Wednesday, July 10, 2013

SINDI....NA LAURA PETTIE (25)

25
Fiona Agapela alishusha pumzi kwa nguvu zote na kusimama kichovu pale alipokuwa amejibanza akimsikiliza mumewe kwa siri. Akazikusanya nguvu na kutoka kwa mwendo wa kunyata huku kichwa kikitazama ule mlango wa kuingilia chumba cha ofisi ya Mzee Agapela ndani ya nyumba yake.


Kule kutazama nyuma kukamfanya apamiane na Jenifa aliyetokezea kwenye kona
‘Whaaat!’ Jenifa akamshangaa
‘Hebu njoo..’ akafanya kuamrisha, akimshika mkono Jenifa na kuelekea naye kule alikotokea Jenifa. Ilikuwa kama alikuwa anamburuza kwa ile haraka aliyokuwa nayo. Wakapelekana chumbani kwa Jenifa na kufunga mlango.

‘Kuna nini?’ Jenifa akauliza kwa mchecheto na Fiona akampa ishara ya kutulia kwanza, akimshika mkono na kumketisha kitandani, Mashaka yakiwatawala kila mmoja kwa sababu yake.

‘Baba yako alikuwa anaongea na Mzee Okello’ Fiona akaongea kwa sauti ya tahadhari
‘Mmh…kuhusu nini?’ ile sauti ya tahadhari ikahamia kwa Jenifa, macho sasa yakimtoka na masikio yake yakifunguka kwa mapana na marefu
‘Ndoa!’ Fiona akajibu haraka haraka kana kwamba jibu lile lingempatia ahueni ya wasiwasi na jakamoyo lililomkumba ghafla.

‘Ndoa?’ Jenifa ahamaki kwa sauti kiasi cha kumfanya Fiona amzibe mdomo haraka sana
‘Shi shi shii..’ akatamka Fiona akiupiga piga mdomo wa Jenifa kwa kiganja chake akizifuatisha zile Shi alizozitamka. Jenifa akajishtukia na kushusha sauti yake
‘Ndoa ya nani na nani?...’ akauliza kwa sauti ya kunong’ona
‘Pamella na Jerry…’ aliyeulizwa akajibu akigeuka pia kutazama mlangoni kuangalia usalama.
‘Khaa! ndoa ya Pamella na mzimu au?... wana uhakika gani Jerry yupo?... mi mwenyewe sina uhakika na kama niliyemuona ni Jerry kwa kweli na kama ulvyosema Pamella amekataa hajui alipo basi itakuwa miujiza kupanga ndoa na mume hajulikani aliko’ Jenifa akaongea kwa mshangao na asielewe

‘Hata mimi ndio nashangaa au kuna kitu kinaendelea hapa na sie hatuna habari?’ Fiona akauliza kidadisi
‘Sijui…’ Jenifa akakataa kwa kutikisa kichwa bao alikuwa hajaielewa mantiki nzima ya wazee wale kuongelea ndoa hali Jerry mwenyewe alikuwa hajulikani alipo.
‘nenda kazungumze na Pamella…’ Fiona akamsukumizia Jenifa mzigo mzito  alioutua hapo hapo

‘Pamella!?...aaah! yule mtu?...hapana bora nikae posta masaa kumi naongea na sanamu la bismack kuliko kutumia hata dakika zangu tano kuongea na yule mwanamke…I hate her mnoooo’ Jenifa akakiri yake akiukwepa mzigo wa Fiona.

‘Sasa tutajuaje kinachoendelea?’ Fiona akahoji akionekana wazi kusumbuliwa na hali ile kupita maelezo
‘Tukae tu kimya tuone mwisho wa mchezo utakuwaje…. watajua wenyewe wanaotaka kuandaa harusi na mume hewa…’ Jenifa akajitoa na asijue mwenake Fiona alikuwa na maslahi gani katika sakata lile. Fiona akashusha pumzi na hapo hapo wakajikuta wakitazamana na kutoleana macho bada ya kumsikia Mzee Agapela akimuita Jenifa kwa sauti.

Jenifa akanyanyuka na kutoka akimuacha Fiona peke yake. Lile hamaki aliyokuwa nayo sasa ikajitokeza kama kama sindano itoboayo nguo. Jerry alikuwa hai! huu ukweli alioanza kuuamini ulimnyima usingizi, ulimtesa tangu Jenifa alipomwambia alimuona Jerry akiwa na gari kama la Pamella. Aliweweseka! Hakutaka jambo lile liwe kweli hata chembe.
Alihema kwa nguvu kiasi cha kutoa sauti mdomoni, mabega yake yakinyanyuka na kushuka kila sekunde iliyokatika. Uso wake uliojaa jitimai iliyochanganyikana na mashaka ulipoteza nusu ya urembo wake. Alihisi maji aliyoyafumbata kiganjani yalianza kuchuruzika!
8888888888888888888

Pamella Okello alitoka supermarket akiwa na mizigo iliyoonekana kumuelemea kidogo sambamba na kule kuongea na simu wakati akilielekea gari lake. alipata tabu kidogo kuibana simu kwa bega lake la kushoto hali pia akijaribu kufungua mlango wa gari pasipo kudondosha kifurushi hata kimoja. Akafanikiwa!

Akiwa ameibana simu yake vile vile akarudi nyuma na kufungua mlango wa siti ya nyuma na kutua vitu vyake vyote, kisha akarejea siti ya mbele na kuingia garini. Hakuwasha gari, aliiondoa simu upande wa kushoto na kuihamishia mkono wa kulia sasa ikiwa imeshikiliwa kwa mkono.
‘Baba?... amekuja lini?’ akauliza akiwa amekunja uso katika namna ya kutomuelewa mpigaji

‘OMG!.... kweli?....Khaa!...sasa?.....Yesuuu… amekuja na mama?.... okay…sawa…poa basi…. poa…. haya bwana’ akawa anaujibu upande wa pili na kisha akakata simu na kuilaza mikono yake juu ya usukukani, mdomo ukiwa wazi, macho yakikikodolea kioo cha mbele pasipo kukitambua akilini. Alikuwa ameduwaa!

Akawasha gari na kuondoka eneo lile akielkea nyumbani kwao, alikokuwa baba yake. Njia nzima alikuwa akipanga na kupangua kipi cha kuongea na kipi cha kuficha. Kipi cha kujitetea na kipi cha kukiri.  Nusu saa baadaye alishafika nyumbani na kushuka kwa kasi akilifuata lango la kuingilia ndani. Pale sebuleni hakumuona mtu zaidi ya watumishi waliomtazama tu na wasitamani hata kuongea naye. Akazikwea ngazi haraka haraka na kuelekea sehemu ya mapumziko iliyokuwa ghorofani.

Akamkuta mama yake ameketi akinywa juisi na kusoma majarida ya urembo
‘Mamaaa’ Pamella akaita kwa furaha na kukimbilia mama yake mbaye naye alipogeuka na kumuona Pamella alisimama kwa furaha na kumlaki binti yake. Wakakumbatiana kwa nguvu zote.

‘Pam…where have you been?’ mama yake akamuuliza akimtazama kuanzia juu mpaka chini. pamella akamtazama tu mama yake na kutabasamu
‘hebu kaa chini kwanza…’ mama akamvutia kiti binti na kuketi pamoja naye
‘amekuja saa ngapi’ Pamella akauliza
‘muda mrefu kidogo…. baba yako ana hasira sana wewe…you lied to us Pam why?’ mama yake akamhoji

‘….baba yako alijua unaishi humu ndani....amekuja hajakukuta…and dada wa kazi amefukuzwa sababu yako’ Mama yake hakumpa hata nafasi ya kujitetea
‘It is a long story mama…. na…’ hakumalizia akageuka nyuma na kumuona baba yake akiingia pale walipokuwa

‘Oooh Dad…’ Pamella akajikuta akinyanyuka na kumkimbilia baba yake, akamkumbatia kwa furaha mno. Mzee Okello akaonekana kufurahi sana kumuona Pamella binti pekee kati ya wanawe wanne wa kiume.

Mazungumzo yakaanza. Lawama, maonyo, maswali na kila aina ya mawaidha ya mzazi kwa mwanawe yakaongelewa. Pamella akieleza sababu za kuhama akificha ukweli kuhusu kuwa na mahusiano na Patrick Mazimbwe. Akaficha tena kuhusu kujua alipo Jerry na akaeleweka na kupewa masharti ya kukaa uko aliko kwa miezi miwili tu na angepaswa kurejea nyumbani pale.Kwa shingo upande akakubaliana na wazazi wake.

Wakati akinyanyuka na kuagana na wazazi wake huku akiwahakikishia alikuwa salama Pamella alisikia mama yake akimwambia baba yake kwa sauti ya ukali huku akimbinya mkono kwa staili ya kumzuia asiseme alilotaka kusema
‘Not now Daniel please!...’ aliisikia vema kauli hii lakini hakuielewa. Akaaga na kuondoka akiwa na mtumishi mmoja ambaye aliambiwa aondoke naye. kichwani alikuwa na maswali mengi mnoo kuhusiana na kauli ile.
8888888888888888888

Pamoja na furaha yote ya kuwa na Sindi Nalela mule ndani, bado Jerry alionekana mara kadhaa akipoteza furaha yake na kuzubaa. Sindi aliyekuwa ameketi kwenye kigoda akichambbua mchele alimtazama Jerry kila mara na asimuelewe.
 Mvuke uliotoka kwenye sufuria lililokuwa kando yake juu ya jiko ndio uliomshtua Sindi na akajikuta akiutua ungo na kuufunua mfuniko. maji yalikuwa yamechemka.

Akanyanyuka kivivu akiuweka ungo wa mchele kitandani na kusimama, huku akiikaza khanga yake kiunoni. Akamatazama tena Jerry.
‘unawaza nini Jerry?’ akamzindua na Jerry akatabasamu tu asijibu lolote.
‘si uniambie’ Sindi akakazania akiwa amesimama pale pale na Jerry akatikisa kichwa kulia na kushoto kukataa

‘Niko poa tu….halafu hilo jiko lako linaongeza joto humu ndani bwana’ akabadili maongezi na Sindi akaligundua hilo. Hakutaka kumsinikiza amwambie hilo lililokuwa linamtatiza. Akachukua jiko lake na vitu vyake vingine vya kupikia na kutoka kordoni.

Jerry alikuwa na msususiko moyoni. Alikuwa na hasira zilizochanganyikana na kutoelewa hatima ya maisha yake ya kujifichaficha. tangu amsikie Pamella akimuongelea Fiona, moyo wake ulishaanza kufikiria mengine mengi tofauti na alivyokuwa akiwaza mwanzo. Angeishi vile mpaka lini? Alishachoka kungoka kuambiwa mara hivi mara vile na watu aliwaajiri kufuatilia suala lake.

Akakumbuka aliyoongea na Meddy nay eye Jerry kujiapiza angejitokeza mbele ya familia yake ili lwalo na liwe kuliko huku kuishi kama digidigi akiwakwepa watu asiowajua. Wakati akiwaza na kukata shauri kujitokeza alikumbuka mchezo mchafu anaomchezea Sindi.

Moyo ukamuuma mno, alitamani sana kumwambia Sindi ukweli kuwa yeye hakuwa masikini wala yatima kama alivyomuaminisha. Alikuwa akiipima imani ya Sindi kama angempenda pamoja na hali ile ya umasikini. Ndio kwanza mapenzi yao yalichanua na moyo wake ulishakubali kuwa na Sindi. Alijiuliza uongo ule angeliuendeleza mpaka lini?

Akatulia tena na kuwaza zaidi, mikanganyiko ilikuwa mingi kichwani mwake. Akasonya kwa sauti na kutoka kitandani pale alipokuwa ameketi.  Akasimama katikati ya chumba chake akishusha pumzi kwa ghadhabu na kuipiga teke ndoo tupu iliyokuwa imesahaulika pale karibu na kitanda. Ndoo ile ilipaa kidogo na kubamiza kiti kilichokuwa na ndoo nyingine yenye maji ya kunywa. Mlio ukasikika mpaka kordoni na Sindi akaingia pale ndani haraka.

‘Hey…kuna nini?’ akamuuliza Jerry akimshangaa
‘Leave me alone’ akamjibu akitoka mule ndani na kuishia zake. Sindi akaduwaa kwanza. hakuwahi kumsikia Jerry akiongea kiingereza hata cha I love you I miss you. Akakunja uso zaidi akitafuta kilichomtibua Jerry na hakukiona. Muda mfupi tu walikuwa wamepakatana wakicheka. Sindi akashusha pumzi ndefu kidogo akishindwa kumuelewa mwenzake. Laiti tu angelijuayaliyokuwa kichwani mwa mwenzake ngelimuonea huruma.
8888888888888888888888

Nyanza Mugilagila kule kijijini shinyanga alikuwa na hekaheka kubwa mno. Mpaka muda ule aikuwa hajaamini alichoambiwa na Alma kuwa Sindi alikuwa Dar es Salaam. Alma hakumueleza ukweli zaidi kuwa Sindi alikuwa na Jerry uko aliko. Aliogopa kumchanganya na asijue kuwa taarifa ile tu aliyompatia ilishamchanganya mno Nyanza.

kichwa chake kiliwaza kuliko kawaida. Alitoka pale kitandani na kulifuata boksi lililokuwa limehifadhiwa darini na kulitoa. akarudi nalo kitandani akiikalia biblia iliyokuwa pale kitandani. Akasonya na kujiinua kidogo, akiondoa ile biblia na kuitupilia kando. Mungu alisahaulika kwa muda!

Akalifungua lile boksi na kulimimina kitandani, akilikung’uta kuhakikisha pesa zote zilzokuwa mule ndani ya boksi zilizondokea kitandani. Akaanza kuzihesabu kwa pupa mpaka alipoziweka zote kiganjani na kupata idadi. Macho yalimcheza cheza kama mtu aliyekuwambuka kitu.

Akaziacha zile pesa kitandani na kutoka mbio mpaka kwenye kona moja ya chumba. Akalifuata panga na kuchimba chimba kwa tahadhari kisha akatoa kibubu kilichokuwa kimezikwa hapo. Akakikung’uta na kurejea nacho kitandani kwa kasi.

Akakifungua kwa kutumia lile panga na kutoa noti zilizokunjwa kunjwa  na kuziweka kitandani, akianza tena kuzihesabu kwa kuziokota na kuzikunjua kisha kuzilaza kiganjani. Alipohitimisha akaunganisha na zile alizokuwa nazo. Akatabasamu kwa huzuni. Alishapata nauli ya kumleta Dar!

Akili yake ilishamuamrsha kuja jijini kumtafuta Sindi na asijiulize wapi angempata, angeanzia wapi na kwa nani? hayo hakujiuliza wala hakusumbuka kujipa muda wa kuuchambua uamuzi wake. Alishaamua kuja Dar na hata kama mama yake angefufuka na kumzuia si ajabu asingemsikia!

Alfajiri ya siku iliyofuata Nyanza Festo Mugilagila akaondoka kijijini kwao Mzimbuni. Akiwa amemuaga Alma na mdogo wake ambaye alikuwa shule karibu na kijiji chao. Akaondoka akiwa na uso wenye furaha na matumaini, matumaini makubwa ya kumuona Sindi Nalela, mwanamke aliyeuteka moyo wake na kukimbia nao.
8888888888888888888888

Mitaa ya mbezi beach ilishatulia muda huu wa saa tano kasoro usiku. Baa chache zilizokuwa bado ziko wazi eneo hilo zilijaa utulivu wa kutosha. Jerry alikuwa akiendesha gari la Meddy  alilokuwa akitumia na kuliegesha hoteli ya New Afrika kila alipoelekea kwa Sindi.

Aliliendesha akiifuata barabara ya vumbi kidogo yenye changarawe iliyokuwa na utulivu wa aina yake. Akakata kona kadhaa na kulielekeza gari moja kwa moja mbele ya geti kubwa lililokuwa limekumbatiwa na ukuta mrefu wenye nyaya za ulinzi juu.

Mlinzi aliyekuwa zamu akatoka na kama mtu aliyemfahamu Jerry akamruhusu kuingiza gari ndani kwa kumfungulia geti. Jerry akaingia na kuzima gari. kisha kwa sekunde kadhaa akainamisha kichwa kwenye usukani kama mtu aliyekuwa anawaza.

Akakata shauri na kuteremka, taratibu kwa mwendo wa kujikokota akaufuata mlango mkubwa wa kuingilia ndani ya nyumba hiyo na akasita kubisha hodi. Sekunde chache zikakatika mlangoni pale akiwa ametumbukiza mikono mfukoni na kuinua kichwa chake juu kama mtu aliyeitazama dari, pumzi zikiyajaza mashavu yake kama puto na kutoka taratibu.

Akageuka kama mtu aliyetaka kutoka lakini moyo wake ukasita na akajikuta akiugeukia tena mlango na kuufungua. Kitasa kikatii na mlango ukafunguka. Sebule ilikuwa kimya. Akaingia na kuurudishia mlango nyuma yake. Huku akiangaza huku na kule. Kama mwenyeji ndani ya ile nyumba akaifuata kordo iliyokuwa inampeleka kwenye mlango uliokuwa wazi nusu na taa yenye mwanga ikiwaka.

Alitembea kwa tahadhari mpaka alipoufikia mpango na kuchungulia ndani. Pamela alikuwa na simu sikioni kama kawaida akiwa ameibana kwa bega lake akizunguka huku na kule. alikuwa akichagua nguo kabatini na kuiweka kifuani kisha kujitazama kwenye kioo kama ilimpendeza. Nguo kadhaa zilikuwa kitandani.

Yote hayo Jerry hakuyaona, aliuona mwili mzuri wa Pamella aukiwa ndani ya gauni laini la kulalia lililomkaa vema na kuvutia. Aliduwaa pale akili yake ikisambaa na kutawanyika.

Pamella akakata simu na kuirusha kitandani, akageuka taratibu kama mtu aliyetaka kutoka mule chumbani na akagongana uso kwa uso na Jerry Agapela. Hakumtarajia wala hakutarajia kumuona pale. Ujio ule ulimfanya amtazame Jerry kwa mshangao wakati akizipiga hatua kumfuata. Wakakumbatiana kimya kimya pasipo kusemeshana lolote. Wakatulia vle wakiwa wamefumba macho kimya kimya…..

....... NYANZA HUYOOO ANAKUJA MJINI.....

1 comment:



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger