Thursday, April 18, 2013

SINDI....NA LAURA PETTIE(8)

8

SEHEMU YA NANE

Sauti ya kilio ilisikika ndani ya nyumba hii sambamba na sauti ya mkanda uliokuwa unatua juu ya mwili wa huyo aliyekuwa akipiga mayowe. Mama Sindi alikuwa amesimama nje akihaha huku mikono ikiwa kichwani. 

Wanawe mapacha nao walikuwa wakizunguka zunguka huku na kule na  mara chache wakiukaribia mlango na kuchungulia kwa tahadhari kisha kutoka hapo na kukung’uta kung’uta viganja vyao mithili ya mtu aliyeungua na moto. kichapo kiliendelea ndani!



Punde mlango ukatanuliwa na Mzee Nalela akatoka akiwa amefura, mkanda wake ukiwa begani. Akawapita aliowakuta nje kana kwamba hakuwaona. Mama Sindi na wanawe wakakimbizana kuingia ndani na kumkuta Sindi akiwa ameketi chini akilia na kusugua sugua zile sehemu zilizosulubiwa na mkanda.

‘Ona sasa unakoelekea mwanangu….’ Mama Sindi aliongea kwa huzuni, akimtazama binti yake mbaye kipigo kilimtembelea jioni hii, siku mbili mbele tangu Mzee Dunia alipomuona na Nyanza kule njiani.

Mzee Dunia alimtafuta Mzee Nalela na kudai mahari yake, akichochea utambi wa kuelezea aliyoyaona, hili lilimkasirisha Mzee Nalela mno. Sindi alipaswa kuenenda kama msichana aliyechumbiwa tayari na si kuonekana akiwa na mwanaume mwingine wakizurura kama wapendanao.

Sindi alilia kwa uchungu akizitazama alama za mkanda uliopita mwilini mwake kwa nguvu zote. Mama Sindi akamuagiza Danze akalete maji ya moto na kitambaa kwa ajili ya kumkanda Sindi wakati yeye na Denzi wakimnyanyua na kumpeleka chumbani.

‘ninavyokukanya uwe unanisikiliza Sindi…’ Mama Sindi alimsemesha mwanawe kwa kilugha wakati akikamua kitambaa na  kukibandika kwenye kiwiko cha mkono wa kushoto wa Sindi.

‘Yalaaah…Mamamamamamaa….uuuuuwi’ Sindi aligugumia maumivu akijinyooosha na kuyasikilizia maumivu ya maji ya moto na ya mkono pia. Wadogo zake waliokuwa wameketi karibu naye nao waliuma meno wakiyaakisi maumivu ya dada yao.
‘Mzee Dunia amechukia sana….anaweza kutudai hata mahari aliyotoa kwanza’ mama akamlalamikia binti yake

‘ aje tu aidai…. hivi hamkumuelewa shangazi?....Sega atafute pesa ya karo kwa nguvu zake… mama hukulazimishwa kuolewa na baba kwanini mimi mnanifanyia hivi’ Sindi aliongea haraka haraka hapo hapo akipiga piga mguu chini sababu ya maumivu ya kukandwa.

‘….ukikaa kumsikiliza shangazi yako yule hata mume hutapata….tayari ana ndoa mbili zilizovunjika….atakufunza nini cha maana?….mwanamke aliumbwa kuvumilia hali zote…kumvumilia mwanaume mwanangu…..usianze mashindano na malumbano…’ mama aliacha kumkanda na kujaribub kumuweka sawa Sindi lakini akakatizwa

‘ hata kama nanyanyasika mama?....ona nilivyopigwa… kwa vile tu sitaki kununuliwa..’ Sindi alilengwa na machozi upya
‘kutolewa mahari si kununuliwa Sindi….’ mama akadakia

‘Sio kununuliwa ikiwa inatolewa na mtu unayempenda na uliyemruhusu ailete hiyo mahari sio hivi mama…sio hivi jamani’ Machozi yaliteremka kwa kasi naye hakujishughulisha kuyafuta, alikuwa anakitazama kiwiko cha mkono wake kilichokuwa imevimba kuliko sehemu nyingine alizopigwa.

Mama Sindi akanyamaza, akatulia tu akimtazama binti yake, akatulia hivyo kwa sekunde kadhaa kisha taratibu akanyanyuka na kutoka mule chumbani. Sindi akautazama kwa hasira mlango uliorudishiwa na mama yake wakati akitoka, aolewe na dunia kwa ajili ya Sega..... kwanini yeye awe kafara?.... aliutamani muujiza ambao ungemtoa katika mtihani ule, akamfikiria Nyanza, akaumia maradufu alipokumbuka itampasa kumwambia ukweli wa hali halisi, ataupokeaje? 

'Sijui...Sijui jamani' akaropoka kwa sauti akitikisa kichwa. Wadogo zake wakimtazama kwa mshangao!
88888888888888888888888888

Ofisi wa Mzee Agapela ilikuwa na watu wawili ndani yake. Mzee Agapela mwenyewe na mwanasheria wake aliyekuwa ameketi huku akiwa amepakata faili kubwa ililokuwa limeegemea mguu wake uliokuwa umebebeshwa juu ya mguu mwingine.

Mwanasheria yule mtu mzima, alikuwa akimtazama Mzee Agapela kwa umakini mkubwa, wakati Mzee huyu alipokuwa akizungumza hali akiwa amesimama dirishani akitazama nje, kikombe cha kahawa mkononi, na mkono mwingine ukiwa mfukoni mwa suruali.

‘sibadili kitu….’ Mzee Agapela alitamka akigeuza shingo na kumtazama mwanasheria wake kwa macho yaliyokosa tafsiri ya moja kwa moja
‘Lakini robo tatu ya mali zakokumuachia Fiona?.....Kristus!....sitaki kuingilia maamuzi yako lakini kwanini awe Fiona?’ Yule mwanasheria aliliondoa lile faili mguuni pake na kulibwaga mezani, wakati huo huo akimtazama mzee Agapela alivyokuwa akitoka pale dirishani na kurejea kwenye kiti chake.

‘Nilimuandika yeye tangu ‘will’ yangu ya kwanza….na atabaki kuwa yeye mpaka nitakapoona umuhimu wa kubadili’ Mzee Agapela alikisukumizia mbali kikombe cha kahawa alichokitua bele yake wakati alipokuwa anaketi.

‘What about your son?....your blood?’….’ Mwanasheria alimbana zaidi, akiweka maadili ya kazi yake pembeni na kumvaa mteja wake kama rafiki yake wa siku nyingi.

Kristus Agapela hakujibu, alimtumbulia macho yule mwanasheria kana kwamba jibu la swali lake lingepatikana usoni mwake.
‘Hujamsamehe?’ swali jepesi lilimtoka yule Mwanasheria na swali lile ndilo lililomfanya Mzee Agapela ayakimbizie macho yake mbali na kushusha pumzi. Ni kama vile Swali lile ndilo lilobeba jibu la swali la mwanasheria wake.

‘….the past is over Dennis….’ alijitetea
‘lakini makovu bado yapo na umeyawekea alama…..come on Kristus unajisikiaje kumfanyia hivi mtoto wako…. and now hujui alipo how do you feel?…. Fiona ni…’ Yule mwanasheria aliikaza sauti yake kuonyesha msisistizo lakini Mzee Agapela alitikisa kichwa akikataa kuyaelekeza mazungumzo upande ule na akamkatisha.

‘No changes kwenye hiyo will…na mikataba mingine yote make sure iko legally right…’ Mzee Aliweka msimamo wake na hapo hapo akibadili mada, akanyanyuka a kupandisha suruali yake vema, akikusanya baadhi ya mafaili na kuyashika mkononi.

Dennis, mwanasheria wake alisikitika lakini alikuwa nje ya uwezo wa kutatua kile kilichokuwa kikiendelea. Akaichukua briefcase yake iliyokuwa kando ya kiti chake na kuanza kupakia mafaili yake katika ile briefcase.

Akaagana na Agapela, wakipeana mikono na kutakiana siku njema. Dennis Mazimbwe akaondoka akimuacha mzee Agapela amesimama pale pale, vile vile akiitazama picha ya Jerry Kristus Agapela, iliyokuwa juu ya meza. Akameza mate kwa taabu kidogo. Alikuwa amemsamehe kijana wake lakini moyoni mwake bado ukungu wa hasira ulikuwa umemtawala.
888888888888888888888888

Nyanza alikuwa shambani akilima, jua la utosi lilishasogea na kuweka kivuli sehemu kubwa ya eneo lile. Pamoja na hali ile Nyanza alikaza mkono na kulima kwa bidii zote akimalizia kipande cha shamba kilichobaki. Wakati akiendelea kutupa jembe ardhini na kutifua ardhi kwa bidii zote, mdomoni alikuwa akiimba nyimbo za lugha yao ili kujiongezea morali ya kulima.

Ghafla tu akasimamisha lile zoezi na kutazama ng’ambo ya pili ya eneo lile. Kulikuwa na njia nyembamba iliyotengenezwa kwa baiskeli zilizokuwa zikikatiza hapo mara kwa mara. Kilichomfanya asimamishe shughuli yake ni gari dogo lililokuwa likitumia njia ile kufika likotaka kufika.

Wakulima kadhaa waliokuwa shambani walisimama wima mithili ya watu waliokuwa wakitoa heshima zao, wakilishangaa lile gari. Nyanza akakaza macho yapate kuona vema aliyekuwemo ndani ya gari lile lakini hakuona mtu. Vioo vilikuwa vyeusi ti!

Njia ile haikuwa ya magari, ni dhahiri aliyekuwa andani ya lile gari alikuwa mgeni wa maeneo yale an ndio kilichoichota akili za wakulima wale akiwemo Nyanza. Gari lile likakazimisha njia mpaka sehemu ambayo miti iliyofungamana ilimzuia dereva kupenya zaidi.

Akalirudisha nyuma kidogo ambako nako lilikwambia katika tuta lililochimbwa na tairi kwa kadiri alivyotaka kujiondoa katika mkwamo ule. Wale waliokuwa wakilishangaa lile gari sasa wakakaza macho zaidi waangalia hekaheka ya dereva na gari lake. Likamshinda!

Mlango wa dereva ukafunguliwa na mguu wa kike, wenye rangi tulivu, ulionakshiwa na kiatu cha kisasa chenye soli fupi ulitangulia kuonekana kabla ya mwanamke mrefu, aliyekuwa ndani ya Tshirt nyeupe na kikaptura cha jeans, kutokezea.

Nywele zake ndefu, zilizolainishwa na kemikali zikipepea sababu ya upepo uliokuwa ukivuma kuelekea kule alikokuwa. Akashuka na kuiondoa miwani ya jua aliyokuwa amevaa, akazunguka upande ule uliokuwa na tairi lililochimba tuta na kulitazama. Akaonekana kuchoshwa na ile hali. Akaachana na lile tairi na kuangaza huku na kule., moyo wake ukijaa hofu kidogo kuona robo tatu ya wakulima kule mashambani wakiwa wima wakimtazama yeye.

Kwa hali ya woga, akatoa simu yake na kupiga namba kadhaa kisha akaiweka sikioni na kusikilizia upande wa pili. Wakati simu ile ikiita, yule binti akaliona kundi la wanaume wakiwa na mashoka na majembe wakija uelekeo ule aliokuwa amesimama. Akaikata simu haraka na kuugeukia mlango aliokuwa ameuegemea. Akaufungua haraka na kujitoma ndani kwa kasi. Aliogopa!

Nyanza aliyekuwa analiona tukio hili vema, alitabasamu na hatimaye kuangua cheko ndogo akiburudika na woga wa yule binti. Alijua wazi watu wale walingelimdhuru hata chembe. Yule binti akawasha gari na kutaka kuliondoa pale lakini tairi likachimba zaidi udongo na kulifanya gari lititie zaidi.

Akahamanika zaidi alipowaona wale wanaume wakiwa wamesimama karibu na gari lake wakimtazama pasipo kumsemesha wala kumpa ishara yoyote. Nao walikuwa wakilitazama gari namna lilivyokuwa likizidi kudidimia

Wakati akihangaika kuvurumsha gari ili litoke eneo lile, kijana mmoja akalisogelea dirisha la gari na kuchungulia ndani. Tukio lile lilimuwewesesha binti yule na akajikuta akiuachia usukani na kupiga yowe mikono ikitetemeka. Simu iliyokuwa mapajani mwake ikiita haikumzindua.

Alikuwa katika hamaki kubwa, akili yake iliyawazia mabaya mengi ambayo yangemkuta muda ule pasipo kujipa hata nafasi ya kuwazuri zuri moja ambalo lingefanya akili yake itulizane na kuomba msaada!

Nyanza aliweka jembe lake begani na kuanza kushuka taratibu akilifuata lile kundi la wanaume lililokuwa limesimama katika lile gari, wakisemezana  kwa kilugha….

….BINTI HUYU NI NANI?.....  JERRY NA BABA YAKE WANA SAKATA GANI?.....TWENDE TARRRRTIIIIIBU …UTAYAJUA YOTE!

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger