Monday, September 16, 2013

SINDI....NA LAURA PETTIE (39)

39
‘Karibu..’ Sindi Nalela alitaka kuiondoa ile hali ya kuzubaa iliyomkuta Patrick Mazimbwe pale mlangoni. Hakujibiwa!


Sindi akautanua mlango kwa mapana kidogo na kujirudisha nyuma hatua moja akiwa ameuegemea mlango na Patrick akanyanyua mguu kwa kutaka kukivuka kizingiti cha mlango lakini akajikwaa kwenye lile jenereta lililokuwa miguuni pake, kujikwaa kule ndiko kulikomrejeshea akili yake sawia.


Akababaika kidogo na kukumbuka kilichomfikisha pale mlangoni. Soni zikamtembelea na akajikuta akijiinamia na kucheka kidogo kabla ya kulinyanyua lile jenereta na kuanza kuingia nalo ndani. Hatua mbili tatu za kumfikisha ndani zilimtosha, akalitua lile jenereta pale sebuleni na kumgeukia Sindi aliyekuwa anaufunga mlango.

Wakatazamana sasa, kila mmoja akitabasamu na asijue kipi kitangulie kati ya salamu na utambulisho. Kule kugwayana kukapita sekunde tu na wote wakajikuta wakigeuza shingo zao kutazama mlangoni ambako Dennis Mazimbwe alikuwa anaingia.

‘Ooh!...’ Dennis akashtuka kuwakuta watu wawili ambao hakutarajia wangekutana katika mazingira kama yale na wakati kama ule.
‘unaendeleaje binti?’ akamdaka Sindi kwanza wakati akiufunga mlango kwa kuusukuma kwa mguu kutokana na kuelemewa na mifuko ya bidhaa alizokuwa amebeba. Patrick aliyekuwa amerudisha macho yake kwa Sindi alishtuliwa na kaka yake.

‘Come on Pat!...hebu nisaidie hapa’ Dennis alimnyooshea Patrick mikono akimuonyesha ile mifuko. Patrick akaiwahi na kuidaka huku Dennis akimpa maelezo ya wapi pa kuipeleka. Akaondoka na ile mifuko kama mtu mwenye haraka ya kuwahi kurudi pale sebuleni.

Dennis akamkaribia Sindi na kuondoka naye kuelekea chumbani alikomfikisha mara ya kwanza. Dakika mbili baadaye akarejea sebuleni na kumkuta Patrick akiwa ameshaliweka sawa lile jenereta na ni kama vile alikuwa akimsubiri yeye ili amuage.

‘Kazi imeisha steshonari?’  Dennis akamuuliza Patrick mara tu alipofika pale sebuleni na Patrick akaitikia kwa kichwa akichungulia kordoni kama mtu aliyetarajia kuona mtut mwingine akitokjezea uko.

Dennis akalifuata kochi na kujitupa kama mzigo, akilegeza tai yake na kutanua miguu yake kujipa nafasi ya kulitalawa kochi vizuri.
‘huyu ni nani?’ Patrick akauliza kwa mshawasha anaye akijiweka kwenye kochi la pili. Dennis akatabasamu kavu, tabasamu lililofikisha ujumbe uliokusudiwa. Hakutaka kumzungumzia Sindi! Patrick akashusha pumzi na kiherehere kikzidi kumtekenya kiasi cha kushindwa kujizuia kuhoji tena na tena.

‘Ni mdogo mno kuchukua nafasi ya Daniella…’ Patrick aliongea kwa kubabaika na Dennis akamtazama kwa jicho la mshangao uliozimwa ghafla na kicheko kifupi kilichokosa tafsiri rasmi.
‘Sivyo unavyofikiria…’ Dennis akamjibu mdogo wake akishusha pumzi kwa sauti na kumtazama mdogo wake. Alimtazama tu na ukimya ukapita tena kati yao.

Patrick akatabasamu na kujiinusha, akijiandaa kuaga na kuondoka. Hakuwa na mazungumzo mengi na kaka yake. Tofauti yao kiumri na tabia ya ukimya ya kaka yake vilimfanya mara zote akose namna ya kuzungumza naye achilia mbali ukaribu wa mtu na mdogo wake.

‘Ngoja niwahi kwangu… naona muda umeenda’ Patrick akazuga akisugua sugua mikono yake kama mtu aipashaye moto. Dennis akaitikia kwa kichwa tu huku akimtazama
‘utaniagia kwa binti ndani…’ Patrick akaendeleza mazungumzo ambayo Dennis aliendelea kuyaitikia kwa kichwa tu pasipo kujibu lolote huku Patrick akitamani kupaza sauti na kumuita binti yule ili japo amuone tena na kumuaga.

Akaondoka kwa kaka yake kichwa kikiwa na michirizi ya maswali iliyomuachia nyufa za kutosha. Binti yule alikuwa nani?... alikuwa pale kama nani?... Dakika mbili tatu alizomtazama mrembo yule, Patrick Mazimbwe alihisi akili yake ilikimbilia kusikojulikana. Moyo wake ulikuwa umempenda Sindi Nalela. Alitaka kumjua, alitaka kumfahamu lakini zaidi alihisi moyo wake ulitaka kummiliki binti yule lakini tatizo alikuwa ni nani kwa Dennis kaka yake? Alikosa jibu!

Dennis Mazimbwe alitulia pale kochini kwa dakika nyingi tu, akionekana kutopea kaika mawazo. Akiwa katika hali ile aligeuza kichwa chake taratibu na kuitazama meza iliyokuwa na vitabu kadhaa juu yake pamoja na fremu ya picha yenye ukubwa wa wastani iliyokuwa imeegeshwa hapo. Aliitazama picha ile kwa kina, uso wake ukionekana kujaa simanzi.

taratibu akayateremsha macho yake toka katika ile picha na kutazama sakafuni, akayatembeza macho yake sakafuni taratibu na kuyainua juu sasa akiitazama dari huku kichwa kikiwa kimeegemea kochi.  Akashusha pumzi nyingi kwa mkupuo ulionyanyua mabega yake juu na kuyateremsha chini taratibu.
‘Daniella!...’ akalitamka jina hili kwa hisia zote huku akifumba macho kama mtu anayesikilizia maumivu.

Alikuwa amemkumbuka mkewe wa ndoa, alikuwa amemkumbuka mno Daniella Carter. alikuwa amewakumbuka watoto wake mapacha, Ilishapita mwaka mzima tangu utokee mfarakano mkubwa kati yake na mkewe, mfarakano ambao mpaka dakika ile ulikuwa kama uliotokea jana yake. Ulimuumiza moyo mno na kitu pekee alichokuwa akikisubiri ni huruma ya Daniella kwake.

Maisha yake yalikuwa yamejaa vurugu za kutosha. Pamoja na watu wengi kumuona kama mwanaume msomi, mtulivu, mwenye furaha na mafanikio ya kutosha wengi hawakuwa wakijua maisha halisi ya Dennis Mazimbwe! Laiti tu wangejua theluthi ya jitimai aliyokuwa nayo Dennis pengine wengi wangekiri si kila mara pesa huleta furaha!
8888888888888888888888

Nyanza Mugilagila alikuwa amemaliza kufanya hesabu zake za biashara. Kiasi cha pesa alichokuwa nacho kitandani kilimfanya atabasamu peke yake. Biashara ilikuwa imemuendea vile alivyokuwa anataka na kwa kiasi kikubwa alikuwa na furaha moyoni mwake. Wakati akimalizia kuzihifadhi zile pesa katika sanduku lake, akaiona biblia yake ndani ya sanduku na kuitoa. Picha ya Sindi iliyokuwa katikati ya biblia hiyo ndio hasa iliyomfanya aichomoe biblia toka sandukuni.

Akaketi kwa kuegemea ukuta, huku akiitazama ile picha ya Sindi aliyoishika kwa mikono miwili. Ugumu wa kumpata Sindi ulikuwa wazi mbele yake japo hakutaka kukiri hilo lakini moyoni pia hakukata tama. Alisali kila alipolala na kila alipoamka akimlilia Mungu amrudishe Sindi mikononi mwake.

Aliitazama picha ile kwa dakika kadhaa kisha taratibu akairejesha kwenye biblia na kuitupia sandukuni tena. Alisikitika peke yake, Pamoja na kuzunguka huku na kule, pamoja na kukutana na wanawake wa kila aina katika ile biashara ya mitumba bado Nyanza hakuwa amekongwa moyo na mwanamke yoyote yule zaidi ya Sindi Nalela!
88888888888888888888

Saa sita mchana katika jengo la ofisi za Jerry Agapella kulikuwa na pilikapilika kubwa. Wafanyakazi walikuwa wakipitapita huku na kule huku wakipata vitafunwa na kubadilishana mawazo. Ndio kwanza walikuwa wamemaliza kumkaribisha Jerry Agapella ofisini kwa mara ya kwanza tangu atoweke katika mazingira ya kutatanisha.

Mkurugenzi alikuwa amerejea kazini rasmi na siku hii alikuwa ofisini kwake katika kiti cha kazi, akifunua faili hili na kufunika lile, akipokea simu hii na kukata ile. Aliteleza na kiti toka sehemu moja kwenye nyingine huku simu ikiwa sikioni na mara kadhaa akilazimika kuibana kwa bega ili mikono iweze kushika hiki na kile kwa wakati mmoja. Alikuwa na kazi kpitiliza!

Wakati akitekeleza majukumu yake, mlango wa ofisi yake ukafunguliwa taratibu na maua yakatangulia mbele na kumshtua Jerry.
‘Hellow!’ sauti ya kike ikaita na muitaji akisikilizia muitiko wa salamu yake kabla ya kujitokeza
Jerry akatabasamu na hatimaye akacheka kabisa! alishamtambua muitaji kwa kuitazama miguu tu!
‘hata ungekuwa nje ningekutambua tu Pam…’ akategua kitendawili na kufanya Pamella ajitokeze mzima mzima huku naye akicheka.
Jerry akanyanyuka na kumlaki Pamella. Wakakumbatiana kwa bashasha kwanza wakitaniana na kucheka.  Jerry akayapokea yale maua na kuyaweka juu ya meza kisha akamgeukia Pamella na kuendelea kuzungumza naye.

‘Wait kwanza..’ Pamella akamkatisha akimtazama Jerry usoni
‘nini?’ Jerry akauliza kwa wasiwasi na shauku
‘Umekula?’ Pamella akauliza
‘No…’ jerry akajibu akitikisa kichwa na Pamella akamshika mkono tayari kumuongoza nje ya ofisi
‘Tunaenda wapi?’ Jerry akauliza kwanza
‘niachie mimi…’ Pamella akajibu, akilifuata koti la Jerry lililokuwa limeegeshwa kwenye kiti chake cha kazi na kuja kumvalisha Jerry.

‘I just miss my best friend…’ Pamella alimnong’oneza Jerry wakati akimvisha lile koti na kufanya Jerry aitikie kwa kichwa akikubaliana na ile kauli. Wakatoka wakicheka mule ofisini na kuingia mapokezi ambako vicheko vyao vilikata ghafla.

Clarita Gabson alikuwa mapokezi akiwa na maua yake pia. Ndio kwanza alikuwa anamalizana na sekretari wa Jerry. Pamella Okello sasa akamshikilia Jerry vizuri kwa mbwembwe zote akitaka Clarita amuone kwa marefu na mapana.

Jerry alisimama kama sanamu, mkono wa kulia ukiwa mfukoni na mkono huo huo ukiwa umeng’ang’aniwa na Pamella. Mkono wa kushoto ulikimbilia shingoni ghafla kabla ya kuteremka na kuingia mfukoni pia. akatabasamu wakati akimtazama Clarita ambaye anaye tabasamu bovu liliupamba uso wake kwa lazima.

‘Congrats!’ Clarita akamudu kutamka wakati akimfuata Jerry na kutaka kumpatia yale maua. Mkono wa kulia uliokuwa umeng’ang’aniwa na Pamella ulishindwa kutoka kwa vile Pamella aliudidimiza usiinuke na wakati huo huo alishindwa kuyapokea yale maua kwa mkono wa kushoto. Usingekuwa ustaarabu!

Pamella akayawahi na kuyapokea kwa mtindo wa kuyanyakua.
‘Mmmh…mazuri…’ akayanusa na kuyasifia kisha kuyatupia kwenye moja ya viti vilivyokuwa mapokezi hapo. Clarita akaduwaa!
‘Lets go!...’ Pamella akamuamrisha Jerry ambaye alimtazama Clarita kwa tabasamu na kumshukuru kwa kumuinamia kidogo huku ule mkono wa kushoto ukitoka mfukoni na kushika kifua ili kufikisha hiyo heshima. Wakaondoka!

Clarita akawatazama kwa mshangao, kuanzia walipopiga hatua ya kwanza mpaka walipotokomea mbele ya upeo wake
‘Shit!’ akalaani akihema kwa ghadhabu na Sekretari akicheka  kichinichini. Akayanyakua maua yake na kuinua kichwa chake juu, pasipo kuaga akatoka kwa hatua ndefundefu na kuishia. Sekretari aliyekuwa na baadhi ya mabinti pale mapokezi wakaangua kicheko kirefu kwa tukio lile.

‘aisee kuna siku zitapigwa hapa mpaka mshangae…’ binti mmoja alivunja kicheko
‘Hands down kwa Pamella…the girl knows how to handle bitches!’ Sekretari akadakia
‘saaana!... ulikuwepo siku ya sherehe ya Mzee Agapella… Pamella mwehu aisee… aombe Mungu asitokee wa kumpindua tu…’ binti mwingine aliyekuwa kwenye mashine ya fotokopi alionya

‘Hakuna!... Pamella ana pesa…ni mzuri… amesoma halafu mzee wake anajulikana… Jerry atataka nini kwa mwanamke mwingine mpaka amuache Pamella?.... akitokea wa kuuteka moyo wa Jerry akamuacha Pamella Okello I swear nitatembea uchi mwenge mpaka posta…’ Sekretari alijiapiza kabisa na kufanya wenzake wacheke.
8888888888888888888

Siku mbili tatu baada ya Sindi Nalela kufika nyumbani kwa Dennis Mazimbwe. Nanny aliyekuwa mtumishi wa Dennis alijitahidi kumzoesha mazingira ya nyumba ile huku akimsaidia kutibu majeraha madogo madogo aliyokuwa nayo. Nanny alicheka peke yake namna Sindi alvyokuwa akijifunza kutumia baadhi ya vifaa vya umeme vya mule ndani.

Alicheka zaidi alipomuwashia Sindi mashine ya kusafishia carpet iliyomfanya Sindi aruke kwa hofu. Alijikuta tu akimfurahia binti huyu mno na ndani ya siku hizi mbili aligundua kitu kikubwa ambacho alisita kumuuliza lakini pia alitaka sana kukiongea na Dennis kwanza. Alihisi Sindi alikuwa na mimba changa!

Jioni hii baada ya kazi zake, Nanny alimuaga Sindi na kuondoka zake na hivyo kumuacha Sindi peke yake. uenyeji alioanza kuupata angalau ulimuondolea hali ya kujikunyata. Aliweza kuwasha luninga na kuangalia kupoteza muda au hata kuingia jikoni na kupika hiki au kile.

Muda huu wa saa mbili usiku, Sindi alikuwa amejikunyata katika sofa akiwa anatazama luninga huku akimenya chungwa juu ya sahani aliyokuwa ameipakata. Ghafla akasikia mngurumo wa gari ana akahisi mwenyeji wake Dennis alikuwa amerejea toka kazini. Akajiinusha kidogo na kwenda kuchungulia dirishani.

Akaguna kwanza! halikuwa gari la bosi wake, akatanua pazia zaidi na kuchungulia vema lile gari lililoingia na kuegeshwa karibu kabisa na ngazi za kulifikia lango la kuingilia ndani. Mlango wa dereva ukafunguliwa na kijana jamali mtanasati akateremka na kujinyoosha kidogo, akirekebisha suruali yake kiunoni na kufunga mlango.

Sindi akafumba macho kwa sekunde mbili nzima! akayafumbua na kukodoa tena pale dirishani safari hii akiyatoa macho yake kana kwamba alitaka yaone kwa umbali ambao hakupata kuuona tangu azaliwe. Bado alichoona mwanzo ndicho hicho hicho alichokiona muda ule. Almanusura apige yowe lakini sauti ilikwamia kooni na kumletea ukavu wa sauti.

Alimeza mate kwa juhudi kubwa akizidi kutumbua macho na sasa mikono ikimchezacheza kwa hamaniko.

Kijana aliyekuwa akimtazama alisimama pembeni ya gari lile akionekana kuongea na simu taratibu na hapo hapo akipiga hatua akizifuata zile ngazi kwa madaha.
‘…Niko hapa kwako tayari…Mzee amesema niipitie niichukue…sawa…’ alisikika akiongea na sauti ile ile, sauti ya mtu yule yule.
Sindi alihisi pumzi zikikaribia kukata. Akaachia pazia na kurudi kinyumenyume huku akitetemeka. Alikuwa amemuona Jerry Kristus Agapella!

Mlango aliokuwa akiutazama ukagongwa!

ITAENDELEA....

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger