Friday, April 26, 2013

SINDI....NA LAURA PETTIE (10)

10
SEHEMU YA 10


Asubuhi ya Siku iliyofuata Pamela Okello aliondoka na gari lake alilokuwa amekodi mahali uko Shinyanga mjini, akiwa amemuachia Jerry Agapela pesa za kutosha pamoja na simu ya mawasiliano. Wakati anaondoka pale kijijini alimkumbuka Nyanzambe Mugilagila, kijana aliyeonana naye jana yake na kumnasua toka katika zahma la kukwama matopeni.

Moyo wake ulitaka kumuona tena kijana huyu, alitaka tena kuisikia ile lafudhi nzito ya kiume iliyomchangamsha jana yake, alitaka tena kukiona kiumbe hiki na nafsi yake haikumpa hata nafasi ya kuipuuzia hamu yake ya kumtia machoni. Akaegesha gari palepale alipoegesha jana yake na kuteremka.



Hatua mbili tatu zilimfikisha katika kibanda kidogo kilichokuwa kikitumika kama sehemu ya kutengenezea baiskeli. Waliokuwepo eneo hilo hawakuingia hata nusu ya hadhi ya mtu aliyetaka kumuuliza. Akatulia kidogo akiwatazama na wale aliowakuta wakimshangaa.
‘Namtafuta Nyanzambe’ akatoa shida yake asijali uungwana wa kujuliana hali kwanza na hakuna aliyemjibu. Lafudhi yake laini iliyorembwa kwa sauti maridadi iliwafanya watazamane kwanza na kusemezana kilugha. Naye Pamela akawatazama kwa  awamu akikunja uso kidogo kuonyesha kutowaelewa.

Wakasemezana na kucheka kisha wakamgeukia Pamela, wakizidi kumshangaa sio tu kwa yale mavazi yake bali pia kwa ule umaridadi wake ambao haukulingana hata theluthi na huyo aliyemuhitaji.

Pamela akazungusha macho katika namna ya kuonyesha kuchoshwa na zile mbwembwe zao na mishangao yao wale mafundi baiskeli. Akasonya na kugeuka akitaka kuanza kuondoka lakini uko alikogeukia ndiko huyo aliyekuwa anamtafuta alikuwa anatokea, akiwa na baiskeli yake akiikokota taratibu huku ikiwa na magunia makubwa mawili ya mkaa.

Pamela akatabasamu na kusimama akingoja Nyanza amfikie pale alipokuwa
‘Pole!’ likamtoka hili neno pengine bila kutarajia, macho yakikisawiri kifua kipana cha Nyanza kwa matamanio. Nyanza akatabasamu akishika baiskeli ile kwa mkono mmoja na mwingine akinyanyua baiskeli kwa nyuma na kuiweke breki yake ya kusimamia.

‘Unaondoka?’ akamuuliza Pamela akitanua mikono yake hewani
‘Yeah….nilitaka kukuaga na kukushukuru tena na tena’ Pamela akaeleza nia yake na Nyanza akatabasamu tu kwani moyoni hakuona umuhimu wa msichana kama yule kuhangaika kumtafuta ili kumshukuru tu.

‘Unaishi wapi?’ Pamela akauliza tena lakini Nyanza akainamisha kichwa chini akitoa tabasamu lililomfikishia ujumbe Pamela kuwa hakutaka kumfikisha anapoishi.
‘Okay…usijali’ Pamela akaligundua hilo
‘Safari njema…’ Nyanza akamuaga pasipo kuondoka wala kuonyesha dalili za kuondoka. Ni kama alitaka kuhitimisha mazungumzo na mwanadada yule kwa wakati ule.

Pamela Okello akaganda kama sanamu akimtazama Nyanza ambaye alijikuta akitaka kucheka pia kutokana na wale mafundi baiskeli kusimama wima wakiwasikiliza kana kwamba waliambiwa wakariri kila watakalosikia.

Tendo lile la kutaka kucheka hali akitazama walionyuma ya Pamela, lilimfanya Pamela ageuke na kutanza hicho alichotazama Nyanza. Wale mafundi wakajibaraguza kushika hiki na kile na hilo likamfanya Nyanza acheke kwa sauti kidogo na angalau kumletea Pamela tabasamu la kulazimisha.

‘ Karibu tena dada…’ Nyanza akaaga tena akiikwatua breki ya baiskeli na kuiweka tayari kwa kuondoka.
Pamela Okello akaitikia kwa kichwa, huku moyo wake ukimshinikiza amwambie Nyanza wakaketi katika gari na kuzungumza, hakuweza kuyasema hayo, hakuweza hata kidogo, ugeni ulimsumbua na mazingira hayakumruhusu. Akashusha pumzi na kuondoka eneo lile kurejea kati ka gari lake. Akalondoa gari kwa kasi.

Nyanza akakipita kile kibanda akitaniwa na wale mafundi baiskeli, akapiga kona na kufika kwao. Kibanda kile kilikuwa mbele ya nyumba yao. Akaingia katika uwanja wa nyumba na kumkuta mama yake akivaa raba zake kwa ajili ya kwenda kazini.
‘leo umechelewa sana mama’ Nyanza akamsemesha mama yake huku akishusha yale magunia toka kwenye baiskeli
‘Nimekuona na mwanamke hapo nje’ mama yake akiwa na uso wa shari akamvaa mwanaye. Nyanza akashindwa kulitua lile gunia alilokuwa amebeba na akashindwa kulirejesha alikolitoa, akabaki ameduwaa nalo mikononi hali likimuelemea

‘Mama unanifuatilia!?’ Nyanza akamuuliza mama yake uso ukijikunja kutokana na ule uzito wa gunia la mkaa changanya na hali ya kumshangaa mama yake ambaye sasa alisimama wima mbele yake.
‘hebu tua hilo gunia kwanza khe!...’ mama yake akajibu na kumfanya Nyanza auweke chini ule mzigo na kusimama wima akimtazama mama yake kiudadisi
‘nina mwanamke mmoja tu maishani mwangu’ Nyanza akajitetea
‘Kwani nimesema unao kumi….na huyo mwanamke wa kumtambia hivi yuko wapi?....Sindi? Sindi huyuhuyu mtoto wa Nalela ekhee…..na kama ndiye mwanamke uliyeokota uko unamleta tumlipie mahari…. basi mwaka huu wangu!’ Mama aligeuka na kweda kuufunga mlango wa nyumba kisha akageuka na kuanza kuondoka, kijana wake akiwa bado anamtazama tu na asimmalize.

‘Hivi ni kitu gani Sindi amekukosea mama….kwanini unamchukia hivi?’ Nyanza alimfuata mama yake haraka kabla hajavuka kizingiti cha geti la bati.
‘Mama siku zote humtakia mema mwanawe…..Sindi sio wa daraja lako mwanangu’ Mama yake akamuasa
‘Kivipi mama?....wote tumeshindwa kufika mbali kielimu sababu ya umasikini, wote tumetoka familia masikini na isitoshe tuko imani moja…na sasa kipi cha kunitofautisha na Sindi’ Nyanza aliongea kwa jazba kidogo, alishaanza kuchoshwa na risala za kumtaka aachane na Sindi.

Mama yake akamtazama usoni kwa muda, asipepese hata macho.
‘Mungu anipe uhai…siku moja utarudi hapa hapa na utaniangukia miguuni na utakiri kuwa huyu binti sio daraja lako’ Mama yake amamweleza taratibu lakini kwa sauti ya ukali
‘Kwanini?’ aliuliza akisisitiza na sauti ikipaa hewani zaidi

‘Sindi Nalela!...Sindi!....umeshapigana mara ngapi sababu ya Sindi?....unaishi maisha ya mashaka, wasiwasi na dhoruba zote sababu ya Sindi!....bado tu huoni kama ni mtu wa kukimbiliwa na mamia ya watu?....hujagundua tu atakupa ugonjwa wa moyo?....’ Mama yake aliongea kwa uchungu sasa, akitaka kijana wake aone ugumu wa kummiliki Sindi Nalela.

‘Mama….sijashindwa kummiliki Sindi….na hakuna mwanamke chini ya jua nitakayempa moyo wangu zaidi ya Sindi….’ akajiapiza mwenyewe na asikumbuke Mapenzi ni kama kamari, ukipata wewe anakosa yule.

Mama akasikitika sana, akatoka na kuishia zake akimuacha kijana wake amesimama pale kama mjinga fulani. Sauti ya mama yake ikirindima kwa mara ya pili kichwani na mwangwi wake uligota kwenye akili yake na kumkumbusha Jerry Agapela na wanaume wengine aliowahi kukunjana nao mashati sababu ya Sindi. Akachoka!
8888888888888888888888888

Sindi Nalela alikuwa jikoni akikoroga uji uliokuwa unakaribia kuanza kuchemka. Alikuwa akizungusha mwiko kwenye sufuria pasipo hata kuangalia ni nini alichokuwa anakikoroga. Macho yake yalikuwa yakipepesuka huku meno yake ya juu yakibarizi mdomo wake wa chini. Ni dhahiri akili yake haikuwa pale kwa wakati ule.
‘Ooh….yallah!’ akapiga yowe akiruka na kukuna sehemu ya mguu iliyorukiwa na uji ulioanza kuchemka kwa fujo. Akababaika akitafuta cha kuipulia, mwisho akatumia khanga yake kuipua lile sufuria la uji na kulitua kando.

Akaufunika ule uji na kuchochea kuni kidogo, kisha akabandika sufuria lililokuwa na viazi vitamu. Sindi akarejea kuketi katika kilekile kigoda alichokuwa amekalia. Akilala kwa nyuma kidogo na kujiegemeza katika ukuta mchakavu.
Akashusha pumzi kwa nguvu na kutikisa kichwa kulia na kushoto, akisikitika, na muda huo kelele zikisikika sebuleni kwao.

Akasogeza shingo karibu na mlango na kutega sikio, akiwa ameifumbata mikono yake kifuani
‘….nilishasema, nikasema na sasa nasema….kama kuna baba mwingine humu ndani mwenye mamlaka zaidi yangu mfanye mnavyotaka lakini kama mimi ndio baba humu ndani…Sindi anaolewa na Mzee Dunia….sitaki mjadala’ sauti ya baba yake ikiongea ilimfanya atanue macho yake zaidi na kusikiliza kwa makini uso ukiwa na ndita kadhaa.

‘Baba Sega….Sindi ni mtoto wetu…hebu angalia hiki tunachomfanyia jamani…hebu…’ mama yake alimtetea
‘Nyamaza!...pumbavu!’ Baba yake alikemea
‘Sio suala la kunyamaza angalau tumsikilize mtoto jamani…mwanamke ana haki sawa na…’ Mama Sindi hakumalizia sentensi yake, sauti ya kuchapwa kibao cha uso ilimfikia vema Sindi ambaye alijikuta akifumba macho na kusikilizia kile kibao kana kwamba alichapwa yeye.

ukimya ukatawala kwa sekunde
‘Afunue tena mtu mdomo kuhusu hili suala na ndio tutajua nani ana mamlaka humu ndani…. hayo mambo yenu ya vikao na harakati za jinsia na takataka gani sijui….ziishie kwenye madawati ya mikutano huko huko…msiniletee upumbavu wenu ndani mwangu…nimeeleweka?....nauliza nimeeleweka?’ Mzee Nalela aliuliza kwa jazba

‘Ndio…’ sauti ya mama yake ikajibu ikiwa na kwikwi za kilio. Sindi akajiinamia kwa uchungu, akingoja sauti ya kufungwa kwa mlango ndipo amfuate mama uake. Baada ya kusikia mlango ukibamizwa Sindi alichomoka na kumfuata mama yake sebuleni. akamkuta amekaa sofani akilia kichinichini.

‘Mama…’akamuita akimkumbatia huku naye akilengwa na machozi. Wakalia kwanza
‘Sindi mwanangu….kubali yaishe tu….hata mimi niliozwa hivi hivi…ona mpaka leo niko ndoani na sijathubutu kuachika’ Mama Sindi alisema akifuta machozi

‘Angalau uliolewa na kijana mama….Mzee Dunia?...Dunia? aaargh…mama…. na kujitunza kote huku…leo nikampe heshima yangu yule mzee kama mke wa ngapi sijui… mama kweli?’ Sindi alilalamika akijua wazi mama yake hakuwa na la kumtetea.

‘na anajua u bikra na ndio maana ametoa mahari kubwa kwako….tafadhali usifanye ujinga wowote ukatuletea aibu ambayo itageuka adhabu kwangu….ndio kuzaliwa mwanamke mwanangu….ndio kuwa mwanamke….kifua hiki hakikupewa milima hii ili unyonyeshe tu….ni ili uhifadhi pia machungu na magumu kama haya…’ Mama Sindi aliongea kwa huzuni akimtazama mwanawe usoni na machozi yakimtiririka.

Sindi akatazama pembeni, hakutaka kuyashuhudia machozi ya mama yake. Akanyanyuka na kuelekea chumbani akimuacha mama yake anamtazama kwa huruma.
8888888888888888888888

Suala la kuolewa na Mzee Dunia lilimuumiza sana Sindi Nalela. Angemueleza nini Nyanzambe, angeanzia wapi. aliutumia muda mwingi akiwaza mno. Sku hii mara baada ya kumaliza darasa lake alibaki pale darasani akiwaza na kuwazua.

Aliukumbuka usiku uliopita, aliukumbuka vema. Nyanza alilia mbele yake akimuomba amruhusu kuwa mwanaume wake wa kwanza usiku huo. Akiwa na nguo za ndani pekee juu ya kitanda kichakaavu cha Nyanza, mwanaume huyu alimbembeleza sana amruhusu amuingilie lakini Sindi alimkatalia katakata. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Sindi kubaki mtupu vile mbele ya Nyanza.

Aliumia sana kuona Nyanza akihangaika na  kumbembeleza namna  ile, laiti tu ingekuwa si ile mahari ya Mzee Dunia si ajabu Sindi angekubali kuukata utepe wake usiku huu katika kitanda hiki.
‘Niahidi nitakuwa mimi…’ Nyanza alikata tamaa
‘Nimekuahidi mara ngapi Nyanza…huniamini?’ Sindi aliuliza huku akiumia zaidi kujua alikuwa akiahidi uongo kwa mara nyingine tena. Nyanza asingeweza kuwa mwanaume wa kwanza maishani mwake. Nyanza akapiga magoti mbele ya Sindi akimtazama namna alivyokuwa akiivaa blauzi yake hali matiti yenye ujazo wa wastani, yaliyosimama imara  na kuiva kama embe bolibo yakitikisika katika namna ya kuvutia pale Sindi alipoinua mikono juu kuipitisha blauzi yake.

Nyanza alihema kwa mhemko mkali, akifumba macho na kuivumilia ile hali kwa juhudi kubwa. Akayatazama mapaja manono yaliyojaa na kuvutia mbele yake. Akili yake ikavurugika kabisa alipopitisha mikono yake mapajani hapo akianzia magotini na kuteleza kueleka kiunoni. Nguo ya ndani nyekundu aliyokuwa ameivaa Sindi ilimsisimua zaidi na almanusura apotewe na fahamu.

‘Sindi….niahidi nitakuwa wako milele’ alirai tena na Sindi akatulia sasa na kumtazama Nyanza, akitamani sana kumueleza ukweli wa hali halisi na akashindwa.
‘nitakuwa wako milele Nyanza….angalau nipunguzie hizi ahadi unazonishinikiza kuahidi kila siku’ Sindi akalalamika na Nyanza akamtazama Sindi kwa kiulizo

‘Nakushinikiza?.....ni kweli nakushinikiza?’
‘Ni kama huamini mimi ni wako’ Sindi alimuelewesha na Nyanza hakujibu kitu tena. Alinyanyuka na kukaa kitandani akihema.
‘Kwanini usiniruhusu tu’ akazungumza akigeuka kumtazama Sindi
‘Hapana….. nilisema nitakaa hivi mpaka siku ya ndoa’ Sindi alijitetea
‘Ndoa yako na nani?’ Nyanza akauliza, lilionekana swali la kipumbavu kwa wakati ule
‘Nyanza!...’ sindi akaita kwa sauti, na kuita kule kukamfanya Nyanza aukimbize mkono wake  wa kushoto mdomoni mwa Sindi na kumfumba mdomo

‘Shhhh!...mama amesharudi’ akamkumbusha na Sindi akajikuta akicheka kichinichini. Akanyanyuka na kuvaa gagulo lake kabla ya sketi, kisha akatupia khanga yake kwa juu. Nyanza alikuwa akimtazama muda wote alipokuwa akivaa. Alishavumilia sana na akiingoja kwa hamu siku ambayo Sindi angemruhusu kumgusa, mara zote aliishia kumbusu na kumpapasa hapa na pale pasipo hata kumruhusu kumvua nguo lakini leo walifika mbali zaidi, Sindi alitoa nguo zake na Nyanza akayaona ambayo aliyagusa tu juu ya nguo. Yote haya yalizidi kumchanganya kupitiliza!

Nyanza akatoka na kuchungulia nje akihakikisha usalama kisha akamtoa Sindi, huku wakiwa wameinama wakakimbia kitahadhari na kutoka pale kwa akina Nyanza. Waliikamata njia yenye vichaka kidogo na kutokezea kwa akina Sindi. Wakapitia dirishani pale pale alipotorekea siku ile aliyokwenda kumngoja Nyanza kule porini.
888888888888888888888888

Wiki moja baadaye Sindi Nalela alikuwa kwa rafiki yake Maria ambaye alikuwa anaishi peke yake sasa baada ya familia yake kuhamia mashambani ambako walikuwa wakilima mpunga. Jioni hii mara baada ya kufundisha, alipita kwa Maria kwa minajili ya kumjulia hali na kuongea naye hili na lile. Akiwa amejitupa kwenye sofa dogo lililokuwa sebuleni hapo Sindi alimuona Jerry Agapela akija usawa wa mlango. Kwanza aliachama kwa mshangao kwani hakutarajia kumuona  Jerry pale tena wakati kama ule. Akajiweka sawa na kuendela kushangaa zaidi pale Jerry alipoingia na kusimama mlangoni akimtazama Sindi kwa tabasamu pana.

Jerry aliuona mshangao wa Sindi waziwazi akamfuta na kuketi kando yake. Akili ya Sindi akigutuka na kuuona uenyeji wa Jerry ndani ya nyumba ile.
‘Unafanya nini hapa’ akamuuliza Jerry
‘Kwani ni dhambi mimi kuwa hapa?’ Jerry akajibu kwa mtindo wa swali na wakati huo huo Maria aliyekuwa nje akiingia ndani na kumkuta Jerry

‘Loh! Jerry….haya vipi?’ Maria akamuuliza Jerry huku akitabasamu pia na kutua beseni la vyombo alivyokuwa naosha kule nje. Kule kuchangamkiana kwao kulimfanya Sindi awatazame kwa awamu na kwa viulizo vingi.
Maria na Jerry wakaongea wakitaniana na mazungumzo yao yakimpa picha kuwa walikuwa wameshaonana mara kadhaa na kufahamiana. Sindi akatulia tu akiwasoma na asiwaelewe kwa alfabeti wala namba.

‘Naenda kununua kiberiti Sindi….nisubiri’ Maria akaaga ghafla na Sindi akasimama naye akitaka kuaga na kuondoka
‘Ningoje bwana nakuja!’ Maria kamsisitizia bila kungoja jibu la Sindi, akatoka na kuwaacha wenyewe

Sindi akarejea kuketi kwenye kochi akitazama pembeni na Jerry aliyekuwa kando yake akimtazama yeye.
‘Sindi..’ akaita kwa sauti ya chini akiipeleka mikono yake maungoni mwa Sindi ambaye aligeuka na kuikwatua mikono ya Jerry
‘Sitaki’ akajibu kwa ukali ambao haukuakisi ukali aliotaka uonekane, neno sitaki lilitoka katika namna ya kubembeleza

Jerry akasimama na kuuelekea mlango, kaurudishia na kurudi pale sofani wakati Sindi akimtazama  kwa wasiwasi
‘Nakupenda!’ akasema kwa kujiamini
‘Nilishakwambia nina mtu Jerry…..na isitoshe nilimuona msichana wako siku ile….’ Sindi alijibu akimkumbuka Pamela
Jerry hakujibu kitu, alimkazia macho Sindi kana kwamba alikuwa akimpigia mahesabu na Sindi hakuhimili yale macho, akayakwepesha na kuangalia mbele

‘Jerry akamsogelea kwa ukaribu zaidi, Sindi alipojaribu kuinuka, Jerry alimuwahi na kumrejesha kitini na kufumba na kufumbua Sindi alijikuta mikononi mwa Jerry hali midomo yao ikiwa imeungana. Alihea kwa taabu kidogo akijaribu kujinasua mikononi mwa Jerry wakati huo huo akiifurahia ile hali na akitamani iendelee. Mikono ya Jerry ailimiliki na kumpapasa kiustadi zaidi, alihisi nguvu zikimuishia, mwili ukimsisimka na pumzi zikikimbizana puani mwake bila mpangilio.

Jerry akamuachia, kisha akatulia akiwa ameinamisha kichwa chini kwa sekunde kadhaa
‘I’m Sorry!’ akatamka akiinua uso na kumtazama Sindi ambaye alikuwa akihema na kuusikilizia ule msisimko ambao bado ulipita mwili kama shoti ya umeme. Alitamani kushikwa tena na kupapaswa tena wakati rohoni alitamani kumtandika Jerry kibao cha kumkumbusha kuwa ahakupaswa kumgusa! Mwili nafsi vilipingana!

Jerry akanyanyuka na kuishia zake wakati Sindi akimtazama anavyoishia. Dakika moja baadaye Maria akarejea na kumkuta Sindi amejiinamia
‘Nimepishana na huyu mtu hapo nje  akili iko maili sita…nimemuita hajasikia…vipi? ’ Maria akauliza akionyesha sehemu aliyokuwa amekaa Jerry
Sindi hakujibu, naye alinyanyuka na kuondoka. Maria akaguna na kugeuza kichwa haraka kutazama kule mlangoni alikotokea Sindi. Hakuwaelewa!

.....KUNA NINI KINAENDELEA HAPA?....TWENDE TU UTAJUA YOTE!

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger