Tuesday, September 10, 2013

SINDI.... na LAURA PETTIE (38)

38

Jua la saa nne asubuhi lilishachomoza kwa makali ya kiasi chake. Utulivu mkubwa ulikuwa umetanda eneo kubwa la jumba la Mzee Okello… sauti chache zilizosikika zilikuwa za watumishi waliokuwa wakifyeka nje na kupunguza michongoma iliyoizunguka nyumba hiyo. Kwa mbali zilisikika ngurumo za magari toka barabara kuu ya lami iliyokuwa mita kadhaa toka lilipo jumba hilo.


Rebecca Okello, mke wa Mzee Okello, mwanamama mwenye umri wa makamo tu, mwenye uzuri wa asili na umbile la kuvutia alikuwa amesimama dirishani akiwa na kikombe cha kahawa mkononi hali mkono mwingine ukiwa umekishikilia kisosi kilichoambatana na kikombe cha kahawa, aliinywa taratibu kahawa yake huku akitazama nje kupitia dirishani pale na akili yake ikionekana kuchotwa na mawazo yaliyoitesa nafsi yake mno. Uso wake ulikosa nuru!

Ni kama vile Kahawa ile ilishindwa kupita kooni kama alivyotarajia, aliimeza kwa mafunda ya kuhesabu kwa taabu na akajikuta akishusha pumzi na kugeuka kukitua kile kikombe juu ya kabati lililokuwa na sinia lililobeba jagi la kahawa na sukari. Alikitua kisosi kisha akakiweka kikombe juu yake. Akageukia kule dirishani safari hii akifumbata mikono yake pamoja chini ya kifua chake. Alitulia vile akiwaza, akiumizwa na aliyokuwa akiwaza na wala asitambue kuwa mumewe Mzee Okello alikuwa amesimama mlangoni kitambo tu akimtazama!

‘Becca!..’ Mzee Okello akamuita mkewe ambaye wala hakumsikia, akapiga hatua kumfuata na ahatimaye akamshtua kwa kumgusa begani. Rebecca akageuka na kumtazama mumewe usoni, akijilazimisha kutabasamu na akijilazimisha kuvunga kwa kutaka kukichukua tena kile kikombe cha kahawa lakini mumewe akamzuia na kumshika mkono.

Akamuondoa pale dirishani na kumleta mpaka kitandani, akaketi na kumuomba mkewe aketi kando yake. Sekunde tatu za mwanzo alimtazama mkewe kwa upendo hasa!
‘Becca!..’ akamuita kwa sauti ya upole sana na mkewe akamtazama kwa uso ule ule uliokosa nuru huku akiyateremsha macho yak echini kama mtu aonaye soni
‘kama kuna kitu kitapunguza siku zangu za kuishi basi ni kukuona ukiwa huzuni Rebecca… tangu juzi unalia kimya kimya… kuna tatizo gani mke wangu’ Mzee Okello aliongea taratibu akimtazama mkewe ambaye uso wake ulizidi kusawajika na matuta kadhaa yakajipanga usoni pa mkewe, alionekana wazi kushindana na hali Fulani ya uchungu ambao Mzee Okello alitakamani kuujua na hatimaye kuuondoa. Mkewe hakujibu!

‘Nafanya kila ninaloweza kukupa furaha Rebecca…. kila ninaloweza mama… lakini…’ akakosa la kuongeza na kubaki mdomo wazi baada ya mkewe kuangua kilio cha chinichini. Mzee Okello akashusha pumzi sasa na kumkaribia mewe zaidi. akamvutia ubavuni pake na kumkumbatia. Rebecca akalia kwa muda kisha taratibu akajiondoa mikononi mwa mumewe na kujiinamia tena.

‘nimekuumiza wapi mama?... umesikia nini?’ Mzee Okello aliuliza naye akionekana kukosa raha sasa
‘Una mwanamke mwingine…’ Rebecca akajibu akiwa bado amejiinamia na akijua wazi alikuwa akidanganya. Kilichokuwa kikiitesa nafsi yake ni tukio la kumkuta Fiona akimbusu Dennis Mazimbwe. Aliumizwa kupitiliza na mpaka dakika ile hakuwa amepata suluhu na Dennis. Mzee Okello akakunja uso na kumtazama mkewe kiudadisi.

‘Becca!’ akamuita kwa mshangao kidogo na kubweua huku tabasamu likija taratibu usoni pake
‘Mwanamke?... niache mwanamke bora duniani ndani mwangu niende nje kutafuta nini?... nani amekwambia ujinga huo?... ‘ Mzee Okello aliongea na mkewe akiupeleka mkono wake usoni pa Rebecca na kumfuta vijimachozi vilivyokuwa vimebakia mashavuni.

‘Siwezi… siwezi kufanya ujinga huo…never!... Never Rebecca… njoo mama’ akamsogelea mkewe na kumuweka tena kifuani pake kwa mapenzi yote na asijue kilichokuwa moyoni mwa mkewe. Dakika mbili baadaye kitita cha pesa kilikuwa mezani na Mzee Okello alimtaka mkewe akanunue alichohitaji, akamtaka atulize nafsi kwani hakukuwa na mwanamke wa kumzidi yeye maishani mwake Mzee Okello. Alipotoka na kuishia Rebecca akaketi kitandani na kuangua kilio upya, akiomboleza kwa uchungu zaidi huku mikono yake ikiwa kifuani., aliyafumba macho yake na machozi yakamtiririka kwa kasi huku midomo ikimchezacheza. Alilia haswa!
Ooh Dennis…Dennis why?’ alisema akiwa amejiinamia na kuendelea kulia
888888888888888888

Patrick Mazimbwe aliegesha gari lake nyumbani kwa kaka yake Dennis muda huo wa saa nne asubuhi na kuremka kwa kasi kidogo, akishindwa hata kufunga mlango wa gari lake. Alikimbia kidogo kuwahi mlangoni na kubonyeza kengele mara kadhaa akiashiria haraka aliyokuwa nayo. mlango ukafunguliwa na bibi wa makamo aliyempokea kwa tabasamu na kumbatio la furaha

‘Nanny!..’ Patrick alimlaki bibi yule
‘Patty…ooh mwanangu… haya vipi?’ alilakiwa Patrick kwa furaha kubwa na Patrick akamkumbatia na kumbusu pajini bibi yule huku naye akionekana kufurahi kumuona
‘Jenereta lipo?...’ akamuuliza kwa haraka yule bibi na kumkatishia furaha yake
‘Huulizi hali zetu kwanza…wakimbilia kuuliza Jenereta…kwani ndio lililokufungulia mlango?.... Patrick!!…’ yule bibi alisema kwa ukali kidogo akifunga mlango na kumvutia Patrick ndani zaidi akimpeleka sehemu ya kulia chakula

‘No!...unajua nina haraka sana… steshonari kubwa kule juu umeme umekatika na jenereta imegoma kuwaka…kuna kazi Fulani… ooh Dennis!’ Patrick alikatisha maelezo yake mara tu alipomuona Dennis akitokea kwenye kordo akiwa na nguo za kulalia. Hakutarajia kumuona Dennis pale muda kama ule siku kama ile.

Dennis alifikicha macho yake kuashiria ndio kwanza alikuwa anatoka usingizini. Akawakaribia na kumsugua sugua begani yule bibi huku akimbusu utosini na kuachana naye kisha akamgusa begani Patrick na kuachana naye, akaifuata meza na kujimiminia chai ya moto. Pasipo kuweka sukari akapiga funda moja la kugugumia na kutua kikombe.

Wakati wote huu Yule bibi na Patrick wakimtazama kwa mshangao. Akawageukia na kujaribu kutabasamu.
‘Hujaenda kazini?’ yule bibi ambaye ni mtumishi wa miaka mingi wa Dennis alimuuliza Dennis akionekana wazi kushangaa kumuona Dennis pale
‘nitaingia mchana nadhani… huh!...mbona uko hapa muda huu?’ Dennis alijibu na kumgeukia Patrick

‘Nimefuata Jenereta mara moja…’ Patrick alijibu kwa adabu na Dennis pasipo kujibu kitu aliwapita tena na kuelekea chumbani kwake akiwa na kile kikombe cha chai. Lakini kabla hajaufikia mlango wa chumba chake alisita na kuwageukia Patrick na yule bibi, akawakuta bado wanamtazama. Akatabasamu na kugeuka mzima mzima sasa akiwatazama vizuri na kama mtu aliyekumbuka jambo alitembea tena kurejea pale walipokuwa.

‘unamfahamu Pamella Okello?’ akamtandika Patrick swali moja jepesi tu lakini lililomfikia Patrick kama konde la uzani wa dunia. Patrick akatoa macho na kumtazama yule bibi kana kwamba alihitaji amsaidie kujibu. Yule bibi akamonga Patrick konzi la kisogo
‘jibu!’ bibi akamuamrisha kama mtoto
‘yeah!...namjua…amekuwaje kwani?’ Patrick akauliza uso wake ukipoteza hali ya kujiamini na Dennis akibinua midomo yake na kutikisa kichwa juu chini mara kadhaa

‘Mna ukaribu wowote au urafiki..’ Dennis akauliza tena akiguguna ndani kwa ndani na  kutikisa kichwa kulia na kushoto harakaharaka akimaanisha kama kuna chochote zaidi ya hivyo alivyovitaja.

‘hapana..no!,,,,najua tu ni binti wa Okello…nothing more…nothing serious… kwani kunaa…’  akakataa haraka haraka lakini pia akataka kudadisi zaidi ila Dennis hakumpa nafasi hiyo, aligeuka na kuanza kuufuata tena mlango wa chumba chake na kuishia chumbani.

Patrick akatoa macho na kushusha pumzi ndefu mithili ya mluzi.
‘unamjua si ndio….umemdanganya kaka yako!’ Bibi akamsuta
‘I swear Nanny… mambo yanakoelekea sasa mmmh…’ akaguna tu na kufanya yule bibi acheke wakati Patrick akionekana kutafakari ghafla

‘Clarita hajambo?’ Bibi akauliza na Patrick akagutuka na kukumbuka kilichomleta
‘Jenereta liko wapi?... nataka kulichukua sasa hivi…nitalileta jioni…’ alisisitiza shida yake na bibi akamvutia jikoni kumuonyesha lilikokuwa hilo jenereta. Akalichukua na kulipeleka kwenye gari. Baada ya kuliingiza kwenye buti ya gari. Alisimama kwenye mlango wa gari na kumtazama yule bibi.

‘Nikija saa moja nitakukuta?’ akamuuliza
‘Saa moja kamili ukija na dakika tano hunikuti… ila nadhani Deni atakuwepo sidhani kama ataenda kazini leo…’ yule bibi alijibu akitabasamu
‘Hivi ana nini leo… kwanini hajaenda kazini?’ Patrick akauliza akianza kutumbukiza mguu garini

‘Mi hata sikujua kama yupo… atakuwa na yake tu… kaka yako anahitaji kumrudisha Daniella na watoto haa nyumbani… haya mambo ya mke yuko amerika mume yuko Afrika tabu tupu vijana… mimi nazeeka na babu yenu Magomeni pale… tunaona nyumba za makuti zinageuka maghorofa pamoja…tunashangaa pamoja… tunakwepa vifusi pamoja…’ bibi aliongea kwa vitendo kidogo na kufanya Patrick acheke kwa sauti na hata mlinzi aliyekuwa akijiandaa kufungua geti alicheka pake yake kule getini.

Patrick akaingia garini na kuwasha gari akimpungia mkono yule bibi na kuondoka eneo lile. Kichwani akiwaza na kuwazua sababu za Dennis kumuuliza ghafla habari za Pamella Okello. aliguna mara kadhaa na maswali yake yalikosa majibu ya kuridhisha!
88888888888888888888888888

Alitembea kivivu kwa kuyumba yumba wakati akiufuata mlango uliokuwa ukigongwa kwa fujo kidogo. Pale sebuleni aliitazama saa yake na ukutani na mshale mdogo ulikuwa unaikaribia namba 11 huku ule mrefu ukiwa kwenye namba 10. Alipiga mwayo mrefu aliojaribu kuuzuia kwa kiganja cha mkono. kisha akajvuta na kufungua makomeo kadhaa kabla ya kuhangaika na mlango wa chuma uliotangulia uko nje.

Jenifa akaingia kwa jazba kidogo akimpita Jerry ambaye aliurudishia mlango na kumgeukia mdogo wake, mwayo mwingine mrefu ukifuatia
‘Hiki nini sasa…’ Jenifa akashangaa chupa za pombe zilizokuwa juu ya meza

Jerry hakujibu wala hakuonekana kutaka kulijibu lile swali, alijivuta na kujitupa kwenye kochi, akajiegemeza kizembe na kumtazama mdogo wake.
‘Nimegonga jamani….nimegonga nusu ya kuota sugu kha!... ndio kulala au kufa?’ Jenifa akauliza kwa dhihaka akiruka chupa kadhaa za pombe zilizokuwa chini na kuketi sofani.

Jerry hakujibu aliendelea kumtazama Jenifa kana kwamba alikuwa akimletea burudani kwa wakati ule
‘una matatizo gani Jerry… mama analalamika umemkataza asimuone baba hospitali… una matatizo gani eeh’ Jenifa alihoji kimamlaka wala simpe kaka yake nafasi ya kujieleza
‘wale ni watu wazima wanajuana wao…. wewe unapowaingilia na kuanza kuwafarakanisha… unakuwa na lengo gani hasa…. baba sasa hivi ana…’ Jenifa aliongea kwa jazba na Jerry akamkatisha kwanza kwa kupunga mkono hewani akimaanisha hakutaka kusikia zaidi ya kile alichosikia

‘Mama?... hivi bado tuna mama dunia hii?... mama?... Jenifa!... yule mwanamke anakufadhili kwa lipi hasa mpaka unamtetemekea?...’ Jerry alikuja juu sasa
‘Sio kumtetemekea… amenipokea pale kwake na amenirudisha chuo… wewe si ulikuwa unamtegemea Pamella… wewe unavyomtetemekea Pamella kakufadhili kwa lipi?...’ Jenifa alirudisha mashambulizi yaliyomfanya Jerry amtolee macho kwa mshangao.

‘Umesema?’ akauliza kwa kutaka uhakika alichosikia
‘You heard!’ Jenifa akamjibu kwa kiburi

Jerry akajirudisha nyuma na kujilaza kizembe tena, akifumba macho na kutulia vile vile

‘Nimekuja kukwambia tu kuwa acha kuingilia ugomvi wa wazazi Jerry….utaleta matarizo maugbwa zaidi’ Jenifa alikata ukimya akimtazama kaka yake
‘Pumbavu!...nyanyua ngoko zako utoke humu ndani upesi’ Jerry alifoka akinyanyuka na kumuonyesha mlango Jenifa

‘unanifukuza?!’ Jenifa alisimama akiuliza na kushangaa lakini akiwa na ule mshangao Jerry aliukwanyua mkono wake na kumburuza kuelekea mlangoni. Pochi ya Jenifa ikadondoka lakini Jerry hakujali alimkokota mdogo wake mpaka mlangoni. akaufungua mlango na kumsukumia nje, akafunga mlango!

‘Jerry  pochi yangu….Jerry…Jerry’ Jenifa alipiga piga mlango akimgongea Jerry ambaye aliiokota ile pochi na kufungua mlango. Akairushia mbali ile pochi na Jenifa akaambulia kuitazama ikipita pale mlangoni na kupepea kuelekea kwenye ngazi. Jerry akafunga mlango na kumuacha Jenifa ameduwaa mlangoni.

Jazba za Jerry hazikuwa za kawaida. Alishagombana sana na kaka yake lakini haikuwahi kutokea kashikashi ya kutupwa nje namna hii. Aliweweseka pale mlangoni kwa sekunde kadhaa kabla ya kutoka taratibu na kuifuata pochi yake ambayo ilipotua chini ilifunguka na kutawanyia mbali baadhi ya vitu vilivyokuwemo ndani. Aliinama na kuviokota taratibu, mara kadhaa akiutazama mlango aliotokea na asimiani kama ni yeye ndio alisukumiwa nje vile.

kule ndani Jerry alirejea kochini na kujibwaga tena pale, akionekana kuelemewa na ulevi aliotandika usiku uliopita sambamba na mawazo juu ya Sindi Nalela.
888888888888888888888

Saa Nane mchana, Sindi Nalela alikuwa ameketi kitandani akimalizia kupata chakula. tabasamu lake dogo na tulivu liliupamba uso wake mara tu alipomuona Dokta Kashindye akiingia pale wodini.
‘naona umepata nafuu haraka sana… una maumivu yoyote?’ Dokta alimuuliza huku akitabasamu na Sindi akatikisa kichwa kukataa
‘Sasa..’ dokta akaongea kwa kuivuta hiyo sasa akiuma midomo yake kwanza kama mtu anayepangilia sentensi yake vizuri
‘Okay… aliyekuleta hapa…atafika muda wowote ule naaa…’ akavuta tena lile neno na huku akikunja uso kidogo kisha akahairisha kuzungumza alichotaka kuzungumza

‘Subiri kidogo..’ akaomba udhuru na kutoka akimuacha Sindi na maswali kichwani. Alikumbuka vema kilichotokea, lakini hakukumbuka alifikaje pale. alikuwa na maumivu kidogo mguuni na hata alipoligfusa tumbo lake alihisi lilikuwa kama lilivyokuwa. alijikagua hapa na pale na kuona michubuko midogo mkononi, plasta ndogo kwenye kiwiko na michubuko kwenye mguu ule uliochotwa na gari.

Alimshukuru Mungu kwa kumuokoa lakini moyo wake ulikosa utulivu. alitaka kumuona huyo aliyemgonga na kumuokoa. kuna kitu alijiuliza sana tangu ile alfajiri aliyopata fahamu. litaka kuficha kila kitu kuhusu yeye lakini pia roho ilisita. Hakumuamini mtu mjini hapa tena hasa baada ya maisha yake na Jerry Agapella. Mambo mengi yalipita kwa kasi kichwani mwake na akakosa uamuzi wa maana. Bado alikuwa anaweweseka na tukio la kutengana na Jerry!

Mawazo yake yakakatwa na ujio wa Dokta Kashindye akiwa ameongozana a mwanaume mrefu, mtu wa makamo, mwenye mvi chache za kutosha, mwembamba kiasi mwenye mwili mkakamavu. Miwani ya macho iliyokuwa usoni pa mwanaume yule ilimkumbusha mtu aliyemuona akimuinamia dakika chache kabla ya kupoteza fahamu. Akahisi ndiye aliyekuwa akimngojea!

Dennis Mazimbwe alimfuata Sindi kitandani na kumsabahi, akimpa pole nyingi na kuketi kwenye kingo ya kitanda. mguu mmoja ukifika chini na mwingine ukielea hewani.
‘Unajisikiaje sasa?’ akamuuliza Sindi huku akimtazama kwa umakini mkubwa. alikuwa binti mzuri mno na zile aibu za kike alizokuwa nazo kwa mwanaume yoyote rijali wa umri wowote lazima angelimtukuza Mungu kwa uumbaji wake. Dennis alimkodolea macho Sindi na kukosa la kuongea kwa sekunde kadhaa mpaka pale Dokta Kashindye alipoamua kuokoa jahazi.

‘Anaweza kutoka hata sasa…’ akatoa ruhusa na Dennis akaitikia akimtazama Sindi na kisha kumgeukia Dokta, akikosa kabisa neno la kuongeza. Dakika tano zlitosha Sindi kujiondoa pale kitandani na kusaidiwa na Dennis kuondoka wodini.

Ukimya mkubwa ulitawala garini wakati wakielekea nyumbani kwa Dennis Mazimbwe. Mpaka wanafika na kupokelewa na Bibi, Dennis hakuwa amemuuliza hata jina lake la kwanza tu. Bibi akampokea kwa bashasha kwa vile alishaelezwa kuhusu ujio wake.

‘Akamsaidia kutembea kwa kumshikilia mpaka ndani ambako alimpitisha mpaka kwenye chumba alichokuwa ameandaliwa.
‘Aah aah… achana na sanduku mwanangu…au kuna dhahabu umo?’ bibi alimtania Sindi wakati Sindi alipotaka kupokea sanduku lake toka kwa Dennis

‘Ngoja nikuandalie kitu unywe kwanza… tulia upumzike kwanza…sawa?’ bibi alitoa maelekezo na Sindi akatabasamu kiuoga kidogo na kuitikia kwa kichwa akiwa ameshapandishwa kitandani. Dennis akatabasamu na kutikisa kichwa wakati bibi akiongea na Sindi. Kisha wakatoka na kumuacha Sindi mwenyewe akishangaa kupitiliza, akiangaza macho huku na kule mdomo ukiwa wazi, akistaajabu ukubwa wa chumba, mapambo, na kila lililokuwemo mule ndani.

Kule nje ya chumba Bibi alimtazama Dennis kwa macho ya kumsuta
‘Ulitaka kuua malaika wa watu huyu kwa mawazo gani sasa?....anaitwa nani?’ bibi akauliza akimtoa Dennis mlangoni pale na kuanza kuelekea naye sebuleni

‘Sijamuuliza kitu kuhusu yeye… zungumza naye?’ Dennis akamrushia majukumu yule bibi aliyempapasa mgongoni na kutabasamu
‘hilo sio kazi… sema lingine…’ bibi akajibu na kufanya Dennis acheke chinichini
‘ni mzuri..’ Dennis akasema akitabasamu na akimtazama yule bibi katika namna Fulani ya kungojea jibu la kufurahisha

‘Dennis!!...’ Bibi aksitisha kutembea na kumtazama Dennis usoni kwa umakini lakini Dennis aliendelea kitabasamu
‘una mke na watoto… huyu ni binti yako kabisaaaaa’ bibi akaonya
‘Sijafika uko Nannny…’ Dennis akajitetea akizidi kutabasamu
‘Kwani huwa mnafikaje uko?... nikusikie tena!...’ akaonya Bibi akimuachia mkono Dennis na kupiga hatua chache kuelekea mbele

‘Nataka kwenda mlimani city mara moja… kama nitachelewa tafadhali mwambie huyu binti asitoke wala asiwe na wasiwasi…. kesho uwahi kidogo kuja ili asijisikie mpweke sana’ Dennis akaongea na yule bibi ambaye aliitikia maelezo yake na kuridhia.

Dennis akaondoka, na bibi alipomaliza shughuli zake, akamuaga Sindi na kumpatia maelezo kadha wa kadha huku akilitambua jina la Sindi nay eye akijitambulisha kama Nanny. Akamuacha Sindi mwenyewe mule ndani.

Saa mbili kasoro usiku, Sindi alitoka chumbani akichechemea mara baada ya kusikia kengele ikilia mno. taa zilikuwa zinawaka sebuleni hivyo alipotoka alipepesa macho kuangaza kama kulikuwa na mwenyeji yoyote lakini hakuona mtu. Kengele ilizidi kulia na Sindi akajikuta akilazimika kuufuata mlango huku akichechemea.

Akahangaika kuufungua na alipoweza aliutanua mlango taratibu na kuuweka wazi. kijana jamali mwenye aliyefanana mno na yule baba wa makamo aliyemtoa hospitali alikuwa mbele yake. Walitazama tu pasipo kuongea lolote!

‘Wow!...’ Patrick alipiga ukunga akimtazama Sindi usoni, akili ikimpotea ghafla na mshangao wake ukipitiliza na kumduwaza. Alimtazama Sindi kuanzia chini mpaka juu na kumtulizia macho, tabasamu la Sindi likiuchachafya ubongo wake na kumfanya zezeta kwa sekunde kadhaa.

‘Karibu!’ sauti ya Sindi ilipiga masikio yake na kuyatia uziwi wa muda, wakati ubongo wake ukipokea mawimbi ya sauti ya Sindi.

Hakuwahi kumuona msichana yoyote maishani mwake aliyempitisha katika mshtuko wa aina ile. Ndani ya moyo wake alikiri msichana huyu alikuwa mzuri, alikuwa na mvuto wa aina yake, alikuwa na nguvu ya asili, nguvu ya kuvuta na kunasa. Patrick akamtumbulia macho Sindi Nalela asiweze kuitikia ile karibu wala kupiga hata hatua moja ya kizembe kuingia ndani. alimkodolea macho tu mithili ya mtu aliyepigwa na shoti ya umeme ghafla!

Sindi akazidi kutabasamu asijue ni kiasi gani alizidi kuuharibu mfumo wa fahamu wa Patrick Mazimbwe na jenereta lake lililokuwa miguuni pake.


…..USIKOSE KUJUA NINI KITAJIRI…. NIPE MAONI YAKO….

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger