Monday, April 15, 2013

SINDI....NA LAURA PETTIE (7)

7
SEHEMU YA SABA
Siku mbili baada ya ugomvi wa ngumi kati ya Jerry na Nyanzambe. Jerry alikuwa akizungumza na Mama Alma, nesi aliyekuwa akimhudumia na kumtazamia kidonda chake.

‘Hali yako haijawa njema bwana mdogo….sitarajii ujitoneshe kiasi hiki na uone ni jambo dogo’ Mama Alma alimgombeza Jerry wakati akifunga vifaa vyake baada ya kumsafisha kidonda


‘Ilikuwa bahati mbaya mama…’ Jerry alisema akijitutumua kutabasamu katikati ya maumivu aliyokuwa anayasikia
‘Na isijirudie tena…umenielewa?’ Mama Alma alimuuliza uso ukiwa na ile huruma ya kimama. Jerry akaitikia kwa kichwa na akuagana na mama Alma ambaye alitoka na kuishia akimuacha Jerry pale alipokuwa akiuma meno na kujilaza chali.

Akili yake ilikuw ana mengi kwa wakati ule. Alitabasamu alipofikiria sababu za yeye kutoneshwa vile. Mwanamke!
Hakuwa mtu wa kupigana sababu ya mwanamke na mpaka dakika ile hakukuwa na mwanamke mbaye angesimama na kudai Jerry alikuwa mali yake. Wakati akiwaza hili jina la mtu likapita katika akili yake Pamela Okello! Mwanamke mrembo, msomi mwenye maisha yake, rafiki yake wa muda mrefu sana na mwanamke ambaye alikuwa akimpigia misele siku nyingi, akimbembeleza awe wake, akimshawishi na kujitahidi kumvutia kwake bila mafanikio.

Pamela Okello alikuwa amegoma kuwa mpenzi wake, alikuwa amegoma kuvunja urafiki wao sababu ya mapenzi, alimkatalia Jerry katakata akiutetea urafiki wao. Alikuwa akimngoja Pamela maishani mwake lakini ghafla hisia zake zilianza kutekwa na Sindi Nalela ambaye ni kama alimvamia na kuuchukua moyo wake jumla jumla. Jerry alicheka kivivu akikumbuka tukio la yeye kutandikwa ngumi.

Tabasamu lile likafifia taratibu alipoirudisha akili yake katika kile alichokuwa akikiwaza usiku na mchana. Moyo wake uliumia na akajikuta akifumba macho na kuyasikilizia maumivu yale sambamba na hasira zilizomtembelea kila alipofikiria kitu hiki
‘baada ya kumuua mama ameona na mimi animalize….i hate you….i hate you’ alitamka kwa ghadhabu kali alimfikiria baba yake. Alizisikia vema kauli za wale waliomteka na kumburuza kama gunia. Aliwasikia vema wakati wakipokea maelezo ya namna ya kumuua na aliisikia vema mmoja wa wale watu waliomteka akimuarisha mwenzake ampigie simu Agapela.

Moyo ulitikisika kwa ghadhabu…. Aliuma meno na kudumba tena macho safari hii akiyasikilizia maumivu ya moyo na maumivu ya kidonda chake.

8888888888888888888888888
Jerry Agapela alishusha pumzi na kuikodolea macho dari kana kwamba ingempatia majibu ama japo tulizo la moyo kwa wakati ule. Alikuwa na mipango mingi kichwani aliyotaka kuitekeleza mara baada ya kupona kidonda chake ubavuni. Kwa wakati huu alitaka kujificha kujijini pale huku akijipanga ni wapi aianzie mipango yake. Maisha yake yalishakuwa hatarini na kibaya zaidi akihisi baba yake ndiye aliyekuwa anamuwinda.

Alitulia vile akiipa akili yake nafasi ya kutulia, akiomba Mungu aliyoyaongea na mwenyekiti yawe kama alivyoahidi. Kumficha!
Akashusha tena pumzi kwa mkupuo na kugeuza kichwa chake taratibu akitazama dirishani. Moyo wake ulijaa utusitusi na ghafla tu alimkumbuka marehemu mama yake. Aliumia, aliumia sana lakini akajikaza kiume na kutabasamu kizembe akijifariji, faraja ya uongo, faraja ambayo haikudumu moyoni walau kwa sekunde tano. Uso wake ulijaa makunyanzi ya huzuni akafumba tena macho kuupisha uchungu uliomchoma mithili ya mshale wa moto.

Wakati akiwa katika hali ile, Chidi aliingia mule chumbani akiwa na kikombe cha uji. Akamtazama Jerry namna alivyokuwa amezama mawazoni na kutikisa kichwa. Haikuwa mara ya kwanza kumkuta katika hali kama ile. Alitamani kujua yanayomsibu lakini Jerry alikuwa msiri kwake. Akamfuata mpaka pale kitandani na kumshtua
‘Hey…’ alipaza sauti kidogo na kumfanya Jerry ageukie kule alikosimama, tabasamu dogo likiijiunda usoni pake.

‘Usiniambie bado unamuwaza Sindi?’ akamtania Jerry akingoja anyanyuke kidogo na kumkabidhi kile kikombe cha uji
‘hahahahaaa…. kama tu nataka kupokea kichapo kingine….’ Jerry alijibu akipokea kile kikombe na moja kwa moja kukikimbizia mdomoni. uji wa moto ulimchoma midomo yake na akajikuta akiupuliza kupunguza makali.

‘Nyanza yule bwege sana aisee…. ameshapigana sana  sababu ya Sindi….kuna siku alichapana ngumi sokoni kidogo alale polisi’ Chidi alikuza stori akivuta kiti cha chuma kilichokuwa pembeni na kukalia kwa mtindo wa kukigeuza sehemu ya mgongo wa kiti kuelekea mbele.

Jerry akaacha kupuliza uji na kuangua kicheko kidogo
‘Jamaa akajiunge na masumbwi tu….yaani alinishtukiza na ngumi za ghafla acha kabisa….kwanza nilidhani ananitandika na kipande cha ubao….ila niliposhuhudia anatoka mikono mitupu nikasema dah!.... jamaa noma’ Jerry alisimulia akicheka na kumfanya chidi naye acheke kwa sauti zaidi.

‘Yule na mimi hazipandi kabisa….tulishazinguana kipindi f’lani sababu ya huyu huyu Sindi…. ikawa kila tukikutana mahali ugomvi tu…. mpaka tukawekewa kikao na wazee…. jamaa hajiamini na demu wake kabisa’  Chidi alisimulia sakata lake na Nyanza

‘Na ndio atampoteza sasa…. but honestly….yule binti hamstahili mtu kama Nyanza…. she is smart upstairs na ikitokea akaoga akatakata…akavalishwa kimjini mjini unaweza kuporwa mtoto yule na rais’ Jerry alitania
‘mambo ya shigongo rais anampenda mke wangu….’ Chidi alirejea moja ya vitabu vya mwandishi mahiri wa simulizi na kuleta kicheko kati yao

‘Toka moyoni I love that girl….’ Jerry alizungumza akitikisa kichwa kulia na kushoto

‘we lala hapo umuote tu…. kuna jamaa wa mitaa ya kule karibu na soko….baba yake ndio anamiliki shule inayoonekana kule kilimani…. alipiga misele pale miezi na jeuri ya pesa zake mpaka akawekeana na dau na mchizi mmoja anamiliki mabasi ya kutoka town  uko….. hela zilienda na mtoto alimkosa’ Chidi alimvunja moyo Jerry ambaye alimsikiliza kwa makini, usoni akionyesha mshangao na dalili za kutoamini.

‘ watoto wa kike wanavyopenda hela…huyu wa wapi sasa’ Jerry aliuliza kwa mshangao
‘Ndio ujue mshamba mshamba Nyanza kakamatia kifaa….wewe na pesa zako utaishia kula kwa macho tu’ Chidi alitania akinyanyuka toka pale alipoketi
‘Kakamatia wapi na mnasema hajafungua kizibo’ Jerry alibisha akipiga funda kadhaa za uji na kujilamba midomo
‘na ndio ukisogolea unakula ngumi zako mbili tatu hurudi tena’ Chidi sasa alifanya Jerry acheke kwa muda na kwa sauti zaidi.

Chidi akajinyoosha na kupiga mwayo mrefu
‘napeleka mahindi hapo mashine….tutaonana mida’ Chidi akaaga akipiga tena mwayo na Jerry akaitikia kwa kichwa akimpa ishara ya dole gumba. Akabaki mwenyewe.
‘Sindi Nalela…’akalitamka jina hili kwa sauti ya chini ya kuvutia yenye mbwembwe, akirejesha tabasamu lake usoni. Kwa wakati ule hakuwa na hakika kama alitaka kufanya alichokuwa anataka kufanya ingawa moyo wake ulishamwashia taa ya kijani.
88888888888888888888888

Wakati Jerry Agapela na Chidi wakimzungumzia Sindi Nalela. Binti huyu alikuwa ameketi kitandani akichezea chezea kucha zake akiwa amejiinamia. Alitulia hivyo mpaka pale mlango wa chumba chake ulipofunguliwa na Alma kuingia kwa kasi na kuufunga mlango. Hali ya kiwewe ikamshika Sindi ambaye alimtolea macho Alma akimtazama toka alivyoingia mpaka alipoketi kando yake.

Wakatazamana! Alma akimshika Sindi viganja vyake na kumtazama kwa huruma wakati Sindi alikuwa akimtazama Alma kwa usongo wa kujua atakachotamka Alma.
‘Niambie tu…’ Sindi alimudu kutamka akipepesa macho yake meupe yaliyoanza kujaa chembechembe za machozi. Alma akameza mate  na kumtulizia macho Sindi, akimtazama machoni kana kwamba hakutaka kutamka lakini ilimpasa kutamka alichotaka kutamka

‘Amekataa…’ akajitutumua na kumpa jibu Sindi na akishuhudia mtetereko wa Sindi uliyoyaruhusu mafungu ya machozi machoni yake yadondoke kwa awamu, akiangua kilio cha chini chini huku akiwa ameziba mdomo wake kwa mkono wake wa kuume uliokuwa ukitetemeka.

Alma akateremsha mabega yake kichovu, akimvutia Sindi kwake na kumlaza mapajani mwake. alimsugua sugua mgongoni akimtaka anyamaze. Sindi akalia kwa muda kisha taratibu akajiinua akifuata machozi na kumtazama Alma kwa huzuni
‘nitafanyaje?’ akauliza kwa sauti ya kukata tama
‘muache kwanza apoe….bado ana hasira….’ Alma alimpa ushauri ambao Sindi aliukataa kwa kutikisa kichwa

‘Vipi ikiwa ndio ameamua kuniacha?..... Mwambie Maria akaongee naye jamani’ Sindi akazungumza akiomboleza
‘haitasaidia Sindi…mwache atulize akili yake atakufuata tu’
‘Sidhani Alma….alimuona akinigusa, alisikia yote aliyoongea’ Sindi akatoa wasiwasi wake akiuvuta upande wa ncha ya khanga kukausha kamasi nyepesi puani.

‘kwani kosa lako nini…. si hukumgusa wala kufanya kitu cha ajabu?’ Alma alitaka uhakika na  Sindi akabetua bega lake la kushoto juu chini akikataa kutofanya chochote
‘sasa hekaheka ya nini?....unavyo mpaparikia ndio unamjaza kiburi….hebu tulia kwanza tuone mwisho wake’ alma alitoa pendekezo ambalo kwa Sindi ilikuwa kama vile kumtaka ajisahaulishe kuhusu Nyanzambe wake! Hakujibu, alijiinamia kinyonge machozi yakimuandama tena.
888888888888888888888

Jioni ya kesho yake Mama Sindi akiwa anatwanga mahindi nje, anaona pikipiki ikija upande wa nyumba yake. Anaachana na kazi ya kutwanga na kusimama akiitazama ile pikipiki mpaka ilipofunga breki uwanjani pake. Wifi yake Mama Solomon akiwa na sanduku lake dogo alishuka katika pikipiki naye akaweka mchi kando na kumlaki. Wakisalimiana kilugha wakati Mama Solomon alipokuwa akitafuta hela ya kumlipa dereva wa pikipiki.

Dakika mbili mbele walikuwa mkekani nje ya nyumba, vicheko vikitawala na stori za kilugha zikichukua nafasi. Nusu saa baadaye Denzi alikuwa alileta uji wa ulezi katika vikombe na kuwakabidhi. Mkeo wao wape nje ulizaa kikao ghafla mara baada ya baba yake Sindi kufika.

Giza lilishaingia sasa na kikao kikahamishiwa ndani ambako taa ya kandili iliyokuwa katikati ya sebule liongeza mwanga kiasi. Sindi alikuwa jikoni akipika pamoja na wadogo zake huku Peter akiwasumbua kwa hili na lile. Sindi akanyanyuka na kusimama kwenye kizingiti cha mlango akisikiliza yale yaliyokuwa yakiendelea sebuleni

‘…..Sijaona mantiki ya kumuoza Sindi kwa mtu mzima aliyejiishia vile’ Mama Solomon alipinga hoja ya kaka yake kumuoza Sindi kwa Mzee Dunia
‘Imebidi mama Solo…..Sega anahitaji kwenda chuo…hela inayotakiwa ni nyingi sana…. shamba langu ndio walichukua na fidia sikupata…. hatumuozi kwa kupenda hata yeye anajua anaolewa ili tumsomeshe kaka yake’ Mzee Nalela alijieleza kwa dada yake.

‘Sega mwenyewe yuko wapi?’ Mama Solo akauliza
‘yuko mjini uko kwa rafiki yake’ Mama Sindi alijibu, yeye na mumewe wakimkodolea macho Mama Solomon, dada mkubwa wa Mzee Nalela ambaye ni mwalimu katika shule moja ya kata kijiji kingine.

Kwanza mmemnyima Sindi haki yake ya kupata elimu…. na pale alipo Sindi sio mtoto jamani….lazima kuna mahali moyo wake umeshawekeza hisia zake na matarajio ya maisha ya pamoja na kijana mwenzake….’ Mama Solo aliongea kwa hisia na Sindi pale alipojibanza akatikisa kichwa kukubaliana naye.

‘…..mnazikatili hisia zake na kumuoza kwa mzee kama yule….mnamtoa kafara kwa manufaa ya elimu ya kaka yake ambaye sidhani kama akija kufanikiwa atakumbuka kuna mtu amemfikisha hapo alipo kwa gharama ya kuuza furaha yake…. yeye Sega kama anajua zinahitajika pesa za chuo kwanini asiingie shamba akafanya vibarua akakusanya hela?.....wenzake wanalima huku wanavua samaki na bado wanaingia mtaani kubeba matofali ili wapate hela ya kununulia mashamba wayamiliki…yeye kaweka miguu mjini anasubiri dada aozwe huku yeye akasome….kitu gani hiki?’ Mama Solomon aliongea kwa sauti yenye jazba kidogo

‘Sasa mtu msomo kama Sega utamshikisha jembe wapi wifi jamani….mwenyewe anasema kilimo kazi ya kishamba….’ Mama Sindi akalalamika
‘na atawatukana sana tu…kilimo kazi ya kishamba wakati ndio kazi iliyomfikisha hapo alipo…..’ Alizidi kugomba wifi mtu.

‘…Mahari tumeshapokea dada….cha msingi tunamngoja arudi toka uko mjini dasalama alikokwenda …akirudi amalizie mahari achukue mkewe…. mwisho atazalia hapa nyumbani adodee hapahapa…..’ baba Sindi alitoa neno lake ambalo lilionekana wazi kupingwa na Mama Solomon. Mabishano yakazidi kuchanganyia huku jikoni Sindi akisikiliza kila neno.

‘Pwachaaaa!’ mlio wa sufuria kudondoka ndio uliokatiza mjadala mzima. Sindi akageuka haraka kutazama kule ulikotokea mlio. Peter alikuwa amesimama, mikono kichwani huku sufuria lililokuwa na mahindi ya kuchemsha likiwa sakafuni na mahindi kadhaa yakiwa yametawanyika huku na kule. Denzi aliyekuwa anasonga ugali aliachama mdomo wake kwa mshangao wakati Danze pacha wa Denzi aliyekuwa anakatakata majani ya maboga alikunja tama akiwa na kisu mkononi, wote wakimtazama Peter.

‘Sindiii….kuna nini uko’ mama yake aliuliza na pasipo kumjibu Sindi alimfuata Peter na kumtandika vibao mfululizo. Peter akapiga mayowe na wale wanawake pale sebuleni wakanyanyuka na kukimbilia jikoni.
‘Basi imetosha jamani…’ Shangazi akamdhibiti Sindi ambaye alikuwa akimtandika mdogo wake vibao huku machozi yakimlenga.

Sindi akajikwatua toka mikononi mwa shangazi yake na kutoka mule jikoni, akipita kwa kasi pale sebuleni na kuishia chumbani baba yake akimtazama kwa mshangao pia. Alijitupa kitandani na kulia kwa kwikwi. Hasira!
Mama Sindi na wifi yake wakatazamana.
‘kuna la zaidi hapa wifi….kuna la zaidi ya haya mahindi….’ Mama Solomon akaweka wazi hisia zake na mama Sindi akashusha pumzi kinyonge akigeuka kumtazama Peter aliyekuwa amejikunyata chini akilia.

Wakati wakitoka mule jikoni Sindi aliwapita na kutoka nje. Akajitosa katika giza lililopaushwa na mwanga wa mbalamwezi na kutembea mwendo wa haraka akizipita nyumba kadhaa na kukata kona moja iliyomuingiza kwenye kichochoro kidogo na kuibukia nyumbani kwa mama Nyanza. Alimkuta mama Nyanza akichoche moto wa kuni ili uji wa ugali uliokuwa jikoni uchemke. Akamsalimia mama Nyanza kilugha huku akipiga goti na mama Nyanza akaitikia akimkazia macho binti huyu.

Kigugumizi kikamshika ghafla, lilikuwa jambo la aibu kumuulizia mwanaume kwa mama yake. Mwanaume ambaye hakuwa ndugu yake wala mume wake. Alibaki akimtazama Mama Nyanza kwa huruma akitamani sana kutamka lolote la kuelezea shida yake lakini maadili yalimbana. Alifuata nini pale! akajikuta akijiuliza, wakati alipoiburuza miguu yake mpaka pale alitegemea nini?....angezumza nini?...akajiona mjinga mwenye shahada ya upumbavu!

‘ Yupo ndani…’ Mama Nyanza alimuelewa akamrahisishia  njia lakini bado hakunyanyua miguu yake kupiga hata hatua moja kuukaribia mlango wa nyumba ya mjane yule. Angevunja miiko, haikuwa desturi kuingia nyumbani kwa mwanaume ambaye hajakuoa ila mwenye kujulikana kuwa angelikuoa siku moja. Akazubaa tena palepale akiomba huruma ya mama Nyanza ambaye sasa alimtazama Sindi katika namna isiyoeleweka.

‘Sidhani kama atataka kukuona’ Mama Nyanza akamkata Sindi maini
‘Kwanini?’ akazungumza neno la kwanza tangu afike pale na mama Nyanza akamtazama tu kwa jicho kali kidogo na kuinama, akichochea tena kuni zake

‘Sijamtendea kitu mama….sijamuumiza Nyanza na sitarajii kumuumiza’ Sindi alijitetea
‘Naomba uendoke Sindi…. imetosha sasa… Nyanza anahitaji mwanamke mwenye maadili na anayejua thamani yake….’ Mama nyanza alisimama tena na kuongea kwa msisitizo.

Sindi akawayawaya, akalengwa na machozi, akatamani kuangua kilio kilichokwamia kooni. Alikuwa anajua fika mama Nyanza hakuwa anampenda, alikuwa analijua hili tangu alipoanza uhusiano na Nyanza. alijitahidi mno kumshawishi mama huyu japo amchukulie chanya na mkamwana bora lakini haikuwa hivyo. Mama Nyanza  hakuonyesha kumkubali hata kidogo. Daima alimwambia mtoto wake kuwa Sindi Nalela alikuwa si mwanamke wa kukaa naye kwani angempa jakamoyo na maisha ya wasiwasi kutokana na uzuri wake na kule kufuatwa fuatwa na wanaume, lakini Nyanza aliponusurika mara kadhaa kulala polisi au kuumizwa katika ugomvi uliosababishwa na Sindi. Mama Nyanza alihitimisha kuwa Sindi hakumfaa mwanawe!

Machozi yakamporomoka Sindi hali akimtazama mama Nyanza namna alivyokuwa akijishughulisha pasipo kujali uwepo wake pale.
‘Naomba nimuone tu mama…’ alirai kwa sauti ya kubembeleza huruma ya mama Nyanza ambaye aliacha kujishughulisha na kumtazama tena Sindi.

Kama mtu anayetafakari, mama Nyanza alikazia macho Sindi kwa sekunde kadhaa kisha akageuka na kumuita Nyanza mara kadhaa. Nyanza akatoka mpaka mlangoni. Sindi akamtazama kwa huruma machozi yakimjaa tena machozi na kuporomoka. Akateremka chini taratibu na kupiga magoti palepale nje.

‘Nyanza….’ akaita kwa sauti hafifu midomo ikimtetemeka na Nyanza aliyekuwa amesimama mlangoni akataka kumfuata lakini mama yake akampa ishara ya kubaki pale pale.

‘Binti nenda nyumbani…’ mama Nyanza akatoa amri ambayo haikutekelezeka kwani Nyanza alikatilia mbali na kumfuata Sindi pale alipopiga magoti. Akamnyanyua na kumkumbatia mbele ya mama Nyanza ambaye alinyesha wazi kutofurahia hali ile.

Ni kama vile Nyanza alikuwa anangoja Sindi amfuate na waumalize mgogoro. Wakavutana pembeni na kushikana vizuri kimahaba, wakikumbatiana kwa nguvu zaidi.
‘Sitaki kuumia tena Sindi…. sitaki kupigana tena…niahadi wewe ni wangu’ Nyanza alitaka kuhakikishiwa kwa mara nyingine na asikumbuke ni mara ngapomaliomba kuhakikishiwa juu ya hili na akahakikishiwa.

‘….Nyanza kwanini huaniamini jamani….twende tukale kiapo chini ya ule mti pale kanisani labda utaniamini….’ Sindi alitoa wazo na sifikirie mara mbili
‘Kesho jioni twende….pengine nitakuwa na amani….nakupenda mpaka najihisi kuwa mwehu…’ Nyanza alimshikilia vema Sindi pale chini ya mti waliposimama

Wakaongea mengi ya wapendanao wakisuluhisha kilichotokea na Sidni akijaribu kumhakikishia Nyanza kuwa hakukuw ana wa kumtoa kwake.
wakati wakisindikizana, gari dogo aina ya Toyota corolla muundo wa zamani iliwapita taratibu na wao bila hofu walisimama kando na kuipisha. Gari lile liliendelea na safari na wao pasipo kujua aliyekuwa ndani ya lile gari ni Mzee Dunia, mwanaume aliyekwisha toa sehemu ya mahari ya sindi.

Walishikana mikono wakiendelea na safari yao hali kadhalika Mzee Dunia akiwatazama kupitia kioo na kukunja uso. Mwanamke mrembo aliyekuwa ameshikwa mkono alikuwa Sindi, mkewe mtarajiwa. Ghadhabu zilimmendea taratibu…


…….TUKUTANE TENA HAPAHAPA TUJAZANE NINI KILIFUATA?..... USIKOSE KUIFUATILIA TAMTHILIYA HII….LETA MAONI YAKO MSOMAJI

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger