Wednesday, April 10, 2013

SINDI.... NA LAURA PETTIE(5)

5

SEHEMU YA TANO

Jua la asubuhi lilichomoza taratibu kwa miale hafifu huku  miale hiyo ikisindikizwa na mvua za rasharasha zilizoanza alfajiri ya siku hiyo. Upepo mdogo uliokuwa ukivuma kwa mbwembwe uliiyumbisha miti iliyotapakaa kijijini hapo. 

Watu wachache walionekana wakikimbia huku na kule wakikatisha katika ile mvua ya rasharasha na  wanakijiji wengi walijifungia ndani kwanza kuipisha ile mvua huku wachache wengine waliojihimu mashambani wakiendelea na kilimo kama kawaida.


Sindi Nalela alikuwa akiandaa chai jikoni, jiko la kuni alilokuwa akilitumia lilitoa moshi mwingi uliomfanya afikiche  macho na kukohoa kila alipoinama na kupuliza zile kuni zilizobebana katikati ya mafiga.
‘Kuni mbichi Sindi….kwanini usingewasha zile zilizoko nyuma ya mlango?’ Mama yake aliyekuwa anaingia pale jikoni alimsemesha Sindi baada ya kukutana na moshi umetapakaa na kuleta hali ya kukera

‘za nyuma ya mlango ndio hizi mama…’ akajibu akimtazama mama yake kwa taabu kidogo sababu ya moshi
‘Mmh…ndio zimeloa hivi?’ mama akauliza kwa mshangao
‘Sehemu ya bati hapo nyuma ya mlango inavuja’ Sindi akajibu akitoka pale jikoni na kupishana na mama yake mlangoni. Akafungua mlango wa nje na kusimama kizingiti cha mlango akitazama nje kama mtu anayemtafuta mtu. Mvua ile ya rasha rasha ilimzuia kusogeza kichwa mbele zaidi hivyo kutoona umbali aliotaka kuona.

Akiwa hapo mama yake naye akamfuata hapo kizingitini, akichungulia kule alikokuwa anachungulia Sindi.
‘kuna nini uko?’ Mama akauliza
‘Nilimtuma Peter mihogo kule chini naona muda unaenda tu’ akalalamika Sindi
‘Na mvua yote hii unamtuma Peter uko chini…’akaulizwa
‘Mama jamani…mbona huwa namtuma kila mara’ akajitetea

‘Nazungumzia mvua Sindi…. unamjua Peter ni mgonjwa wa kifua alitakiwa awe ndani  muda huu….hebu acha upumbavu mfuate mtoto uko ulikomtuma’ mama Sindi aliongea kwa hasira na Sindi alitoka  na kujitosa kwenye ile mvua. Akiwa amenyanyua mabega yake juu akipambana na baridi.

Ni kama vile Manyunyu yale yalikuwa yanamngoja Sindi alijitose kimiani. Kasi ya manyunyu iliongezeka na kufanya mvua kamili ya kusimamisha shughuli zote. Sindi alitembea katikati ya mvua ile akipaza sauti yake na kuliita jina la Peter. Alivuka nyumba kadhaa akimuulizia mdogo wake. Nyumba ya sita toka pale kwao ndio sehemu aliyomtuma Peter.

‘Aliondoka saa nyingi sana yaani kabla hata ya hii mvua kuanza….atakuwa kwa rafiki yake Mbwana maana ndio alikuwa ameongozana naye’ Mama muuza mihogo alimpa Sindi mwanzo wa safari nyingine. Sindi akashukuru na hapo hapo akisonya na kujenga ndita za kuonyesha kukereka zaidi na kule kutembea katika mvua akimsaka Peter.
 Aliumaliza mtaa wao na kuingia mtaa wa pili sasa kwa kuvuka barabara, nyumba ya tatu toka barabarani ilikuwa nyumba ya mwenyekiti na nyumba ya jirani ndio ilikuwa nyumbani kwa huyo Mbwana rafikiye Peter.

Alipoivuka nyumba ya Mwenyekiti na kuikaribia ile nyumba aliyokuwa anaelekea alisikia jina lake likiitwa. Hakugeuka alichapa mwendo akikimbia mpaka kwenye ile nyumba. Akasimama mlangoni akikausha uso kwa mikono na kukamua khanga yale iliyokuwa imelowa.

‘Sindi….umemfuata Peter?’ sauti toka ndani ilimuuliza wakati akikamua ile khanga yake ambayo hata hivyo bado ilikuwa mwilini mwake.
‘eeh… yupo?’ akauliza akikung’uta mikono yake
‘Peteeer… Mbwana hebu muite Peter uko uani….mwambie Sindi amemfuata’ sauti ile iliagiza na Sindi hakuona sababu ya kuingia ndani mule ndani  akasimama pale pale nje akimngoja mdogo wake.

‘Mama hajambo lakini?’ sauti toka ndani ikamhoji
‘Hajambo…’ Sindi akajibu akiugeuzia uso mlangoni kule ili muulizaji alipate jibu kwa urahisi. Akiwa amesimama pale kwa takribani dakika moja nzima Sindi alionyesha hali zote za kukereka lakini alishindwa kujitosa mule ndani na kwenda kumvuta Peter ili amtoe nje.

Sura yake iliyokuwa imejaa makunyanzi ya hasira huku misonyo midogo midogo ya hasira ikimtoka, ilikunjuka ghafla na kuvaa tabasamu. Jerry Agapela alikuwa akija sehemu ile aliyokuwa amesimama. Alipomkaribia Sindi alijikuta akitabasamu zaidi kiasi cha kuonyesha meno yake yaliyokuwa katika safu nzuri ya kuvutia, mwanya mdogo uliochongeka kiustadi ukizidisha thamani ya lile tabasamu pana la kuvutia.

‘umelowa sana…’ Jerry alimsemesha wakati alipomfikia na kusimama mbele yake akiwa na mwamvuli mkubwa alioushikilia mkononi.
‘Si Peter huyo….nxa!’ akalalamika na kumfanya Jerry acheke
‘Mtoto ni mtoto tu….’ akamtetea
‘Peter naye mtoto aargh!...’ akabetua midomo yake na Jerry akacheka chini chini.

Wakatazamana na ukimya ukapita kati yao, ukimya wa ghafla tu kila mtu akikosa cha kuongea. Sindi akaamua kujibaraguza kwa kumuita Peter kwa sauti kubwa na bahati ikawa yake. Peter aliitika akidai anakuja.
‘Sindi…’ Jerry aliita kwa sauti ya chini. Sauti ambayo kwa  mwanamke yoyote yule lazima mwili ungemsisimka kidogo. Sindi akajibaraguza zaidi kwa kuamua kuushika mlango uliokuwa mbele yake na kuufungua, akichungulia ndani na kumhimiza Peter afanye haraka.

Sindi aliutanua mlango zaidi na Peter akatoka, akipokelewa na konzi matata toka kwa dada yake.
‘Usimpige jamani…’Jerry alimtetea Peter ambaye alisharuka na kusimama kule alikokuwa amesimama Jerry. Ukatokea mvutano kati ya Peter na Sindi huku Jerry akiwa katikati. Mvutano huo ukaisha kwa Jerry kumuombea Peter msamaha.

Kwa vile mvua ilikuwa inaendelea kunyesha, Jerry alijitolea kuwasindikiza kwa kutumia mwamvuli aliokuwa nao. Wakabanana katika mwamvuli ule wakikatiza kona kadhaa hadi kufika nyumbani kwa akina Sindi.  Wakashukuru na Peter akawa wa kwanza kukimbilia ndani na mfuko wake wa mihogo wakati Sindi akiagana na Jerry.
‘utaenda kufundisha kule chini…’ Jerry akauliza taratibu wakati akiagana na Sindi ambaye aliitikia kwa kichwa na kutoka katika ule mwamvuli. Akampungia Jerry mkono na kuingia ndani. Jerry akageuza njia na kurudi alikotoka. Uso ukiwa na tabasamu la matumaini aliyoanza kujenga moyoni mwake.

‘teeena?’ mama yake akamdaka kule ndani
‘Tena nini?’ Sindi akauliza kwa mshangao
‘huyo kijana mnavyozungushana hapa kijijini….. hivi mwanangu huoni picha mbaya unayojengewa?’ Mama yake akalalamika
‘Jamani….hao wajenga picha sasa wajenge tu hata ghorofa la tuhuma … katusindikiza hapa sababu ya mvua…watu mnawaza mengine kabisa…. nimechoka na maneno ya watu sasa…waseme tu’ Sindi akajibu na kupilizia chumbani kwake

Wakati alipoufunga mlango wa chumba chake, Peter aliyekuwa amesimama pembeni ya mama yake aliutazama ule mlango wa chumba cha Sindi kwa tahadhari kisha akamvutia chini mama yake ili usawa wa kichwa cha mama yake ulingane na wake.
‘Kamtomasa tomasa…’ akasema haraka haraka kwa sauti ya chini
‘Nini?...nani katomasa’ mama yake akauliza kwa sauti iliyomfanya ajishtukie na kupunguza sauti, akimtazama mtoto wake kwa mshangao si tu kwa lile neno alilotamka Peter bali ni ile picha iliyomjia ghafla kichwani.

‘Jerry kamtomasa Sindi huku….’ Peter akaonyesha ubavu wake
‘Kamtomasaje?’ safari hii mama aliuliza kwa sauti ya chini zaidi, macho yakiwa yamemtoka vibaya mno.

‘wakati tunatembea wametomasana’ Peter akajibu, uso ukimaanisha kile alichokuwa anakisema. Mama Sindi akanyanyuka na kusimama wima, mshangao, taharuki na hali ya kutoamini vikimtembelea kwa wakati mmoja na muda huo huo mumewe akifungua mlango wa kuingilia ndani huku akiwa ametanguliza majembe. Mama Sindi akajitoa katika ule mshangao na kwenda kumpokea mumewe. Akili yake haikuwa pale tena, alihisi hatari ambayo hakutaka hata kuiwazia namna ambavyo ingeleta majanga pale kwake ila kwa wakati ule, damu ilimchemka!
88888888888888888888

Gari dogo aina Suzuki Vitara ilitembea kwa mwendo wa taratibu upande wa pili wa dunia, mjini huku, jua lililokimbia kijijini kule lilihamia huku mjini. Gari lile liliacha njia ya lami na kuchukua njia ya vumbi iliyoishia katika nyumba moja iliyoonekana kutomaliziwa kujengwa kitambo. Mwanamke aliyevalia maridadi aliteremka kwa kasi na akiwa amejifunika ushungi na kuzama katika ile nyumba akionekana mwenye wasiwasi kupitiliza. alitembea kwa shida kidogo kutokana na sakafu ya ile nyumba kuwa yenye mawe na mchanga. Viatu vyake virefu vilivyombeba kiustadi havikuhimili mabonde mabonde yaliyokuwa katika ile sakafu. Mara kadhaa alilazimika kujishikilia ukutani wakati akikatiza chumba hadi chumba mpaka alipotekezea katika sehemu ya nyuma ya nyumba iliyokuwa wazi.

Alitulia pale akiangaza angaza huku na kule, uso wake uliojaa mashaka ukiongeza ndita kadhaa. Aliporidhika na hali ya usalama alioutaka. Mwanamke yule alipiga mbija moja kali na kutulia, akingoja jibu la ile ishara iliyotoa. Wakati huo akitazama pori dogo lilikokuwa mbele yake. Alitulia kimashaka mashaka mpaka pale vijana wanne wenye miili iliyoshiba walipojitokeza na kumfuata pale alipokuwa amesimama.

‘imekuwaje?.....nilisema yasifanyike makosa ya aina yoyote….na hiki ni nini….waliokota kiatu kiatu na sasa wallet yake imeokotwa…hamuoni itawapa njia ya kumpata?’ alifoka kwa ghadhabu akiwatazama wale wanaume
‘nimetoka milioni 5 za kumteka Jerry na kumuua kimya kimya…..sio kumteka na kumuachia….hebu ona mipango yote imeharibika…..ujinga gani huu?’ aliendelea kufoka

‘Lakini dada  tuna hakika Jerry hatakuwa mzima mpaka dakika hii..’ kiongozi wao alijitetea
‘Una uhakika gani?....hii sio sandakalawe Jimmy….sio mchezo wa pata potea….trace ndogo tu inaweza kugharimu maisha yangu….’ yule mwanamke alihamanika akiwa tazama wale vijana kwa wahaka

‘Alikokimbilia ni porini na jeraha lile la kisu si la kumuweka duniani mpaka sasa….wataokota maiti sio mtu aliye hai… tuamini sisi…ndio tuliopambana naye…inshu ni kungoja iokotwe maiti vinginevyo jua maiti inaozea porini uko….ila la Jerry kuwa mzima sahau kabisa’ Yule kiongozi alijitetea na wenzake wakiitikia kwa kichwa.

‘Vipi kuhusu usiri wa hiki kitu?’ yule mwanamke alitaka uhakika
‘Hii sio kazi yetu ya kwanza Mama….weka imani na sisi na ukisikia popote tuhuma zozote nifuate’ alihakikishiwa na akabaki kuwatazama wale vijana kana kwamba moyo wake ulisita kuwaamini.

Fiona Agapela, mke wa Mzee Agapela alifungua pochi yake aliyokuwa ameibana kwapani na kutoa burungutu la fedha ambazo hakuzihesabu. Aliwakabidhi wale vijana  na wao pasipo kuhesabu walizitia kibindoni. Waliaminiana!

Fiona alitoka eneo lile na kurudi garini, aliingia ndani ya gari na kutulia kwa sekunde kadhaa pasipo kuendesha wala kuugusa usukukani. Alitulia tu akiutazama usukani pasipo kuutambua akilini. Alikuwa na jakamoyo lililomtokota  kwa wakati ule. Moyo wake uligoma kuamini kuwa hatua ya mwanzo ya mpango wake ulikuwa umefanikiwa.

Aliitaka maiti ya Jerry, alitaka kumzika na kulishuhudia kaburi lake ndipo moyo wake ungetulia kwa amani. Akashusha pumzi taratibu, mkono wa kushoto ukishika usukani na ule wa kulia ukitekenya ufunguo, akaliwasha gari, akigeuka nyuma kuangalia akianza kulirudisha nyuma taratibu.

Alitabasamu alipoliingiza gari lake kwenye barabara ya lami.
888888888888888888888888

Nyanza alijitazama mara mbilimbili wakati alipokuwa akijiandaa kutoka nyumbani kwao. Jioni hii alipanga kukutana na Sindi kwenye makutano yao. Pesa kidogo aliyokuwa nayo alimnunulia Sindi doti ya khanga aliyokuwa ameihifadhi kwenye mfuko mdogo mweusi wa nailoni.

Ijapokuwa shati lake lilikuwa limejikunja kiasi cha kuchekesha, lilimkaa vyema mwilini, na kulandana na suruali ya kitambaa iliyokuwa imepauka kiasi kuishia juu kidogo ya viatu chakavu aina ya mokasi alivyokuwa amevaa.

Nyanza alitoka pale kwao mpaka eneo alilotarajia kumkuta Sindi. Akatulia hapo akiifurahia mandhari tulivu iliyokuwa mbele yake huku akimngoja Sindi wake.

Pasipo kukumbuka miadi yake na Nyanza, Sindi alimalizia darasa lake na kusimama nje ya lile jengo alilolitumia kama darasa akizungumza na Jerry Agapela.
‘Kwani ukimpenda mtu lazima uwe naye….’ Sindi alibisha akiwa amekumbatia vitabu vyake kifuani
‘Sio lazima lakini….lazima utapigania kumpata tu’ Jerry alijitetea
‘Nimeshakwambia nina mtu’ Sindi alikaza uzi
‘Najua… na mimi sio mbuzi ni mtu….’ Jerry alipagua hoja ya Sindi akimsogelea zaidi
‘Sitaki…siwezi kuwa na watu wawili kwa wakati mmoja….’ Sindi alirudi nyuma kidogo na kuanza kupiga hatua za kuondoka eneo lile na Jerry akamkimbilia na kuanza kutembea naye sambamba

‘Sindi…’ akamuita, akimuwahi na kumzibia njia
‘Nakupenda…’ akatamka kwa sauti ya chini lakini iliyomfikia Sindi mpaka mtimani. alikuwa na namna ya kulitamka jina la Sindi kimahaba zaidi.
‘Sitaki Jerry’ Sindi akampita Jerry tena akikaza mwendo na Jerry alijua Sindi alitaka kumuacha njia panda. Ile ishara ya kumtekenya ubavuni wakati alipokuwa amewafunika na mwamvuli ilipokelewa na Sindi kwa hali tofauti. Hakuutoa mkono wake pale alipompapasa lakini pia hakumuonyesha dalili za kuikubali hali ilea ma tu kumkubali kama alivyokubali kupapaswa.

Walibishana njiani, wakijibizana na Jerry akipangua hoja za Sindi kila alipomkatalia alilotaka
‘Sitaki sawa?.... nnajiheshimu Jerry…achana na mimi’ Sindi alikuwa mkali sasa, akimjibu kwa sauti kali na yenye mamlaka
‘Najua u bikira’ Jerry akatamka kwa kujiamini na kumfanya Sindi asimame ghafla na kumgeukia Jerry

‘Nini?...umesemaje?’ Sindi akauliza kwa ukali
‘Najua wewe ni bikira’ Jerry akarudia tena na kabla hajatuliza kichwa chake akashtukia akipokea kibao kikali shavuni, kilimfanya aone nyota kadhaa za rangi tofauti
‘Usirudie kuniambia upuuzi kama huu….’ Sindi alionya na kuondoka kwa kasi zaidi. kofi la mpenzi haliumi!

Jerry alimfuata Sindi kwa kasi zaidi na kumzuia kwa mbele, akijitoa mhanga na kuitanua mikono yakekumgusa Sondi ambaye aliipangua kwa kasi.
‘Usinishike Jerry’ alimuonya
‘Nakutaka Sindi…’ Jerry alibembeleza na hapo hapo akitumia nguvu kidogo kumsogelea Sindi ambaye naye alikuwa akirudi nyuma taratibu. Macho yake hayakuweza kumtazama Jerry kwa ukali ule ule. Ni kama vile maneno ya Jerry yalimpunguzia nguvu.

‘Nakupenda sindi…. nakutaka…’ alirai kimahaba akiwa ameshamfikia Sindi na kutaka kumgusa tena. Sindi aliyekuwa amegota kwenye mti uliokuwa nyuma yake alihema bila mpango midomo ikimwemweseka pasipo kukemea.

kufumba na kufumbua, Jerry alihisi akitupwa kando kwa nguvu. Wakati akili yake ikikaa sawasawa na kutaka kutambua kilichomsukumia mbali vile, alishtukia ngumi ya shavu ikimpata sawia na hapo hapo akitandikwa ngumi ya mbavu iliyomfanya apepesuke na kudondoka tena kama gunia la mpunga.

Sindi alipiga yowe la uchungu, akimtaka Nyanza kuaca kupigana. Haikusaidia Nyanza alimtandika Jerry ngumi za kutosha kabla ya kumuachia na kumgeukia SIndi ambaye alirudi nyuma kwa kasi na asitazame aendako.

Nyanza akampita taratibu, akiokota ule mzigo wake wa Khanga na kutokomea, akimuacha Sindi amesimama katikati asijue akamsaidie Jerry au amkimbilie Nyanza.


……. TUKUTANE TENA HAPA HAPA…….

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger