Thursday, March 21, 2013

SINDI....na LAURA PETTIE (3)

3

SEHEMU YA TATU....

Nyanza alikimbilia bondeni kidogo kulikokuwa na vijana wakivua samaki, akawapigia mbija na kuwapa ishara ya kumfuata. Sindi alikimbilia kijijini na kukusanya watu waliokuwa karibu na baada ya dakika kumi na tano Jerry alishazungukwa na wanakijiji, wengine wakimtazama kwa mbali, wengine wakijaribu kumuinua na wengine wakishauriana cha kufanya.

Wakiwa bado katika hekaheka ya kumhoji yeye ni nani na imekuwaje, Jerry akapoteza tena fahamu palepale na taharuki ikazuka kwa hofu kuwa pengine amekufa.



‘hivi Mzee Sagati yupo saa hizi?’ mtu mmoja aliyekuwa amemshikilia Jerry akamuuliza mwenyekiti wa kijiji.
‘Atakuwepo tu….leo wanagawa mbolea tangu asubuhi’ mwingine akajibu na mtoto mdogo wa kiume akiagizwa akimbie kwenda kumuita mwenyekiti.

Mwingine akaagizwa alete baiskeli ya kumbebea toka eneo lile na hapo hapo wengine wakishauri akimbizwe zahanati huku wengine wakifikiria kuita polisi. Mabishano yakawa hayaishi, kituo cha polisi kilikuwa mbali sana na kijiji kile, jengo la kituo cha polisi kilichokuwepo hapo kijijini kilishageuka pagale baada ya kukosa polisi.

Mabishano yao yakatulia alipowasili Mwenyekiti na wazee wachache ambao waliamua kumpeleka nyumbani kwa mwenyekiti wakati wakitafuta namna ya kumfikisha zahanati.
Baiskeli ikaletwa na Jerry akapakizwa na kushikiliwa mpaka kijijini. Alilazwa kwenye mkeka nje ya nyumba na mtu akatumwa kumuita mama Alma ambaye ni muuguzi aje kumtazama.

Kufika kwa mama Alma kukaongeza umati wa watu pale nje  ya nyumba ya Mzee Sagati, watu wakiwa wamesimama makundi makundi, wengine na majembe, wengine na magunia na makapu huku wengine wakiwa mikono mitupu. Baada ya kumtazama na kukitazama kidonda chake. Mama Alma alishauri mgonjwa apelekwe Zahanati haraka baada ya ile huduma ya kwanza aliyopewa.

Jerry akabebwa tena na safari ya Zahanati ikaanza. Msafara wa kumpeleka hospitali ulikuwa na watu sita. Mwenyekiti, Mama Alma, Nyanza na vijana wenzake watatu. Pale Zahanati alipokelewa na huduma zikaanza akiwa chini ya uangalizi wa Mama Alma muuguzi wa siku nyingi wa Zahanati ile. Mpaka saa mbili usiku, hali ya Jerry ilikuwa na nafuu kubwa huku mwili wake ukiwa umekunywa drip za maji na dawa za kutosha.

Asubuhi ya siku iliyofuata Mama Alma alimtaka binti yake aandae uji na kuupeleka hospitali kwa mgonjwa yule aliyeokotwa hapo kijijini. Alma alifanya kama alivyoagizwa na mama yake huku akimtafuta Sindi amsindikize uko zahanati. Saa moja baadaye Alma alimpitia Sindi na wakatoka pamoja kuelekea Zahanati.
Walipoingia ndani ya wodi aliyolazwa Jerry walimkuta Mzee Sagati akizungumza na Jerry ambaye sasa aliweza kuketi kwa taabu baada ya kurudiwa na fahamu muda mfupi tu uliopita.

Mzee Sagati alipomaliza kumuhoji alitoka kwa kupishana na akina Alma aliyemfuata Jerry kwa wasiwasi kidogo akionekana kumtazama kwa kuibia ibia. Alma alitua mfuko uliokuwa na chupa ya uji juu ya stuli ya wastani iliyokuwa kando ya kitanda cha mgonjwa.
‘pole…’ Alma alitamka kiuoga kwa sauti ya chini ambayo hakuwa na hakika kama ilisikika vyema au lah, akijaribu kujizuia kutabasamu na hapo hapo akitaka kutabasamu pia. Jerry akaitikia kwa kichwa, akiuma meno na kufumba macho kwa uchungu wakati akijitahidi kuketi vyema.

‘Nikumiminie sasa hivi?’ Alma akauliza akimuonyesha Jerry chupa ya uji na Jerry akaitikia kwa kichwa tena uso ukiwa bado na makunyanzi ya maumivu.
Alma akashughulika na uji wakati Sindi akiwa amesimama mbali kidogo na kitanda cha Jerry akiongea na mwanamke aliyekuwa amelazwa hapo na mtoto. Jerry alimtazama Sindi, ndio alikuwa amemuona wakati akiwa amesimama na Alma muda ule alipokuwa akiongea na Mzee Sagati, halikuwa hajamtazama vyema lakini sasa macho yake yalijaa nuru yenye nguvu ya kumtazama Sindi kwa kina.

kadiri alivyokuwa akizidi kumtazama Sindi ndivyo alivyojikuta akiyasahau maumivu aliyokuwa nayo ubavuni. Akashindwa kuvumilia alipomuona Sindi akicheka na kuzungumza na yule mtoto ngonjwa.
‘Yule binti ni nani?’ akauliza huku macho yake yakiwa kwa Sindi na  Alma aliyekuwa akihangaika kuupooza uji akageuka na kutazama kule alikokuwa akiangalia Jerry. Kwa tabasamu pana akageuza kichwa na kumuuliza Jerry ambaye alishindwa kuyaondoa macho yake kwa Sindi hata  kwa sekunde kadhaa

‘Nani Sindi?...’ Alma akauliza katika namna ya kupata uhakika
‘ Anaitwa Sindi?...huyo anayezungumza na mtoto’ Jerry akamnyooshea kidole Sindi na Alma akageuka tena kutazama kule alikoelekeza kidole. Akajibu kwa kutikisa kichwa
‘jina zuri’ Jerry akaunda tabasamu ambalo kwa wakati ule lilikuwa tabasamu la kwanza tangu akumbwe na masaibu ya dunia yaliyomkuta. Alma naye akatabasamu  huku akimkabidhi Jerry bakuli la uji. Akalipokea na kulipeleka mdomoni kwa taabu kidogo.

Sindi alimaliza mazungumzo na yule mama na taratibu akajongea mpaka kitandani kwa Jerry. Tabasamu pekee lilitosha kumfanya Jerry ajimwagie uji na hivyo kupiga ukunga wa uchungu na Alma akahangaika kumsaidia kuufuta ule uji uliommwagikia usifikie bandeji aliyokuwa amefungwa ubavuni.
‘oooh pole..’  Sindi alilipokea bakuli la uji wakati Alma akimfuta ule uji uliommwagikia. Kikafuata kicheko cha chini chini kati yao. Hali ilipotulia Jerry akamtazama Sindi usoni wakati akilipokea bakuli la uji na Sindi akakwepesha kwepesha macho kama mtu aliyepoteza kujiamini.

‘Sisi tunaondoka…atakuja nesi mama mtu mzima  na ndiye ataondoka na hivi vyombo’ Alma akatoa udhuru haraka sana akitaka yeye na Sindi watoke eneo lile.
‘Unaitwa nani?’ Jerry akamuuliza Alma ambaye alijikuta akicheka na asijue kilichomchekesha
Alma…’ akajibu huku aibu za kike zikimzengea na Jerry akaitikia kwa kichwa, pengine akitamani kuuliza maswali zaidi lakini ugeni ulimzuia. Hawa mabinti wakatoka nje ya wodi na kuanza kuondoka eneo la zahanati.
Kule ndani ya wodi Jerry aliuma meno tena wakati akijikunja na kulitua bakuli la uji juu ya ile stuli. Akashusha pumzi na kufumba macho
‘Sindi…’ akatamka kwa sauti ya chini lakini iliyojaa mwangi kichwani pake. Hakujua kwanini alikuwa amelitaja jina lile, alichojua lilimpa faraja kwa kiasi Fulani.
8888888888888888888888

Jijini Dar, familia ya Mzee Agapela ilikuwa katika hekaheka kubwa sana. Matumaini ya kupatikana kwa Jerry yalikuwa yanazidi kufifia siku hadi siku. Familia ilikuwa imeingiwa na kiwewe cha kutosha hasa baada ya kiatu chake alichovaa mara ya mwisho kuonekana pasipo yeye wala daliliza uwepo wake eneo lile kilipokutwa kiatu.

Mzee Agapela aliikumbuka vema asubuhi ya siku aliyoonana na mwanawe kwa mara ya mwisho. Alipita pale nyumbani kuwaaga kuwa alikuwa na safari ya kuelekea morogoro kikazi. Hakupitiwa hata na hisia kuwa safari ile ndio ingewaletea sakata kama lile. Alikuwa peke yake garini, pengine angelikuwa ameongozana na mtu labda ingelileta hali ya matumaini kwa kujua kwanza mwenzake yuko wapi.

Masaa sita baadaye gari lake liliokotwa pembezoni mwa barabara likiwa limeegeshwa na milango ikiwa haijafungwa, hakukuwa na dalili ya mtu ndani. Nyaraka za kazi na mizigo ya Jerry ikiwa kama ilivyokutwa na askari wa doria. Uchunguzi ulionyesha kulikuwa na kashikashi wakati wa kumuondoa eneo lile.

Hapakuwa na kijiji jirani wala dalili za watu kuweka makazi hata ya muda mfupi. Mazingira ya tukio lile yaliacha maswali mengi zaidi yaliyokosa majibu. Polisi walikuwa wakiendesha uchunguzi wako kwa kadri walivyoweza.

Ilishatimia wiki moja na siku kadhaa tangu Jerry Agapela aripotiwe kupotea jijini na yeye ndio alikuwa anatimiza siku ya nne tangu aokotwe pale kijijini. Tayari alishatoka zahanati na alikuwa akiishi nyumbani kwa Mwenyekiti. Usiku ule aliotoka hospitali Jerry alimweleza Mwenyekiti ukweli wa yaliyomtokea na kama binadamu Mwenyekiti alimpa nafasi Jerry ajipange kukabiliana na lile lililokuwa mbele yake.  Alimuonea huruma kijana huyu!

Jioni hii Mzee Agapela alikuwa ameketi sofani akiwa mwenye mawazo tele kichwani. Mkewe  alisimama mbali kidogo akimtazama na akitamani pia kujua kilichokuwa akilini mwa mumewe. Akatembea taratibu na kumfuata, akaketi kando yake na kumtazama mumewe kwa upendo
‘Unawaza mno mume wangu….polisi wamesema tusubiri kama ni watekaji si watasema wanalotaka’ mkewe aliongea polepole na Agapela akamtazama tu asichangie ile hoja wala kukubaliana naye

‘leo hujala tangu asubuhi…. kazi hazifanyiki….kila mtu ana hofu na uchungu ila ndio tumeweka imani yetu kwa Mungu…’ Mkewe alizidi kujaribu kumtia moyo na akatikisa kichwa kulia na kushoto bila tafsiri rasmi kuwa alikuwa anapinganana maneno ya mkewe au alikuwa akisikitika. Ukweli wa ishara ile ukabaki moyoni mwake. Akanyanyuka na kuondoka pale sofani akimuacha mkewe anamtazama mpaka alipotokomea.

Fiona, mke wa Agapela alisimama kwa kunyata na kuchungulia kwenye ngazi zilizobebana kuelekea ghorofani. Alisikilizia kwa muda na aliporidhika akashusha pumzi na kutoa simu yake iliyokuwa kwenye bukta aliyovaa ndani ya sketi yake. Kwa tahadhari akasogea kwenye kona huku akiwa na wasiwasi na kubinyeza namba kadhaa kwa haraka. Akaiweka simu sikioni, macho yakimcheza cheza na akizitazama zile ngazi mara kwa mara. Namba aliyopiga ilipokelewa

Mkono wa kushoto ulikuwa umeshikilia simu iliyokuwa sikio la kushoto hali mkono wa kulia ulikuwa ukiziba mdomo katika namna ya kuzuia sauti isisikike mbali na pale alipokuwa amesimama
‘Mmeshampata?...’ aliuliza kwa sauti cha chini akiwa na wasiwasi
‘….nini?....hebu kwanza nini…’ aliuliza kwa mshtuko, uso ukijaa ndita na macho kumtoka, wakati huo huo sauti ya kufunguliwa kwa mlango ikisikika ghorofani. Akaikata simu kwa kiwewe na huku akihema na kuirudisha alikoitoa. Akatembea kwa haraka kuzifuata ngazi,  akivifuta viganja vya mikono yake katika sketi ya kitenge aliyokuwa amevaa. Alitambaliwa na hofu, hofu ya kubumburuka kwa mpango wake. Hofu hiyo ndio iliyomfanya  asitazame alikokuwa anakanyaga na kujikwaa kwenye ngazi zile na kuserereka, akatua chini kwa kishindo. Huku akitumia jicho moja kuchungulia kule alikokuwa mumewe na hapo hapo akikunja uso kwa maumivu. Ikamdibi tu ajifanye ameishiwa nguvu ghafla kwa kutulia palepale chini alipoanguka.

Mumewe aliyekuwa akianza kuteremsha ngazi kueleka chini alimuona Fiona akianguka na hivyo akakimbizana kushuka na kumuwahi huku akimuita Jenifa binti yake aje kutoa msaada.
‘nini mama?....’ Agapela alihoji alipomfikia mkewe hali kadhalika Jenifa akitoka chumbani kwake mbio na kuja kusaidiana na baba yake.
‘Mama unawaza mno jamani….’ Jenifa alimlalamikia Fiona ambaye alijitahidi kulegea kadiri alivyoweza.
888888888888888888888888

‘a…e…i…o..u…haya anza tena…’ sauti ya Sindi ilisikika ndani kijumba kidogo cha udongo ikifundisha watoto kusoma na wao wakimfuatisha nyuma kwa sauti za kuvuta. watoto walikuwa wamekalia vitofali vidogo vidogo wakiwa na madaftari yao.
‘hamnisikilizi nitawachapa….mnaangalia nini uko nje’ Sindi aliwakemea wanafunzi walijikuta wakitazama sehemu moja kwa pamoja.

Akaguna na kugeuka kutazama uko walikokuwa wakitazama. Akakumbana uso kwa uso na Jerry aliyekuwa anatabasamu.
‘Oh! karibu…’ akamkaribisha na Jerry akacheka na kushukuru.
‘Hamjambo?’ akawasabahi wale watoto
‘Hatujambo… shikamoooo mwalimu’ wakaitikia kwa pamoja na kufanya Sindi na Jerry wacheke kwa pamoja

‘Marhaba watoto wazuri…’ Jerry alijibu akisogea zaidi na kuegemeza mikono yake iloe sehemu ya dirisha. Akaanza kuzungumza nao akiwachekesha hapa na pale na mwisho Sindi akaamua kufunga darasa na kuwaruhusu wanafunzi wake waondoke.

Alikusanya vitu vyake na kutoka nje ya kile chumba cha udongo, Jerry naye akiwa ameshazunguka toka kule dirishani hadi mlangoni
‘Wanakulipa?’ akamuuliza Sindi wakati akisindika mlango wa bati sehemu iliyotumika kama mlango
‘kiasi kidogo tu….’ akajibu akigeuka na taratibu wakianza kuondoka eneo lile kuelekea nyumba za wanakijiji zilipo. Walizungumza wakicheka na kutaniana hapa na pale. Jerry akionekana kumfurahisha Sindi kwa kila aliloongea.

Wakati wakikatiza sehemu yenye miti na pori dogo, Nyanza aliyekuwa akikata kuni aliwaona. Akajibanza kidogo na kuwachungulia namna walivyokuwa wakizungumza na kucheka. Jerry akimtolea iuchafu vya miti vilivyomdondokea kichwani wakati wakipita sehemu ile. Nyanza alitulia na panga lake mkononi, akihisi damu yake ikiongeza kazi mwilini, akihisi jazba zikianza kumtawala lakini akajipa nafasi ya kuwatazama wakipita eneo lile bila kuwabughudhi.

Wivu uliomtomasa moyoni ulimfanya amtazame Jerry kwa chuki pasipo hata kujua ni nini walikuwa wakiongea. Kitendo cha Sindi kuonekana mwenye furaha, akicheka na kushiriki mazungumzo yao kwa furaha kilimfanya Nyanza ahisi Jerry hakuwa mtu mzuri kwake. Alichomeka panga kwenye mzigo wake wa kuni na kuanza kuwafuatilia kwa kunyatia nyuma

…..FIONA ANA SIRI GANI?....HOFU YA NYANZA INAHISTAHILI?..... NI NINI KIMEMPATA JERRY?

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger