemesha wenyewe na familia zao.

Baadhi ya vyama sasa vinataka umiliki wa uongozi wa nchi hii na kuufanya wa familia. kwa nini turudishe utemi au uchifu katika siasa za kidemokrasia? Bado kuna changamoto nyingi sana katika siasa ambazo hazinipi hamu ya kuwa mwanasiasa! Kwa nini hakuna wagombea binafsi? haya ni baadhi ya mambo yanayonifanya niwe mtazamaji katika siasa za Tanzania.


Laura Pettie Blog:       Katika muda wako wa ziada unapendelea kufanya nini?
Robert Mkosamali:      Katika muda wangu wa ziada ninapenda kujisome vitabu, kutazama TV hasa zenye habari na wanyama na kuwahudumia ng'ombe wangu na kuwatembelea watu wa kawaida kujifunza maisha yao.

Laura Pettie Blog:       Ukipewa nafasi ya kupata chakula cha usiku na watu watatu wa kaliba yoyote toka popote duniani, ungependa watu hao wawe akina nani?
Robert Mkosamali:      Nikipewa nafasi ya kupata chakula ningependa kuwa na watu wa kawaida na wanaharakati wanaowahudimia watu hao ili kuwaunganisha kuwawezesha kujua ni changamoto gani watu hao wanazo na ni namna gani wangependa changamoto hizo zitatuliwe. Watu wa kawaida watatoka vijijini zaidi.
Kwa mantiki hiyo kwa kuwa siwezi kuwaalika wote hao watu watatu nitakaopenda kula nao ni Rais Mstaafu wa Marekani Bill Clinton, Pope Francis na Rais Paul Kagame.

Laura Pettie Blog: Ni sehemu gani duniani ambayo unatamani kutembelea, nab ado hujabahatika kutembelea sehemu hiyo.
Robert Mkosamali:      Sehemu ambayo ningependa kutembelea ni nyingi sana. Lakini ninaona bado kuna sehemu nyingi vijijini nchini Tanzania ambazo sijapata kuzitembelea na kujifunza tunu mbalimbali za makabila yetu Tanzania.

Hivi karibuni nimetembelea Mbulu nikajifunza simulizi nzuri ya binti mmoja wa Kiiraq aitwaye Imbori aliyehukumiwa kifo kwa kutoswa msituni kwa sababu ya kupata ujauzito kabla ya kuolewa lakini akaokoka. Simulizi hii ilinifanya nitengeneze Documentary ili kuwawezesha watanzania wengine ni aina gani ya maisha watu wa makabila mengine waliyaishi katika kusimamia maadili ya makabila hayo.

Hivyo nikipata nafasi ya kuyatembelea makabila hayo nitawezajifunza maisha mengine ambayo sikuyajua!
Kwa upande mwingine nilipata nafasi ya kuishi katika baadhi ya nchi za ulaya kama Italy, Ufaransa na Belgium na hivyo ninahisi ninahitaji kujifunza zaidi kutoka tunu za makabila yetu Tanzania.

Laura Pettie Blog:       Kila binadamu anazaliwa na kipaji chake, na wengi wetu tunajikuta tukikua na kuzeeka pasipo kugundua talanta tuliyobarikiwa. Kwa upande wako unahisi una kipaji gani?
Robert Mkosamali:      Mimi nadhani kipaji changu ni ufundishaji. Hili linatokana na ukweli kuwa kwa muda mrefu nimekuwa nakimbia kazi hii lakini Mungu siku zote amenirudisha kuifanya. Baadaye nimejikuta naipenda na kuwafanya wanafunzi wapende yale ninayowafundisha.

Mwaka jana Mwnafunzi wangu mmoja alipata zawadi ya kuwa mmoja wa washindi wa EJAT na mshangao mkubwa Mwanafunzi wangu huyu bwana Noel Thomson alinitunuku (dedicated) zawadi hiyo mimi. Hili tendo lilinigusa sana na nilihisi machozi kunitoka. Nilimshukuru Mungu na Noel Thomson kwa tendo hilo.

Kijana huyu alilitangaza tendo hili facebook hata bila kunishirikisha kuonyesha ni namna gani nimemsaidia katika kuifikia hatua hii. Kijana huyu pia amefanikiwa kupata zawadi nyingine mbili za EJAT mwaka huu. Mungu aendelee kumbariki.

Kuna wanafunzi wangu wengine wanaofanya vizuri katika utangazaji katika taasisi za habari za Kimataifa kama BBC na Radio France Internationale. Matunda haya yananifanya niamini kuwa kipaji changu ni ufundishaji!

Bw. Mkosamali alipowatembelea wanafunzi aliowahi kuwafundisha ambao sasa ni watangazaji wa Radio France internationale (RFI)- Pichani akiwa na wanafunzi hao

Laura Pettie Blog: Unapendela muziki gani na mwanamuziki gani chaguo lako namba moja?
Robert Mkosamali:      Ninapenda Country music na mwanamuziki chaguo langu namba moja ni Kenny Roggers. Lakini hata hivyo nimekuwa na mapenzi makubwa na blues na kundi jingine la muziki kama Abba na Maddona pia

Laura Pettie Blog:       Kitabu gani cha simulizi ni chaguo lako namba moja?
Robert Mkosamali:      Ninapenda kusoma Gifted Hands cha Ben Carson japo nimevisoma pia vitabu kama Think Big and Big picture na Take Risk. Kitabu nilichosoma cha zamani ni "Something for Joey" ambacho kinazungumzia mtoto mmoja alikuwa mgonjwa wa Lukemi, Joey aliyempenda kakake John Capalletti aliyekuwa maarufu katika American College Football. Siku moja alipopata zawadi ya Kitaifa iliyotolewa na Makamu wa rais wa marekani aliamua kumtunukia mdogo wake Joey kwa kuwa chanzo cha msukumo wa mafanikio yake katika hali yake ya Ugonjwa.

Laura Pettie Blog: Ni nini Falsafa yako?
Robert Mkosamali:      Falsafa yangu ni katika ubongo kuna sehemu iliyolala ambayo inaweza kuwa chanzo cha mabadiliko katika maisha ya kila mmoja. Tunapaswa kuyapa maisha mtazamo mpya! Kwa kuiamsha sehemu hii ya ubongo!

Laura Pettie Blog:        Jina la ubini wako linafanana na la mbunge wa Muhambwe bw. Felix Mkosamali. Je una undugu na Mbunge huyu?
Robert Mkosamali:      Yap! Mbunge wa Muhambwe bwana Felix Mkosamali ni mdogo wangu. Yeye ni mtoto wa baba yangu mdogo ndugu Francis Mkosamali aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kibondo wakati wa utawala wa Nyerere na baadaye wakati wa Mwinyi. Kwa sasa Mzee wetu amestaafu siasa!

Laura Pettie Blog:       Ni kitu gani watu wengi hawakifahamu kuhusu wewe?
Robert Mkosamali:      Kitu wasichokifahamu kuhusu mimi ni vigumu kukijua. Lakini nadhani wengi hawajui kama elimu yangu kwa asilimia kubwa, ukitoa shule ya msingi nimesomea shule za misheni kwa msaada mkubwa wa Mhashamu Askofu mkuu Paul Ruzoka, Fr. Hans Peters and Shirika la wamisionari wa Afrika yaani the White Fathers na St. Augustine University of Tanzania. Kwa kweli ninawashukuru sana kwa msaada wao huo.

Laura Pettie Blog:       Swali la mwisho, una neno gani la ziada kwa jamii?
Robert Mkosamali:      Neno la ziada katika jamii ni kwamba mababu wana mchango mkubwa katika maisha ya wajukuu wao. Naona jinsi nilivyo imetokana na ukaribu mkubwa na Marehemu babu yangu Late Daud Mkosamali aliyenifanya kuwa rafikiake wa karibu na kuniwekea ndoto za kupenda elimu mbali ya kwamba yeye hakusoma na alikufa huku hajui kusoma wala kuandika.

Kama mpishi mwaminifu wa mzungu Daud alijifunza thamani ya elimu aliyoiturithisha sisi wajukuu wake. Hivyo basi babu zetu wa leo tujue nafasi zetu za kuyapa mwelekeo maisha ya wajukuu wetu.


NASHUKURU SANA BW. ROBERT MKOSAMALI KWA KUUTOA MUDA WAKO KWA AJILI YA MAHOJIANO HAYA…..NASHUKURU SANA KWA HILI!....NIWASHUKURU PIA WASOMAJI WA BLOG HII AMBAO KWA NAMNA MOJA AMA NYINGINE MMENISUKUMA KUMTAFUTA BW. MKOSAMALI ILI KUPATA MACHACHE TOKA KWAKE
NI TUMAINI LANGU UMEJIFUNZA KITU KWA NAMNA MOJA AMA NYINGINE


SHUKRANI KWA KUWA NASI!

4 comments:

  1. Nimeipenda sana hii interview. Hongera Laura you sound professional.... Ikuze talent yako kwa kufanya vipindi vya tv....

    ReplyDelete
  2. Safi sana Petty, nashauri pia ufikirie kuwa na Tv program.. Kupitia mawazo yako mbalimbali naona una mafanikio makubwa sana mbeleni. Salam na Big up nyingi kwa Mr.Mkosamali, amejibu maswali yote kisomi sana. We always proud of You Sir"

    ReplyDelete
  3. NDIVYO INAVOTAKIWA IWE.. UMEHAMIA LEVEL NYINGINE HONGERA SANA

    ReplyDelete



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger