Wednesday, September 4, 2013

SINDI.....NA LAURA PETTIE (36)

36

Jenifa Agapella na Clarita Gabson marafiki wa tangu utoto walikuwa nyumbani kwa Mzee Agapella wakipeana michapo mbalimbali huku wakiandaa chakula chepesi cha kupata jioni ya siku hiyo. Clarita alikuwa na kikopo chake cha ice cream, akiikwangua hiyo ice cream kwa kijiko na kuila taratibu kana kwamba hakutaka iishe haraka, wakati huo akiwa amesimama kwa kuigemea friji kubwa iliyokuwa jikoni hapo.



Jenifa alikuwa akiandaa mayai na mikate iliyokuwa juu ya meza ya kupikia huku mara kadhaa akiiacha kazi yake na kumgeukia Clarita kupiga soga kwanza.
‘Yaani sijawahi kujua hata anachompendea Pamella… hasikii haoni Clari’ Jenifa alizungumza akirejea tena kukoroga mayai aliyoyavunjia katika bakuli

‘That witch!.. nxa!... yaani simpendi Pamella jamani angelijua hili hata kukaribiana na mimi asingethubutu… halafu ulimuona alivyokuwa anamemganda Jerry kwenye Party…’
‘hana aibu yule… nilimchukia zaidi kipindi mama anaumwa… Clarita!...hata kumshika mama mkono alikuwa anaona kinyaa’ Jenifa akageuka tena soga zikipamba moto

‘usiniambie!’ Clarita akashangaa
‘I wish ungekuwepo…. anakuja na Jerry mpaka wodini kisha anasimama mlangoni kule wakati mama yuko huku…’ akasema Jenifa akimuonyesha umbali wa mlango na kitanda cha mama yake ulivyokuwa.

‘hata Salamu?..’ Clarita akauliza akiacha kujiegemeza na kusimama wima, akimkodolea macho Jenifa
‘Nini salamu?... hata pole tu ya mbali walaa’ Jenifa akaongezea chumvi sasa akijisahaulisha zile nyakati chache ambazo Pamella alijitutumua kumkaribia mama yake na kumpa pole, achilia mbali kutoa pesa kuwasaidia hapa na pale. Yote hayo alijisahaulisha kwa wakati ule.

‘Sasa na yote hayo…Jerry anampendea nini?’ Clarita akahoji akipiga hatua kumfuata Jenifa pale alipokuwa amesimama. Wakawa mkabala na kumpunguzia Jenifa kazi ya kugeuka
‘sijawahi kujua haki ya mama…sijui!.... wengine washirikina tu… nasikia hata mama yake alitumiaga mzizi kumkamata yule Mzee… ndio maana hafurukuti kila analosema yule mama yule Mzee anatii tu…’ Jenifa akaongea kiushabiki sasa akisahau baba yake naye alikuwa ameshikiwa akili na mwanamke mwingine wakati wakimuuguza mama yao.

Clarita akatikisa kichwa tu akiwa bado na mshangao usoni. Wakati wakitaka kuzungumza zaidi wakasikia mlango ukifunguliwa na watu wawili wakiingia na kuongea kwa sauti ya juu kidogo. Wakatega masikio wakitazamana!

‘Meddy siwezi ni ngumu kuliko unavyofikiria… na siwezi kumuoa Pamella kama wanavyotaka wao wakati kuna mtu mwingine niliyemharibia muelekeo wa maisha tayari’ Jerry alijitetea mbele ya Meddy akionekana wazi kuchanganywa na kauli ya baba yake iliyomtaka ajiandae kumuoa Pamella.

‘Umeshazungumza na Pamella kuhusu hili suala?’ Meddy akauliza taratibu akimhurumia rafiki yake
‘Lipi?’ Jerry naye akauliza asimuelewe Meddy
‘hili la kumuoa yeye…anajua kuwa wazazi wenu wana mipango gani?’ Meddy akajieleza akiweka mikono yake kwenye mifuko ya suruali na kumtazama Jerry kwa umakini.
‘Sijui…I just don’t know what is going on…. awe anajua au hajui… sijali kuhusu hilo Meddy… akili yangu sasa inawaza cha kufanya juu ya Sindi basi’ Jerry akajibu akishusha pumzi kwa mdomo na kutikisa kichwa chake huku na kule.

Kule jikoni Jenifa na Clarita walitazamana kwa mara nyingine, nyuso zao zikiwa na matuta kadhaa. Hawakuyaelewa yale mazungumzo. Wakajisogeza karibu na mlango wa kutokea jikoni hapo kuelekea sebuleni walikokuwa akina Jerry.

‘Okay may be… umatafute kwanza Pamella umwambie ukweli kuhusu Sindi na hali yake… ama kusanya nguvu umwambie kweli Sindi kuhusu wewe… just come out Jerry.. the truth will set you free…’ Meddy alitoa ushauri na Jerry akamgeukia na kumtazama kana kwamba alichoongea kilikuwa ni kitu kipya kusikika duniani.
‘What!...ni come out?...how?...naanzaje?... nianze tu kuwa Sindi you know mimi ni hivi na hivi… just like that!... na utegemee atakuamini tena maishani mwako… No!.. No Meddy…No!’ Jerry akaweweseka akionekana kuzidi kuchanganyikiwa maradufu. Meddy akamhurumia zaidi, alihisi ni kwa kiasi gani hali ilikuwa tata kwa rafiki yake.

Jerry akakurupuka na kupandisha ngazi haraka akifuata hicho alichokuja kukifuata. Dakika mbili baadaye waliondoka pale na kuelekea kwa Meddy huku nyuma Jenifa na Clarita wakibaki wameachama midomo!

‘Sindi?...Sindi ni nani tena?’ Clarita akauliza yeye ndio akionekana kuguswa mno nay ale mazungumzo. Jenifa alikuwa bado amekunja uso kama mtu aliyekuwa anajikumbusha kitu kichwani kisha ghafla uso ukamchanuka na akajikuta akiachama tena mdomo na kutanua macho hali akimtazama Clarita.

‘Whaat!’ Clarita akahoji kwa shauku naye akimtazama Jenifa kwa msisitizo
‘Aaaww!...hili jina nilishalisikia tena kwenye mazungumzo ya Jerry na Pamella… it was like Pamella alikuwa anamlalamikia Jerry kuhusu huyo Sindi’ Jenifa akategua kitendawili na asijue alimchanganya Clarita kiasi gani

‘But who is she?...huyo Sindi ni nani?’ Clarita akauliza kwa jazba kidogo na Jenifa akabetua bega lake la kulia kujibu lile swali kuwa hakumjua huyo Sindi. Uso wa Clarita ukajaa huzuni ghafla. Mapambano ya kumgombea Jerry hayakuwa yake na Pamella tu, kulikuwa na mwanamke zaidi ambaye alionekana kuwa na nguvu kuliko wao wawili. Alihisi mkuki moyoni kiasi cha kutolipa uzito suala la Pamella kuolewa na Jerry!
8888888888888888888888888888

‘ Mom I’ll be okay!...usijali… nilishaahidi mwezi huu ukiisha narudi nyumbani’ Pamella aliongea na mama yake wakati akimsindikiza mlangoni.
‘Baba yako anaongea hili kila siku…. please honey na iwe kama ulivyoahidi…you don’t want to break your dad’s heart….right?’ Rebecca, Mama Pamella aliongea na binti yake pale mlangoni hali akimtazama kwa upendo bintiye.
Pamella akatabasamu na kumkumbatia mama yake. kisha wakafungua mlango na mama aktoka nje akipunga mkono. Pamella akasimama pale mlangoni mpaka mama yake alipotoa gari lake nje ya geti na mlinzi kufunga geti. Pamella akarudi ndani kwake na kusimama pale sebuleni akiitazama sebule yake asijue aanzie wapi.

 Akayatazama majarida yaliyokuwa yametapakaa kwenye kochi, akavitazama vinywaji vilivyokuwa juu ya meza, akazitazama nguo zilizokuwa kwenye kochi lingine zikingoja kukunjwa, akashusha pumzi na kutikisa kichwa, akionekana kuchoka na kutotamani kugusa chochote kwa wakati ule.

Akajishika kiuno kwanza, akizitazama zile nguo kwenye kochi, akafanya maamuzi!
Akaenda ndani na kurudi na tenga dogo la plastiki la kuwekea nguo, akazikusanya na kuzitumbukiza katika tenga kisha akalifunika. Alipolinyanyua na kutaka kuelekea nalo ndani. Akasikia mlio wa hodi. Uso wake ukakimbilia kwenye saa iliyokuwa ukutani na kuguna!

Alilitua tenga chini na kuufuata mlango. Akaufungua na Patrick Mazimbwe akaingia ndani.
‘wow! hujagongana na mama hapo kwenye kona?’ Pamella akamuuliza akifunga mlango na kumgeukia mpenzi wake
‘Nimemuona anapiga kona pale kwenye baa kuingia barabara kubwa’ Patrick akajibu akilegeza tai yake na kujitupa kwenye lile kochi lililokuwa na nguo.
‘na ungemkuta hapa ingekuwaje?’ Pamella akauliza akilifuata lile tenga na kuliinua tena, akalipachika kiunoni upande wa kushoto

‘Si ndio angenifahamu sasa au?....’ Patrick akajibu akitabasamu na Pamella akamtazama tu bila hata kuliunga mkono lile tabasamu akageuka na kuyanza kuelekea ndani kisha kama mtu aliyekumbuka kitu akamgeukia Patrick
‘you can’t be serious!’akatamka akiwa na uso ulionuna na kuishia ndani akimuacha Patrick anatabasamu peke yake na kunyanyuka kulifuata lile kochi lililokuwa na magazeti. Akayasogeza na kuanza kuyapitia juu juu

Pamella akarejea na kuketi kando ya Patrick ambaye aliyakusanya magazeti yake aliyoyarudika mapajani na kuyabwaga kwenye meza iliyokuwa mbele yake kando ya vinywaji.

‘Sijakuona tangu juzi…’ Patrick akaanza kuzungumza mkono wake wa kulia ukiligusa paja la Pamella lililokuwa wazi kutokana na kuvalia kikaptura kifupi
‘Mama anakaba sana siku hizi…she wants to be kila nilipo yaani natamani likizo iishe haraka nirejee kazini…’ Pamella akajibu mkono wake wa kuume ukikuna kichwa chake na kutibua tibua nywele zake

‘Lazima atamani kuwa nawe muda mwingi..wewe ni binti pakee na zaidi amekuwa mbali nawe miaka sasa…mingapi sijui?’ Patrick akauliza
‘Sita…au saba’ akajibu Pamella akitabasamu
‘Hivi kwanini lakini?...’ Patrick akachimba
‘ni long story Babe….tuyaache hayo…tuongelee yetu sasa… mi nataka kukutana na Dennis kaka yako’ Pamella akapeleka ombi lililotua kama konzi kichwani mwa Patrick

‘Why?’ akajikuta akiuliza haraka uso pia ukibadilika
‘Why?... Patrick!....mimi kufahamiana na kaka yako mkubwa ni dhambi kiasi cha kuuliza kwanini?’ Pamella akahoji akionyesha kutofurahia namna ombi lake lilivopokelewa
‘No..i mean…namaanisha pengine una kitu cha kuongea naye…he is a lawyer bwana… may be una shida binafsi’ Patrick akajitetea haraka licha ya moyo wake na akili yake kujua wazi ni nini Pamella alimaanisha

‘No!,,,sio mambo ya kikazi… nataka nimjue tu nay eye ajue mimi na wewe tu wapenzi…that is all babe…tunahitaji kupiga hatua moja ya uhusiano wetu….mimi mama anajua kila kitu kuhusu sisi…it is time na kwako mmoja ajue kinachoendelea….la bda uniambie huna future na mimi’ Pamella akaongea taratibu akimtazama Patrick usoni na ule uzuri wake ukizidi kung’aa lakini pia ukishindwa kuutuliza moyo wa Patrick ambaye ombi hili lilikuwa gumu kupitiliza. Alishamtambulisha Clarita kwa Dennis, angeanza vipi kumtambulisha Pamella pia.

Dennis alikuwa kaka yake mkubwa, aliyemlea kama mwanaye baada ya wazazi wao kufariki kwa ajali wakati Patrick alipokuwa na miaka miwili. alikuwa mtoto wa mwisho aliyezaliwa uzeeni uko ambaye hakutarajiwa kabisa. Dennis ndiye aliyebeba jukumu la kumtunza wakati huo akiwa ndio ameanza kujitegemea.

Dada yao aliyemfuatia Dennis aliolewa na bahati mbaya alifariki wakati akijifungua hivyo Katika kukua kwake Dennis alikuwa kama baba yake na kaka yake. Asingeweza kumfanyia upuuzi wa kumletea wanawake tofauti tofauti. hivyo ombi la Pamella lilikuwa kitanzi shingoni!

Pamella akamtazama Patrick alivyokuwa amezubaa na ghafla tu Pamella akasimama na kumwambia alikuwa jikoni kwa ajili ya kuandaa chakula chao cha usiku. Patrick akabaki peke yake. Akionekana kukosa raha na kutopea katika mawazo! Mchezo aliokuwa anaufanya ulianza kumchezea mwenyewe bila kujua Pamella Okello ni mtoto halali wa Dennis kaka yake!
88888888888888888888888888888

Usiku huu pia haukuwa mzuri wa Sindi Nalela. Pale kitandani alipoketi alijikunyata na kuukumbatia mto kwa juhudi zote. Akiitafuta faraja na asiione. Moyo ulimuuma mno. alijizuia kutolia lakini maumivu na majuto yaliyokuwa yakimtembelea yalimsukuma kumeza mate kwa juhudi zote na kuyazuia machozi.

akatoka kitandani na kulifuata sanduku lake, akalifungua na kulichambua upoande mmoja kisha akatoa kibahasha ambacho alikimimina kitandani na noti kadhaa zikadondokea kitandani. alihesabu zile pesa na kuridhika zilikuwa sawa na zilimtosha kuondoka pale kurejea kwao. Akazirudisha mahala pake na kuketi kitandani pale kama bwege!

Dakika moja tu ilimkumbusha Mungu alipo, akaifuata biblia yake na kupiga magoti ukingoni mwa kitanda kisha akaiweka biblia mbele yake kifua chake, mikono yake ikikutana na kufumbatana mbele ya uso wake huku viwiko vya mikono vikiwa vimegota kitandani. Akasali!

‘Mungu wangu….nimekosa…nimekosa mimi… Mungu…nitazame…nakuhitaji wakati huu…nakuhitaji Jehova…nimepotea… nimepotea Yesu… nishike mkono..nionyeshe nini nifanye…nionyeshe mwanga wa amani ulipo…’ akasita kidogo na machozi yakamteremka wakati kwikwi za kilio zikimkaba kwa muda, akapumua na kujitahidi kuendelea

‘Nimetenda dhambi kubwa… nimekukosea Mungu wangu…lakini nakuja mbele zako… eeh Mungu wangu…’ akshindwa kuendelea kusali na akajikuta akiketi kitako chini na kulia kwa kuomboleza. Akalia kwa uchungu sana. Alikuwa ametoroka nyumbani kukimbia ndoa, alikuwa amemuacha mwanaume aliyempenda Nyanza, na sasa alikuwa mjamzito pasipo ndoa wala muelekeo. Alikuwa amejivurugia maisha ndani ya muda mfupi tu bila kutarajia. Hakukuwa na cha maana alichofanya!

Alilia zaidi, alipokumbuka usia wa mama yake, alipokumbuka kauli za baba yake, alipokumbuka aibu aliyoitia familia yake na sasa alikuwa anarudi kuwaongezea aibu ya kuwa na mimba ya mtu asiyemjua vizuri. Aliumia, aliumia sana sana sana. Alitamani kuamka toka katika ile ndoto na kujikuta kijijini kwao akiisha maisha aliyokuwa naishi, akijiiba kukutana na Nyanza wake na kurejea kwao. Pengine angeolewa tu na hatimaye angeachika na kumrudia Nyanza lakini sio hivi alivyofanya!

Sindi alilia mno lakini maji yalishamwagika!
8888888888888888888888888888888

Kulipokucha, Asubuhi ya siku iliyofuata Dennis Mazimbwe alikuwa ofisini kwake. asubuhi hii haikuwa njema kwake hata kidogo hasa baada ya kupata ugeni huu uliokuwa mbele yake.
‘You know what Fiona!... get out of my office Now!’ Dennis aliongea kwa msisistizo sentensi ya mwisho akitamka neno moja moja kama mwalimu anayesoma imla kisha neno la mwisho akalipaza na kulipayuka kwa ghadhabu wakati Fiona akitabasamu pale alipokuwa ameketi.

‘Dennis!...’ Fiona akamuita akitabasamu huku akinyanyuka
‘shida yangu n indigo sana..sana sana….kuona WILL ya Agapella…just to know who is written there…and I’m done na milioni 15 ni zako ndani ya wiki hii…ugumu uko wapi hapo?’ Fiona akauliza akiwa tayari amemfikia Dennis pale alipokuwa amesimama kando ya kiti chake cha kazi. Walisimama mkabala na Fiona akaminua kichwa na kumtazama Dennis usoni huku akimung’unya midomo yake na kumrembulia macho Dennis.

‘Nimesema hapana!.... tafadhali Ms. Agapella naomba uondoke…. ninaiheshimu taaluma yangu kuliko unavyofikiria….please show yourself out’ Dennis akapangua mikono ya Fiona na wakati akiishika ili kuiondoa mlango ukafunguliwa na Rebecca akaingia ghafla na kuganda mlangoni akiwashangaa namna walivyokuwa wamekaribiana na vile Dennis alivyokuwa ameishika mikono ya Fiona.

Dennis akaiachia mikono ya Fiona ghafla na Fiona akatabasamu akijinyanyua kidogo na kumbusu Dennis shavuni. kisha kwa mwendo wa maringo akaifuata pochi yake na kuelekea mlangoni alikokuwa amesimama Rebecca, mke wa Mzee okello.
‘He is all yours now’  akamtamkia Rebecca kwa sauti ya chini lakini iliyomfikia vyema na kutoka zake akitabasamu.

‘Dennis! how could you?’ Rebecca akapayuka akiwa amehamanika mno na Dennis akajikuta akitoka mbio kumuwahi Rebecca ambaye alikuwa anageuka ili aondoke. Denis akamkimbilia na kumkamatia kordoni.

‘Niachie!...Dennis!...Dennis!’ Rebecca alikuwa analia sasa akiipangua mikono ya Dennis iliyokuwa imekazana kumzuia asiondoke. Dennis akamshinda nguvu na kumbana ukutani huku akiomba amsikilize.
‘Sitaki…sitaki….niachie’ Rebecca akafurukuta na kufanikiwa kujitoa mikononi mwa Dennis kisha akatoka mbio na kuishia zake nje. Pasipo kujua pale kwenye parking Fiona alikuwa kwenye gari akimtazama alivyotoka kwa kuchanganyikiwa na kuanza kulia kwenye gari. Hata alipopita na gari lake mbele yake hakuliona gari la Fiona. Mwanamke huyu akacheka kicheko kirefu cha ushindi huku akitikisa kichwa. Alichotaka kujua sasa kilikuwa wazi mbele yake!

Kule ndani Dennis alikuwa na hali mbaya mno, alikazana kupiga simu ya Rebecca ambayo iliita pasipo kupokelewa na mwisho ilisikika ikimtaarifa namba hiyo ilikuwa haipatikani.
‘Shit!’ akaibamiza simu yake chini huku akihema kwa ghadhabu kwelikweli.
8888888888888888888888

Fiona Agapella baada ya kuvuruga ofisini kwa Dennis akanyoosha njia mpaka hospitali alikokuwa amelazwa mumewe. Aliegesha gari  lake na kutoka kwa mwendo wa madaha na furaha. Akapita mapokezi na kupandisha ngazi kuelekea wodini. Alipoufungua mlango na kuingia Jerry aliyekuwa ameketi kwenye kiti akijisomea gazeti alinyanyuka haraka huku akimtazama baba yake kama alimuona Fiona.

Alimuwahi na kumkamata mkono akimvutia nje haraka sana. Wakasukumana mpaka nje na kusimama nje ya wodi
‘Nini?....unanizuia kumuona mume wangu?’ Fiona aling’aka
‘Mumeo?....una uhakika Mzee Agapella ni mumeo?....’ Jerry naye alimjia juu
‘Oh! Son naona unakuwa kwa kasi kubwa sana mpaka unasahau nani ni nani katika familia’ Fiona akaongea kwa kebehi lakini akijitahidi kutabasamu

‘familia?....hivi nawe unajihesabu katika familia ya Agapella?.... kwa kitu gani?...kwa lipi?...’ Jerry naye alirudisha kebehi akitabasamu. Kwa mtu aliyembali angehisi walikuwa na mazungumzo mazuri ya kufarijiana!

‘Jerry! siko hapa kugombana na mtu…nahitaji kumuona mume wangu’ Fiona akataka kumpita Jerry lakini akazuiliwa
‘Hataki kukuona!....that is all’ Jerry akamjibu akigeuka kumtazama daktari aliyekuwa nakuja upande wao. daktari alipowafikia akawasabahi kwa awamu na kumuuliza Jerry hali yam zee.
‘hajaamka bado…’ Jerry akajibu na yule daktari akamgeukia Fiona
‘Mama itabidi uongozane na mimi ofisini…tunahitaji kuzungumza’ yule daktari akatamka taratibu mbele ya Fiona ambaye uso wake ulishaa hasira

‘hata hapa liseme tu’ akajibu akimtupia macho Jerry na Jerry akaitikia akimaanisha kutoa ile ruhusa
‘Mr. Agapella ameomba usimuone mpaka atakapotoka hospitali… na sisi tunaheshimu matakwa ya wagonjwa wetu endapo tu yanaonekana kuwa ya msingi… hatutahitaji kutumia nguvu kukuondoa eneo hili… kuwa muungwana tu na ujaribu kukaa mbali na Mr. Agapella kwa kipindi hiki’ Dokta aliongea kwa hatua, uso ukionyesha hali zote za kujiamini na kusisitiza anachoongea.

‘Nini?... siwaelewi’ akang’aka
‘Ndio taratibu zetu…just make sure hujivunjii heshima kwa kuondolewa na walinzi wetu…sidhani kama italeta picha nzuri kwa familia ya Agapella…. asante!’ dokta akainama kidogo na kuingia chumba alichokuwa amelazwa Mzee agapella, akiwaacha mtu na mama yake wa kambo wakitazamana.

‘…. Ulidhani nikirudi nitakukimbia maisha?... I’m back to protect my family!’ Jerry alimuinamia Fiona na kumpasulia kipande cha ukweli ambao ulimfanya Fiona atunduwae. Baridi ikimtembelea mpaka kwenye mifupa. Akimtazama Jerry vile alivyokuwa anaishia kordoni nay eye kubaki akiwa ameachama mdomo wake kwa bumbuwazi. hakutarajia kusikia kauli ile toka kwa Jerry. moyo ulimuenda kasi zaidi alipowaza pengine Jerry aikuwa anajua kila kitu kuhusu kutekwa kwake. Alichachatika!
888888888888888888888888

Saa tatu usiku Jerry aliingia kwa Sindi Nalela na kumkuta amelala kwa kujikunyata kitandani. Aliingia na mbwembwe za hapa na pale lakini Sindi alikuwa amepooza mno. Ule ukali na kiburi cha hapa na pale havikuwepo siku hii na Jerry alionekana wazi kuvimiss ghafla.

Alimuandalia chakuka akiwa kimya na mwenye uso uliosawajika kiasi cha kumtisha Jerry mwenyewe. Baada ya kula. Jerry alipelekewa maji ya kuoga bafuni na alipotoka tu. Sindi aliivamia suruali ya Jerry na kuitafuta wallet. akaipata na kuifuangua kwa pupa. Noti kadhaa za elfu kumi zilizofikia laki mbili na kitu zikamtunduwaza Sindi. Huku akitetemeka akakichomoa kitambulisho cha kura cha Jerry na kukilaza usawa wa macho yake
‘Jerry Kristus Agapella’ alilisoma lile jina akitetemeka vibaya mno kisha taratibu akakirudisha na mwili ukihisi kuishiwa nguvu pia. Akajitutumua kurejesha kila kitu sehemu yake na sasa alitamani kupiga mayowe kwa nguvu zote. Alikuwa amedanganywa, alikuwa ameingizwa mjini. Jerry John hakuwa Jerry John, alikuwa Jerry Kristus Agapella. Maneno ya akina Jamilla sasa yalimuingia kuliko mwanzo na akayaamini kupita imani yenyewe ilivyo.

Wakati akiwa na lile hamaniko lililomkaba vyema, Jerry akaingia pale chumbani na kujifuta maji. kisha akavaa bukta yake na kumfuata Sindi pale alipokuwa ameketi. alimtazama kwa mshangao namna alivyokuwa anatetemeka pasipo kuongea wala kupepesa macho.

‘Sindi!...una nini leo?...nini mama?’ akamuuliza kwa upole na Sindi akasimama ghafla na kuanza kurudi kinyume nyume akimtolea macho Jerry na machozi yakimporomoka.
‘Jerry wewe ni nani?’ akauliza kwa sauti iliyofifishwa na kilio kilichokuwa kimekaba, midomo ikimtetemeka na machozi yakiteremka kwa kasi

‘Mimi ni nani?....una maana gani Sindi’ Moyo wa Jerry uliruka almanusura uchomoke kifuani.
‘Wewe ni naniiii?.... wewe sio Jerry John….wewe ni nani?....unataka nini kwangu?’ Sindi alikuwa ameshaufikia mlango na kusimama hapo akilia kiasi cha kujiinamia.
Jerry alipooza ghafla, nguvu zilimuishia haraka sana na maneno yakampotea kichwani. Akili ilikimbilia kusikojulikana. Swali la Sindi lilikuwa kama shambulizi la kushtukiza, na kule kubabaika kukamfanya Sindi ajumlishe na kutoa, akagawanya na alipozidisha dio akapata jibu kuwa Jerry alikuwa mpelelezi kweli kama alivyoambiwa na akina Jamila.

Jerry alipogutuka na kutaka kuanza kumfuata Sindi, Sindi alikurupuka na kufungua mlango akikimbilia chumbani kwa Jamilla. Jerry akahisi mambo yameharibika. Akataka kumfuata Sindi na kumweleza ukweli wote bila kuacha neno lakini pia akili yake ilikuwa imevurugika mno na Sindi alikuwa amehamanika mno. Wasingesikilizana wala kuelewana.

Akaitafuta simu haraka sana na kumpigia Meddy, akishindwa kujieleza kiufasaha japo Meddy alimuelewa.
‘Usimtafute usiku huu utamfanya azidi kuchanganyikiwa…. hatakuelewa kabisa….jaribu kulala kesho asubuhi tafuta nyumba sehemu nyingine haraka sana…unanielewa?.... tafuta nyumba umhamishe hapo kwanza…kisha ndio sasa nitakuja tuongee naye na tumuweke sawa…muda huu hataweza kukuelewa’ Meddy alitoa ushauri wake naye moyo ukimuenda mbio kana kwamba sakata lile lilikuwa limemkuta yeye.

Jerry akakubali kwa shingo upande. usiku ule ulikuwa usiku mrefu mno kwa Jerry. hakulala kabisa na asubuhi alitoa elfu hamsini na kuziacha kitandani akiacha ujumbe kuwa zilikuwa pesa za matumizi na angerejea baadaye kidogo na kuzungumza naye.

Aliporejea saa sita mchana akiwa na gari la kuhamisha vitu Jerry hakumkuta Sindi Nalela wala nguo zake. Alipomfuata Jamilla naye akashtuka kujua Sindi alikuwa ameondoka bila kumuaga hata yeye rafiki yake. Jerry akachanganyikiwa vibaya mno. akaingia chumbani na kupekua kama mwehu kuangalia vitu vya Sindi na asione hata kimoja. Sindi alikuwa ameondoka zake na nguo zake na vitu vyake tu na kuacha kila kitu alichopewa na Jerry.
Juu ya mto wa kulalia Jerry aliona karatasi iliyokunjwa vizuri ikiwa imelazwa hapo. akaifuata na kuifungua, akishuhudia zile elfu hamsini zikidondoka chini na wala sijali kuziokota
Jerry Kristus Agapella… nimeondoka! tafadhali usinitafute kwa vile sirudi nyumbani… hii mimba ni zawadi ya ujinga wangu nitaamua kuitoa au kuitunza. Nashukuru kwa kuniharibia maisha, nashukuru kwa kunihadaa, nashukuru kwa yote Jerry, Mungu akubariki.
panapo majaaliwa kila kheri.
Sindi Nalela
Yalikuwa maandishi machache, yaliyoandikwa kwa mlalo wa kuvutia, mwandiko wa kike, mwandiko wa mwanamke aliyempenda sana. Jerry aliiachia ile barua ipeperushwe na upepo uliokuwa ukivuma toka dirishani wakati yeye akiwa amesimama kama nguzo akiwa bado haamini alichosoma!

Katika wakati huu, katika kipindi hiki, katika siku hii, Jerry alikitamani kifo ghafla!... upweke ulimvaa na maisha yalikosa thamani ndani ya sekunde chache tu alizojua asingemuona tena Sindi.


…… NIPE MAONI YAKO….

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger