Monday, April 22, 2013

SINDI......NA LAURA PETTIE (9)

9
SEHEMU YA TISA
Kule ndani ya gari yule binti alikuwa kitetemeka kiasi kwamba alishindwa kuiokota simu iliyokuwa imengukia miguuni pake huku ikiita. Wakati akiitazama taswira ya uso wa mtu uliokuwa ukimchungulia kwenye kioo cha dirisha, ghafla tu akayahamisha macho yake na kutazama kioo cha mbele cha gari, akamuona mwanaume wa rika la kati akiteremsha kimpando kidogo kilichokuwa kikishuka kuelekea pale alipokuwa, alimtazama mwanaume huyu aliyekuwa na jembe begani na moyo wake ukaingia amani toka kusikojulikana. Alihisi ahueni ikimjia!



Yule mwanaume aliwafikia na kuwaelekea wale wanaume wengine waliokuwa upande wa kulia wa gari lake. Akamuona akizungumza nao huku akicheka, taratibu akanyoosha shingo yake mbele akitaka kumtazama vizuri kijana huyo aliyekuwa amesimama mkabala na tairi la mbele la kulia, akiwa amelitua jembe lake chini na kuliegesha kwenye gari lake.

Hakujua kwanini, lakini ujio wa kijana yule pale, ulimletea amani  na tumaini la kutoka pale salama. Baada ya mazungumzoa mawili matatu huku akicheka na wale wanakijiji wenzie. Nyanza alizunguka upande ule aliokuwa ameketi yule binti, akipita mbele ya gari na kumfanya yule msichana amfuatize kwa macho mpaka aliposimama kwenye kioo cha dirisha la gari na kumgongea kidogo.

Kwa mikono yenye kutetemeka, alibonyeza kitufe kilichoruhusu dirisha lizame chini taratibu na kukutana uso kwa uso na Nyanzambe. Akamuinulia macho na kumtazama mwanaume huyu ambaye kwa tabasamu la kiuungwana alimsabahi kwanza.
‘habari yako?’ Nyanza alimsalimu
Kama unavyoona…..’ alijibu binti yule kinyonge huku uso wake ukiwa bado haujaondokana na wasiwasi uliomletea jasho usoni.

Nyanza alijirudisha nyuma kidogo na kuangalia tairi la nyuma lililokuwa limetitia katika udongo kiasi cha kutoonekana. Akatikisa kichwa kuashiria hali ilikuwa mbaya mno huku akitoa mlio uliofanana na ule wa kumuitia paka chakula!
‘limetitia sana dada…’ Nyanza alimwambia yule binti akionyesha kina cha kutitia kwa kwenda chini.

Msichana hakujibu kitu, alimtazama Nyanza kama mwokozi wake na hili Nyanza alilielewa.
‘Shuka tujaribu kuliondoa hapa’ Nyanza akampa maelekezo ambayo binti yule aliyatii kwa haraka, akionyesha imani yake kwa Nyanza. Aliteremka na kusimama kando akiwa amekumbatia mkoba wake mkubwa kifuani na sasa ndio akawaona vizuri wale vijana waliokuwa vifua wazi.

Wakamsabahi kwa kumpungia, pamoja na kujaribu kumuonyesha walikuwa pale kwa nia ya kumsaidia, bado binti huyu aliwatazama kwa mashaka kidogo, akiyatupia macho yake mapanga waliyokuwa wameshika sambamba na zile sura zao ngumu zilizoonyesha kukomaa kwa shida za kijijini hali weusi wa dhiki ukiwa umewakomalia miilini.

Nyanza akasemezana nao kilugha na wale vijana wakacheka sana, wakianza kuzunguka kule alikokuwa amesimama Nyanza akilitazama lile tairi. Baada ya majadiliano ya hapa na pale ambayo binti yule hakuyaelewa sawasawa sababu ya kuchanganywa kwa Kiswahili na lugha yao. Vijana wawili waliweka mapanga yao chini na kukimbia kurudi kule walikotokea huku waliobaki wakijaribu kuinua ule upande wa gari uliozama udongoni.

Tairi lilikuwa limechimba mno, Wakashauriana kutumia jembe kuchimba sehemu ya udongo ili kulipa tairi nafasi ya kuchomoka pale. vijana wengine wawili nao wakaondoka kufuata majembe huku mmoja akimletea Nyanza lile jembe lake.

Akabaki Nyanza peke yake na yule binti alikuwa bado amesimama umbali mfupi akimtazama Nyanza kwa udadisi. Taratibu akaivuta tshirt yake na kuivua, misuli ya kiume iliyojengeka vyema kifuani pake na mikononi ilimfanya binti yule amkodolee macho Nyanza katika namna ya kuvutiwa naye.

Akachuchumaa na kuvuta panga mojawapo lililokuwa pake chini na kuanza kuchimba, akiweka nafasi kwa ajili ya jembe. Aliifanya kazi ile kwa dakika kadhaa na ndipo wale vijana wawili walioondoka mara ya kwanza wakarejea na chumba kipana kilichoonekana kuwa na uzito wa kutosha kuwaelemea wale vijana kwani walionekana kukibeba kwa taabu kidogo.

kisha wale waliofuata majembe nao wakarejea, kazi ikaanza. Haikuwa kazi rahisi lakini ilitimia na Nyanza akamwambia binti yule aingie garini na kuliondoa gari huku tairi likipita juu ya kile chuma kipana. Gari likanasuka na binti yule akaliendesha mpaka sehemu aliyohisi ni salama na kuliegesha. Akashuka akitabasamu na kuwafuata wale vijana waliomsaidia.

Akashukuru, akashukuru tena na tena nay ale mashaka aliyoyajenga kwa kuwatazama sura tu, yakatoweka! Akafungua mkoba wake na kuupekua pekua, akatoa noti kadhaa za elfu kumi kumi na kuwapatia wale vijana ambao walizipokea kwa furaha nao wakishukuru. Nyanza akakataa kuzipokea zile pesa!

‘Kwanini?’ binti yule akauliza akishangaa pia
‘Ni msaada tu dada yangu….’ Nyanza akajitetea akiokota jembe lake
‘Kwani hawa waliopokea si nao wametoa msaada’ utetezi wake ulipanguliwa. nyanza kacheka kidogo na kuamua kuupokea ile shukrani.

‘Samahani kwa mwenyekekiti wa kijiji ni wapi?’ binti aliuliza akifunga zipu ya pochi yake.
‘Nyanza anaishi’gi uko….ukienda naye atakufikisha’ga mpaka nyumbani’ kijana mmoja akamjibu na Nyanza akatabasamu wakati binti yule alipomtazama kuashiria kuhitaji msaada wake kwa hali na mali.

Wakaongozana kueleka kwenye gari, Nyanza akivua yeboyebo zake na kuzipakata mapajani mara tu alipoingia garini. Binti yule akacheka kwanza
‘Kwanini umevua sasa….’ akauliza akimtazama Nyanza uso ukiwa bado na tabasamu
‘matope dada’ Nyanza akajibu
‘Hapana vaa tu bwana….mbona mimi nimekanyaga matope na sijavua jamani…. ooh jembe tuliweke kule kwenye buti’ akasema yule binti akitaka kufungua mlango wa gari lake kwa ajili ya kuliweka hilo jembe kwenye buti lakini Nyanza akamuwahi..

‘Nitalipakata dada….usipate taabu’ Nyanza akaliingiza jembe lake kwa taabu kidogo na akipata shida pia kuliweka sawa pale alipolipakata, akinusurika pia kumgonga nalo yule binti ambaye alitamani kucheka kwa sauti lakini alijizuia na baada ya kukaa sawa. Msichana aliwasha gari na wakaondoka kuelekea kijijini.

‘Huku mbali sana na mjini….  kuna mabasi yanatoka mjini kuja huku?’ binti yule akavunja ukimya ulioanza kushika usukani kati yao
‘yapo magari ya Ngosha Trans…ila yana masaa ya kuja na kuondoka….ukiyakosa hayo tunatumia baiskeli au pikipiki za kukodi’
‘Ooh…. hakuna watu wenye magari binafsi’ binti yule akadadisi na Nyanza akaonekana kumshangaa kidogo
‘Kijijini hapa?’ akataka kwanza uhakika
‘Yeah…yaani kama watu wenye magari yao kwa shughuli binafsi tu’ akatoa ufafanuzi na kumfanya Nyanza acheke kidogo

‘Anhaa…kuna tajiri Mzee Dunia na maduka  kule juu ndio ana gari yake’ Nyanza akajibu akimtazama kwa umakini yule binti
‘Mtu mmoja tu ndio ana gari?’ binti yule alishangaa na Nyanza naye akamshangaa kwa kule kushangaa
‘Ehee….alikuwaga nayo mawili…akauza moja….ni tajiri ndio maana ana gari’ Nyanza akajibu na kumfanya yule binti apate picha uko aendako. Umasikini ulikuwa wa kutosha kiasi cha mtu kuhisi kumiliki gari ni utajiri. Akatabasamu tu na kushusha pumzi.

‘Unaitwa nani?’ akatabasamu zaidi alipouliza hili swali
‘Nyanzambe Festo Mugilagila’ akajibu akilitamka jina lake lote
‘Wow! what a name!...naitwa Pamela’ akajitambulisha yule msichana
‘Nashukuru kukufahamu….pindia huko hivi’ Nyanza akamuonyesha kona ya kupiga
‘…nyumba ile pale  ndio kwa mwenyekiti’ akajibu Nyanza na hapo hapo akitazama ile njia inayoelekea kwao

‘Mi’ naishi huku …nishushie tu hapa’ Nyanza akaomba msaada tutani na Pamela akaliegesha gari kando ya barabara, akamgeukia Nyanza
‘ooh…okay!....una namba za simu’ Pamela akauliza na Nyanza akatikisa kichwa kuashiria hapana.
‘Sina simu dada…. Asante sana kwa lifti’ Nyanza akashukuru akifungua mlango wa gari ili ashuke
‘ Okay…basi ….’ akamkatiza Nyanza asishuke na Nyanza aliyekuwa ameshashusha mguu mmoja
‘Chukua hii business card yangu…kama utapata mawasiliano…usisite kunitafuta…asante sana Nyanga kwa msaada’ Pamela akashukuru tena
‘Ni Nyanza…Nyanzambe’ Nyanza akamrekebisha na Pamela akacheka
‘Pole!...Nyanza …Nyanza …Nyanza…nimekariti sasa’ Pamela alifanya mzaha uliomfanya Nyanza acheke kwa sauti kidogo na kuteremka. Akampungia mkono na Pamela akapunga pia na kuliondoa gari kuelekea pale alipoelekezwa.

Alifika na kumuulizia mwenye nyumba, kisha akamuulizia Jerry. Dakika tano baada ya kuongea na mwenye nyumba Jerry na chidi waliingia. Pamela akainuka haraka na kumkumbatia Jerry kwa nguvu mno. Wenyeji wakiwashangaa sit u kwa kule kukumbatiana bali pia kwa mavazi ya Pamela, kwa kuvaa kile kikaptura na blauzi iliyoishia juu kidogo ya kitovu kwao alikuwa nusu uchi!

Baada ya kutambulishana na mazungumzo madogo madogo. Jerry na Pamela wakatafuta faragha kwa kuamua kuongelea garini.
‘I still cant believe you are alive Jerry…’ Pamela aliongea kwa hisia akilipapasa shavu la Jerry
‘Yes I am… na tuombe Mungu azidi kuniweka hai…it is so scary Pam…very dangerous…’ Jerry aliongea taratibu akionyesha ni namna gani alikuwa amejaa hofu juu ya usalama wake.

‘I know…’ Pamela alijibu kwa huzuni
‘….una uhakika hakuna anayejua umekuja huku?...’ Jerry alihoji akiwa ametoa macho na Pamela akaitikia kwa kichwa.

‘So una mipango gani kichwani?’ Pamela akauliza akibetua mabega yake yote mawili. Jerry hakujibu haraka, alishusha pumzi na kufumba macho kichwa chake kikilala kwenye kiti. Akatulia hivyo kwa sekunde kadhaa kabla ya kufumbua macho yake na kukigeuza kichwa chake kumtazama Pamela.

‘….Sijui’ kwa sauti ya kukata tamaa Jerry alijibu huku akiuondoa uso wake machoni pa Pamela na kutazama mbele.
‘kuna chochote naweza kukusaidia?’ Pamela akauliza akianza kufukuza fukuza mbu waliokuwa wameanza kujazana katika gari. Giza lilikuwa linaingia kwa kasi sasa.

Wakaongea mengine mengi, Pamela akimpa picha ya hali ilivyo uko mjini, kuhusu baba yake na matamko yake magazetini. Jerry alikaa kimya tena akiwaza kitu. kisha kama aliyekurupushwa akamgeukia Pamela.
‘….utarudi Dar kesho?’ akamuuliza
‘yeah! I have to… kuna kitu unahitaji?’
‘…simu! na pesa ila sina kadi ya benki hata moja….nimepoteza wallet na kila kitu’ Jerry akasikitika
‘Jerry…huu sio wakati wa kuwaza hayo…niko hapa, nimekuletea simu na pesa…I guessed ungehitaji vyote hivyo…..all I need ni usalama wako tu…kama unadhani hapa uko salama kwa sasa basi….tulia kwanza tujue nini ni nini’ Pamela aliileta nuru usoni pa Jerry akaitikia kwa kichwa.

‘You are the best friend Pam…sijui nikushukuru vipi?....’ Jerry aliugusa mkono wa pamela na kuusugua sugua wakati Pamela akitabasamu
‘You don’t have to thank me….hili ni jukumu langu’ Pamela akajibu akiona soni kwa mbali
‘Baada ya hili nataka kukuoa Pamela…sichoki kukueleza hili hata wakati kama huu’ Jerry sasa aliuhamisha mkono wake toka kwenye kiganja cha Pamela mpaka kiunoni na Pamela akajinyonga kidogo alipouhisi mkono wa Jerry kiunoni pake.

‘na lini utakubali ukweli kuwa we are friends and that is all Jerry….’ Pamela alikazia msimamo wake
‘Come on Pam…. ‘ Jerry alibembeleza
‘No!....’ Pamela alikataa na kuutoa mkono wa Jerry maungoni mwake
‘two years now….miaka miwili Pamela…hunitaki at the same time wanaume wanakuja maishani mwako na kuondoka….cant you see I’m here to stay!’ Jerry alimsogelea Pamela zaidi

‘Jerry!....sikuja kujadili mapenzi.. sawa!.... we can’t be together Jerry that is all’ Pamela alitoa tamko lililomfanya Jerry amtazame tu pasipo kuongeza neno.

Pamela Okello alikuwa aina ya mwanamke ambaye mwanaume yoyote angevutiwa naye. alikuwa mrefu, mwenye weusi wa mng’ao uliochagizwa na sura yake iliyokaa kitutsi. alikuwa na umbile tamu, umbile jembamba la wastani lakini lililogawanyika kike. Alikuwa rafiki yake wa karibu na wa muda mrefu. Alimuamini mno na alimshirikisha katika mambo yake mengi.

Baada ya kuachana na msichana wake wa kwanza maishani mwake, Jerry aliumia sana na alikaa muda mrefu bila mahusiano yoyote mpaka pale moyo wake  ulipomchagua Pamela, lakini akakumbana na kizingiti kikubwa cha kukataliwa huku akishuhudia Pamela akitoka na wanaume wengine ambao waliishia kutengana naye.

Miaka miwili ilikatika na Pamela aliendelea kushikilia msimamo wake. Ndani yah ii miaka miwili Jerry aliweza kuufikia mwili wa Pamela mara mbili na kukutana naye kimwili. halikuwa jambo la hiyari ya moyo, Jerry alibembeleza mno tena kwa machozi ndipo Pamela alipoamua kumvulia nguo. Mara hizo mbili alizolala na Pamela ilikuwa kama alimlia yamini, Jerry alimpenda Pamela maradufu na ombi lake la kuwa naye likakuwa mara mbili zaidi.

Pamela Okello alimgomea na alikatalia katakata, akimweleza wazi kuwa hakuwa tayari kumpoteza kama rafiki kwa sababu ya kujaribu kamari ya mapenzi. Alihisi kama uhusiano wao usingedumu basi angempoteza pia Jerry ambaye kwake alihisi alikuwa kama mhimili wa maisha yake.

Pamela Okello aliiona hali ya mfadhaiko aliyokuwa nayo Jerry, akabadili mada haraka sana
‘Kuna mbu sasa…. twende ndani nikukabidhi kila kitu…but unaiaminihii familia?’ Pamela akauliza akijipiga piga vikofi kukimbiza mbu na Jerry akaitikia tu kwa kichwa kisha akafungua mlango wa gari na kutoka. Pamela akamtazam Jerry alivyopita mbele ya gari na kuielekea ile nyumba ya mwenyekiti. Akashusha pumzi kwa nguvu na kupandisha vioo vya madirisha. Akashuka na kumfuata Jerry ndani.
88888888888888888888888888

Fiona Agapela alikuwa restaurant pamoja na rafiki yake Azda walipata chakula cha usiku. Fiona alitafuta funda lake la mwisho la chakula kwa haraka na kukishushia na kinywaji chake, alipoitua glasi yake, akatumia ulimi wake kusafisha safu ya meno yake ya juu kabla kuchukua kijiti cha kuchokonolea meno.

Rafiki yake aliyekuwa ndio kwanza yu katikati yam lo alinyanyua kichwa chake na kumtazama Fiona usoni.
‘hivi akija kujua hizi hekaheka utatokea mlango gani?’ Azda alimuuliza
‘Hawezi….mpaka leo hii hajajua aliyempumzishia Sophia wake ndio aje kujua hili la usia?..... aah wapi’ alijiamini

‘….lakini hili sekeseke lingekuwa na amani kama J angepatikana tukalia tukazika….haya mambo ya kupotelea wapi sijui…siku ya siku mtu anakuibukia vuuup!’ alionya Azda

‘niliowatuma kazi ni watu wanaoijua kazi yao….wamenihakikishia alikokimbilia siko kabisa…maana walimchukua mpaka porini uko…..wakampakiza kwenye helkopta…wakampeleka vijiji gani uko sijui ila ni Shinyanga….sasa walipompakiza kwenye gari ndio akaanzisha ngumi….piga nikupige ikatembea….ndio mwehu yule akatoroka ila tayari alishakula kisu cha ubavu na walimsaka kweli ikaonekana kakimbilia porini zaidi…’ Fiona aliongea kana kwamba alikuwepo

‘Enhee!’ Azda akaitikia kishabiki huku akitafuna kuku aliyekuwa bado kamshikilia mkononi

‘hawezi kuwa hai….tatizo linabaki ‘Will’ ya bwege huyu sijui itabadilishwa lini’ akalalamika kidogo
‘ukute na hekaheka hiyo wewe ndio umendikwa humo’ Azda akatania
‘Subutu! ….Kristus huyu huyu ….niliwahi kumdadisi Dennis yule mwanasheria wake…akaniambia ameandikwa Jerry…just imagine mali zote zile arithi Jerry wakati mimi miaka nenda miaka rudi napoteza nywele kisogoni…kha!’ Fiona alimchekesha Azda ambaye alicheka kidogo apaliwe.

‘Wanawake tuna dhambi jamani….yaani mzee wa watu anajua anapendwa kwelikweli kumbe wapi….watu tunatimiza wajibu tu…’ azda alishabikia
‘kumbe je….na will ikikaa sawa tu nay eye anawafuata wenzake….’ Fiona akasema kwa sauti ya kunong’ona kidogo akimsogelea Azda.

Wakacheka na kugongeshana viganja vyao
8888888888888888888

Asubuhi ya siku iliyofuata Sindi Nalela alimkia shambani kwanza kisha karejea nyumbani ambako aliweka jembe lake jikoni na kuchapa mwendo kuelekea nyumbani kwa mwenyekiti. Alifika pale nje ya kubisha hodi huku akiendelea kushangaa gari lililokuwa limeegeshwa nyumbani kwa mwenyekiti.

Akatoka mama mwenye nyumba na kusabahiana na Sindi. Sindi akaomba mzigo aliotumwa na mama yake. Mke wa mwenyekiti akaingia ndani na kumuacha Sindi amesimama pale mbele ya nyumba, akilitazama lile gari.

Wakati akilisanifu kwa macho, mbele yake akamuona Jerry akiwa na binti aliyevalia mavazi ya kisasa, wakitembea taratibu kuelekea pale alipokuwa amesimama. Ni dhahiri walikuwa wanatoka matembezini. Sindi akarudi nyuma kidogo kutoa nafasi mlango ingali wakiwa mbali kidogo.

Walipomfikia, Jerry alimchangamkia Sindi ambaye alishindwa kutoa ule uchangamfu wa siku zote akichelela kumkwaza Pamela ambaye hakumjua ni nani kwa Jerry.
‘utaenda kufundisha leo?’ Jerry akamuuliza na Sindi akaitikia kwa kichwa, wakati wote huo Pamela akimtazama Sindi kama kinyago asichokielewa.

Aliazia utosini kwenye nywele nyingi, ndefu na za asili, akaja katika gauni lililopauka na kushikizwa ovyo ovyo, akahamia kwenye khanga kuukuu aliyokuwa amevaa, kisha akaitazama miguu yake iliyokuwa peku ikiwa na tope la shamba. Alimuonea kinyaa!

Sindi akatabasamu tu kipumbavu kila Jerry alopomzungumzisha mpaka pale mwenye nyumba aliporejea na mfuko mdogo ambao Sindi aliupokea kwa kupiga goti mpaka chini kama ilivyokawaida yake na heshima ile ilimfanya Pamela azidi kumtazama kama kituko ila ndani ya moyo wake wa kike alikiri Sindi alikuwa msichana mzuri sana kwani pamoja na uduni wake wote, uzuri asilia wa Sindi ulionekana dhahiri!

Pasipo sababu ya msingi alihisi tu kutompenda Sindi!

....UNA LA KUSEMA?..... LISEME TU!

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger