Tuesday, April 30, 2013

SINDI.....NA LAURA PETTIE (11)

11

Pazia jepesi lililojaa matundu yaliyotosha kuigeuza pazia ile kuwa kama nyavu ya kuvulia samaki, ilipepea dirishani na kuruhusu hewa safi iliyosukumwa na upepo ipenye kwa mapana na kumfikia Sindi Nalela pale kitandani alipokuwa amejilaza chali, akili yake ikiwa imekimbilia kusikojulikana na kukiacha kichwa chake wazi mithili ya mtungi uliotoboka.

Macho yake yaliitazama  dari huku yakifumba na kufumbuka taratibu mithili ya mtu aliyekuwa akinyemelewa na usingizi. Alikuwa ametopea mawazoni kiasi cha kutojielewa sawasawa kwa wakati ule.



Roho ilimsuta na kumchonyota kisawasawa, alikuwa amefanya kitu ambacho hakuwahi kukifanya maishani mwake. Kuguswa na mwanaume mwingine zaidi ya Nyanza! Wakati roho yake ikimsuta lile tukio kati yake na Jerry lilipita akilini mwake kama marudio ya sinema na kumsisimua vibaya mno.

‘hapana…’ akajikuta akitamka kwa sauti, akili ikimrejea na kumuamrisha kutoka pale kitandani na kusimama katikati ya chumba chake cha kulala huku mikono ikiwa kiunoni. Alitembea tembea pale chumbani akijaribu kujiweka sawa lakini haikuwa vile alivyotaka. Shoti ndogo ya msisimko ilimpitia tena na akajikuta akirejea kukaa kitandani na kuketi kitako, akikipakata kichwa  chake mikononi mwake na kufumba macho kwa juhudi kubwa.

Ghafla akanyanyuka tena akiwa amejaa hamaniko lililomfanya aheme bila mpangilio. Kama mtu aliyekumbuka kitu, Sindi alipiga magoti mbele ya kitanda chake, viwiko vya mikono yake vikiegemea katika kitanda na viganja vyake kukutana pamoja mbele ya uso wake, akashusha pumzi ndefu na kufumba macho!

‘…Mungu baba najua nimekosa….najua nimekukosea na nimemkosea mchumba wangu Nyanza. Mungu… eeh Mungu….’ akasitasita akikosa cha kusema zaidi, midomo yake ilimwemweseka tu pasipo kutoa neno lingine na shetani akampitia na kumfumbua macho, akishindwa kuhitimisha sala yake na akajikuta akinyanyuka na kuketi tena kitako, akiwewesesha macho yake, asijielewe asijitambue!

Wakati Sindi akihamanika peke yake, Jerry naye alikuwa ameketi kitandani. Kitabu kilichokuwa mikononi mwake kikiwa kama pambo. Uso wake ulikuwa na hali ya kukosa utulivu hali macho yake yakipepesa na kuchezacheza mithili ya mtu aliyekuwa akizungumza na mwenyewe mawazoni mwake.

‘Sindi…’ akaita taratibu na kuteremsha pumzi. Simu aliyopewa na Pamela ilikuwa juu ya meza ndogo kando ya kitanda alichokuwa ameketi. Mlio wa simu ile ndio uliomtoa mawazoni. Akaharakia kuichukua na kubonyeza kitufe cha kupokelea baada kukitazama kioo cha simu na kumtambua mpigaji.

‘Hallow…’ akaipokea ile simu
‘Sema Jerry….umefikia wapi?’ sauti tamu ya Pamela ilimfanya atabasamu kidogo na kuinua ule mkono uliokuwa na kitabu, akakiweka mezani na kujitelezesha taratibu akijilaza chali.

‘Nimemtafuta Meddy aisee….kasema ndani ya wiki mbili nitakuwa na sehemu salama ya kuishi na kufuatilia zaidi’ Jerry alijibu na kuusikilizia upande wa pili.
‘Ooookay!....cant wait to see you here…and… wait…’ Pamela alikatisha maongezi na akasikika akiongea na mtu pembeni yake, na Pamela akalalamika kimahaba akimtaka huyo aliyefanya akatishe maongezi asimtekenye.

Jerry akafumba macho kwa na kuyafinya kwa nguvu kidogo, wivu ukimtekenya moyo na kumuamshia hisia za uchungu.
‘Jerry..’ Pamela akarudi hewani
‘Pam…’ Jerry akaita kwa sauti iliyojaa wahaka
‘Yes dear…kuna tatizo?’ Pamela akauliza kawaida asijue ni kwa kiasi gani alimuumiza Jerry
‘Uko na Patrick si ndio?’ Jerry akauliza sauti yake ikionyesha kukosa uvumilivu
‘Come on Jerry…. Pat and me have been dating for almost a year now…and you know it’ Pamela akajitetea
‘Why are you doing this to me Pam?’ Jerry akauliza kiunyenyekevu huku akisikilizia maumivu ya wivu
‘I’m your bestfriend na nimeshakwambia hili mara elfu moja zaidi…. ‘ Pam akajibu kwa sauti iliyoshiria hakutaka kusikiwa na yule aliyekuwa naye.
‘na hujali hisia zangu…unanipigia simu ukiwa na mwanaume mwingine na bado unasikilizisha mnayoyafanya sio’ Jerry akalalamika zaidi

‘…umechukulia vibaya Jerry….hukutakiwa kusikia ulichosikia…I’m sorry!.... and how are things there?’ Pamela akamtaka radhi na kubadili mada haraka sana. Jerry hakujibu, akakata simu na kuirushia pembeni ya kitanda. Sekunde mbili zilipokatika simu ile ilianza kuita tena na mpigaji alikuwa Pamela.

Jerry akainyakuwa simu na kuitazama tua pasipo kuipokea. Simu ikaita kwa muda na kukatwa. Jerry akaiweka kifuani na kutulia kwanza. Moyo wake ulikuwa na hekaheka ya ajabu mno. Kiherehere cha moyo kilimfika na amani aliyokuwa nayo ikachukuliwa mateka. Mlio wa meseji ukasikika, Jerry akainyanyua simu na kuufungua ule ujumbe.

‘….Unanikasirikia bure Jerry I know you love me lakini bado mimi ni rafiki tu kwako, anyway ukija tutaongea zaidi. Love you’ aliusoma ule ujumbe kimya kimya na kutikisa kichwa.

Haikuwa mara ya kwanza kukutana na vitimbi kama hivi lakini alivivumilia akijipa matumaini ipo siku Pamella angemuelewa na angekubali kuwa wake wa maisha. Alitabasamu kwa huzuni na kujisikitikia tena na tena. Mwisho akanyanyuka toka pale kitandani na kutoka mule chumbani, akijumuika na familia ya Mwenyekiti wa kijiji kwa mlo wa usiku.
88888888888888888888

MIAKA MITATU ILIYOPITA
Ndani ya hospitali ya misheni ya Imakulata, mwanamke mwenye afya dhohofu alikuwa kitandani akionekana kuwa na maumivu makali mno. Jasho lilikuwa likimtoka kwa fujo na kuweweseka. Sophia Agapela alikuwa kitandani pale akiugulia ugonjwa ambao hakuna aliyeujua mpaka dakika ile licha ya vipimo vyote kufanyika.

Machozi yalimchuruzika pembezoi mwa kona za macho yake wakati akilalamikia maumivu aliyokuwa anayasikia mwili mzima.
‘Jeni….Jeni…niitie baba yako’ alizungumza kwa taabu akiwa amemshikilia binti yake kwa nguvu nyingi. Jenifa binti yake wa mwisho akamtazama mama yake kwa uchungu naye akifuta machozi.

‘Niitie Kristus wangu…Kristus…’ alizungumza akihema kwa taabu zaidi na akiuma meno kwa maumivu na macho yake yakionekana kukosa nguvu ya kumudu kumtazama Jenifa ambaye alimtazama mama yake pasipo kumjibu, alikuwa akiisikia kauli hii kila siku, kila muda na kila wakati aliokaa na mama yake pale hospitali.

Siku hii ya leo ombi la mama yake lilizidi, aligoma kunywa hata maji akitaka aitiwe mumewe Mzee Kristus Agapela. Jenifa aliumia zaidi kwa vile alikuwa anajua ombi lile lisingetimia pamoja na kule kugoma kula na kupiga kelele za kuitiwa mumewe.

Manesi waliokuwa wakimhudumia walimuita Jenifa pembeni na kumsihi akamtafute baba yake na kumleta.
‘Hawezi kuja jamani…..nimeshamfuata sana, ananifukuza kama mwizi….najua hawezi kuja… hawezi’ jenifa aliongea huku akilia kwa kwikwi
‘basi mpigie simu umwambie hali ya leo ilivyo….mwambie amegoma kula, hataki dawa wala hatulii ni fujo mtindo mmoja’ nesi mmoja mtu mzima akamshauri Jenifa ambaye alikuwa akifuta machozi kila dakika.

Pale pale Jenifa akatoa simu yake na kumpigia baba yake, Simu ile iliita kwa muda pasipo kupokelewa na ilipopigwa mara ya pili simu ikakatwa haraka sana. Ukimya ukapita kati yao kwanza kila mtu akiwa ameduwaa. Yule nesi mtu mzima akaichukua simu ya Jenifa na kupiga namba za Mzee Agapela kwa kutumia simu yake, ikaita mara mbili tu na kupokelewa

‘Hallow…’ sauti nzito ya  Mzee Agapela ikasikika
‘hali ya mke wako si nzuri…kuwa na utu angalau ufike…’ yule nesi akakatizwa
‘Who the hell are you?’ akauliza Mzee Agapela kwa ukali
‘Mimi ni nesi namhudumia mkeo hapa hospitali…Mzee hali ya mkeo si nzuri kabisa’
‘Sasa mimi nikija ndio atapona au?...’ akauliza kwa kejeli

‘anakuhitaji... na kiubinadamu huyu ni mkeo…na…’ akakatizwa tena
‘mkimaliza kazi yenu bili inalipwa kama kawaida….akifa mnamjua pa kumpeleka…haya mengine naomba sana msijaribu kuyaingilia hayawahusu’ Mzee Agapela akajibu na kukata simu, akiwaacha wale manesi na Jenifa wakitumbua macho kana kwamba waliamriwa kufanya vile kwa pamoja.

Wale manesi wakamtazama Jenifa kwa huzuni iliyochanganyikana na mshangao.
‘Mzee Agapela ni baba yako mzazi kabisa?’ nesi mmoja akauliza akionekana wazi kutoamini alichokisikia. Jenifa akaitikia kwa kichwa wakati yule nesi mtu mzima akimdaka  pia kwa swali

‘na huyu mama yako ni mkewe wa ndoa?’ Jenifa akaitikia tena kwa kichwa, akiwaacha hoi wale manesi
‘Wanaume!....’ nesi mwingine akashangaa zaidi huku akijinyanyua toka pale alipokuw ameketi na kusimama akijiandaa kuondoka

‘Mume si ndugu yako mwenzangu….hebu ona huyu mama anavyoadhirika jamani…. ndugu wengine wako wapi?’ Nesi yule aliyesimama akamhoji Jenifa
‘Mama hana ndugu…. kuna marafiki zake walikuwa wanakuja siku hizi siwaoni’ Jenifa akajibu akinyoosha shingo yake na kutazama mlangoni mwa kile chumba walichokuwemo. Manesi nao wakageuka kutazama kule alikotazama Jenifa.

Jerry Agapela alikuwa amesimama kwenye kizingiti cha mlango. Jenifa akamkimbilia na kumkumbatia kwa nguvu, akipata nguvu ya kulia tena akiwa kifuani kwa kaka yake. Jerry akajikaza na kumbembeleza mdogo wake a hapo hapo yule nesi mtu mzima akianza kuzungumza na Jerry.

Wakatoka na kurudi wodini alikolazwa mama yao. Jerry alipomkaribia mama yake alihisi nguvu zikimuishia. Alikuwa anazidi kudhoofika kupitiliza. Sophia alifumbua macho kwa taabu na alipomuona Jerry, akatabasamu kivivu huku macho yake yakijaa machozi kwa kasi ya ajabu.

‘Naumia…Jerry…’ akalalamika na kuita mwanawe
‘Naam mama..’ Jerry akamuinamia mama yake
‘Naumia….naumia…’ akalirdia neno hili mara kadhaa machozi yakizidi kumchuruzika.
‘Pole mama…’ Jerry akamjibu mama yake akijikaza kiume kiasi cha mishipa ya kichwa kumsimama.

‘Yuko wapi?....’ Sophia akauliza kwa sauti hafifu akijaribu kutabasamu katikati ya yale maumivu. Jerry akainamisha kichwa chini. hakuwa na jibu, hakuwa na la kumwambia mama yake, hakuwa na kusema kwa wakati ule. Sophia akapaza sauti na kuangua kulio ambacho kilileta kelele kidogo ndani ya chumba kile na ikabidi yule nesi na wenzake wamshike Sophia na kumlazimisha kutulia huku wakimchoma sindano ya usingizi ili atulie.

Jenifa na Jerry waliliona tukio lile na mioyo yao haikuvumilia kuendelea kuona hali ile. pamoja na uanaume wake, Jerry alilengwa na machozi, mishipa ya shingo ikimtutumka wakati alipojaribu kujizuia kulia.
‘hatuwezi kuendelea kumlewesha madawa ya usingizi kila siku….’ Nesi mtu mzima aliwaambia akina Jerry waliposimama nje ya chumba cha mgonjwa
‘na nini kitafuata sasa?’ Jerry akauliza kwa suati ya kukata tama

‘Anamuhitaji mumewe…baba yenu….hatujui nini kitafuata akishamuona lakini ni vema aje…amsikilize….vipimo vyote vilivyochukuliwa hakuna hata kimoja kinachoonyesha hata minyoo basi….hakuna!.....’ yule nesi aliongea kwa huzuni

‘Baba hawezi kuja…. hawezi….’ Jerry alijibu kwa simanzi akionyesha wazi kukata tama kwa hali ya mama yake
‘Hivi yuko Dar es salaam hii hii kweli?’ yule nesi aliuliza kwa mashaka na watoto wa Sophia wakajibu kwa kuitikia kichwa. Nesi akashusha pumzi na kuwatazama hawa ndugu wawili katika namna ya kutamani kuwasaidia na asijue awasaidie vipi.

Akaagana nao na kuwaacha wenyewe kwanza. Wakatoka nje na kwenda kuketi sehemu iliyokuwa na bustani ya kupumzikia. Jenifa alilia kwa uchungu na kwa hasira pia, akimtazama kaka yake kama tumaini pekee lililobaki maishani mwake
‘Jeni…it is gonna be okay…. mama atapona and… and…’ alikwamia hapo, akishindwa kuhimili donge lililomkaba kooni na kumfanya atiririkwe na machozi. Wakakumbatiana na kulia kwanza, wakishindwa hata kufarijiana.

Familia yao ilikuwa imeparaganyika. Baba yao alikuwa amewafukuza nyumbani kwao na hivyo Sophia na wanawe walikuwa wakiishi chumba kimoja mitaa ya kinondoni. Jerry alikuwa amemaliza chuo na harakati za kutafuta kazi zilikuwa zimepamba moto. Jenifa alikuwa ameishia kidato cha tano baada ya baba yake kutomlipia karo.

Mwaka mmoja tangu ndoa yake iingiliwe na Fiona na kisha Sophia kufukuzwa, Sophia alianza kwa kuchanganyikiwa kisha kuanza kuumwa ugonjwa usioeleweka. Miezi sita tu ilitosha kumkongorosha na kubaki mifupa mitupu. Mumewe alifika mara moja tu ndani ya hiyo miezi sita akimlipia bili ya matibabu pekee baada ya kikao cha wanandugu kumlazimisha kufanya hivyo.

Sophia hakuwa na ndugu, mtu pekee aliyekuwa kama ndugu yake alikuwa ni mumewe aliyemchukua toka katika kituo cha watoto yatima na kumuajiri kama mfanyakazi wa ndani na baadaye akajikuta akimpenda na kumuoa.
Jerry na Jenifa waliishi maisha magumu mno, wakitegemea vibarua vya Jerry hapa na pale na misaada kidogo ya ndugu. Kuna wakati walilala njaa, kuna wakati mgonjwa wao alitegemea makombo ya wagonjwa wenzake ili asilale njaa.

 Ni bili tu ndio iliyolipwa na Mzee Agapela, mengine yote yaliyobaki hayakumhusu. Sophia aliteseka sana na aliumia zaidi alipowatazama watoto wake waliopeana zamu kumhudumia yeye huku mumewe akila maisha na mwanamke mwingine. Mwanamke ambaye yeye Sophia alimuita rafiki!


.......NIPE MAONI YAKO MPENZI MSOMAJI.....

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger