Sunday, March 17, 2013

SINDI....na LAURA PETTIE (2)

2
SINDI......NA LAURA PETTIE (2)

Asubuhi ya siku hii ilikuwa siku ya ibada kwa wakristo walioishi kijiji cha mzimbuni, Ndani ya kanisa lililoezekwa kwa mabati chakavu, ibada ilikuwa inaendelea na waumini walikuwa wamesimama wakiimba wimbo kwa kutumia vitabu cha nyimbo ambavyo vilionekana kumilikiwa na waumini wachache huku waliobaki wakiwa wamekariri beti za wimbo huo.

Mbele ya moja ya mabenchi ya mbao yaliyosimikwa ardhini alisimama mama yake Sindi, akifuatiwa na Peter kisha Sindi, Maria na Alma, marafiki wa Sindi pamoja na  bibi yake Sindi. Wakati waumini wengine wakikazana kuimba Sindi na marafiki zake walikuwa wakiimba huku nyuso zako zikionyesha wazi akili zao hazikuwa eneo lile.



Maria na Alma walicheka kichini chini na kukanyagana huku wakiibia kuwatazama Sindi na Nyanzambe aliyekuwa amesimama mstari wa katikati wa mabenchi akiwa na mama yake. Kwa vile alikuwa mbele kidogo, aliweza kugeuka na kumtazama Sindi kwa kuibia kila mara huku Sindi yake akimtazama na kukwepesha macho kila Nyanzambe alipoibia kumtazama na wakati huo huo wakiendelea kuimba wimbo uliokuwa ukiimbwa.

Kuibia kule kukakoma baada ya Mama yake Nyanzambe kumvuta mwanawe sikio katika namna ya kuchekesha na kumtaka aiweke akili yake katika kile kilichokuwa kinaendelea ibadani. Tukio lile lilifanya Maria, Alma na Sindi wacheke kichini chini kiasi cha kuwafanya Mama Sindi na bibi wawatazame mabinti hawa kwa mshangao na macho ya kuwaonya kuacha upuuzi wa kucheka wakati wa ibada.

Ibada ilipoisha, waumini walitoka nje, wakisambaa huku na kule kwa minajili ya kusalimiana, kutambulishana na wengine kuelezana hili na lile. Mama na Sindi pamoja na mama mkwe wake walikuwa na wakizungumza na akina mama watu wazima huku Sindi akiwa nyuma ya mama yake  na hapo hapo akitazama huku na kule, macho yake yakimtafuta Nyanzambe.

Alipomuona, alifungua kitabu cha nyimbo na kutoa bahasha kwa uangalifu, akainama kidogo na kumpatia Peter, akimuonyesha Peter mahali alipo Nyanzambe ambaye naye alionekana kutotulia kabisa akizungusha shingo yake huku na kule.
‘Haya twendeni!...’ Mama Nyanza alimsemesha kijana wake, huku akimuhimiza mdogo wake Nyanza kuangulia wakati huo akiwa ametoka ksalimiana na mchungaji aliyeendesha ibada hiyo. Nyanza akakunja uso na kugeuza shingo huku na kule

‘Nyanza!...’ mama yake aliita akisisitiza na akiwa ameshapiga hatua mbili tatu. Mdogo wake Nyanza alitabasamu akionekana wazi kujua kaka yake alikuwa akitafuta nini. Kwa unyonge akaanza kumfuata mama yake ambaye naye aligeuka na kuanza kuondoka. Alipogeuka tena nyuma akamuona Peter akimkimbilia na uso wake ukachanua kwa furaha. Peter alimfikia na kumpatia ile bahasha iliyokuwa imekunjwa kunjwa mno. Nyanza akaipokea haraka na kuitia mfukoni, akikipapasa kichwa cha Peter kama namna ya kumshukuru. Akakaza mwendo kumharakia mama yake.

Njiani wakati wa kurudi nyumbani, Mama Sindi alitoa duku duku lake akionyesha wazi kutofurahishwa na tabia ya Sindi.
‘naona umeanza kusahau maadili ya ibada…’ alisema Mama Sindi akigeuza shingo nyuma na kumtazama Sindi aliyekuwa bega kwa bega na bibi yake
‘Unamfundisha nini Peter…mnapocheka cheka kanisani kama mwehu…’ aliendelea kugomba na bibi yake Sindi akamtazama mjukuu wake na kutikisa kichwa
‘Mi najua alichokuwa anacheka’ Peter akadakia akitabasamu na kumtazama Sindi ambaye alimkazia macho kama onyo la kutosema alichotaka kusema
‘Alikuwa anacheka nini’ mama akauliza akiwa amemshika mkono Peter na safari ya kurudi nyumbani ikiendelea.
‘Niseme nisiseme?’ huku akifanya mbwembwe za kitoto akamuuliza Sindi ambaye aliendelea kumkazia macho. Peter akacheka kitoto na mama yake akimtaka aseme bila hofu

Mazungumzo yake yakakatizwa na mlio wa honi ya baiskeli toka nyuma. Wote wakasogea pembeni kuipisha ile baiskeli, na muendesha baiskeli akasimama kwanza kusalimiana na akina mama Sindi
‘wameleta mbegu za mahindi, unapeleka kitambulisho unapewa mfuko wa mbegu na mbolea gunia tatu…’ yule muendesha baiskeli akazungumza kwa lafudhi nzito yenye Kiswahili kibovu bovu mara tu baada ya salamu na Mama Sindi kumuuliza alipotoa magunia ya mbolea aliyopakia nyuma ya baiskeli

‘Wanagawia pale pale pa siku zote au ?’ Mama Sindi akauliza
‘wanatolea kwa mwenyekiti….kule ofisi za kilimo nasikia pamejaa maji…mamvua yaliyonyesha jana….maji mpaka kule sokoni…’ mwendesha baiskeli akaeleza zaidi na kufanya wote washangae.

‘Ile mvua ya usiku ndogo vile ndio maji yamejaa’ bibi yake Sindi alishangaa
‘yamejaa acha kabisa….tangu yule mzungu azibage mtaro wa maji na lile liukuta lake… mvua ikinyesha maji yote yanakusanyikia sokoni kule hadi ofisi ya kilimo….’ muendesha baiskeli sasa akapanda vizuri baiskeli yake

‘Haya bwana…ngoja na sisi tukaangalie….’ Mama Sindi aliagana na yule muendesha baiskeli ambaye alianza kunyonga baiskeli yake na kuishia
‘Sindi nenda nyumbani na Peter…mama hebu  twende tukaangalie kilichopo uko….tusije tukakosa hata mbegu tu na mvua ndio hizi’ Mama Sindi alitoa maelezo ambayo Sindi aliyapokea kwa kutikisa kichwa na taratibu wakatengana Sindi na Peter wakiendelea na safari huku Mama Sindi na mkwe wake wakigeuza walikotokea.
8888888888888888888

Sindi Nalela ni mtoto wa pili katika familia ya Mzee Nalela iliyobarikiwa watoto watano. Sega  Nalela akiwa mvulana na kifungua mimba, baada ya kuhitimu kidato cha sita alikuwa nyumbani akingoja kujiunga na chuo kikuu. Alishapata chuo jijini Dar es Salaam lakindi ndio kipato cha mzazi wake hakikutosha kumuweka mjini hata wa wiki moja sembuse kulipia gharama za usajili.

Alikuwa katika hati hati ya kukosa kujiunga chuo kwa kukosa pesa ya usajili uliokaribia laki tano ukiachilia mbali sehemu ndogo ya ada ambayo alitakiwa kulipia wakati akisubiri bodi ya mkopo imkamilishie ada iliyobaki na kumpatia pesa za kujikimu.

Sindi Nalela alikuwa mtoto wa pili, binti mzuri mwenye urembo uliofubaishwa na umaskini uliokuwa ndani ya familia yao. Pamoja na kuishia darasa la saba Sindi alifahulu kujiunga na kidato cha kwanza shule ya wasichana msalato lakini hakuwanikiwa kwenda shule kutokana na umaskini.

Alikaa nyumbani akilima pamoja na wazazi wake mpaka pale Mzee wake aliponyang’anywa shamba na uongozi wa kijiji baada ya sehemu kubwa ya mashamba ya wanakijiji kununuliwa na Mwekezaji wa kizungu bila wao wananchi kushirikishwa. Tangia hapo hata ile pesa aliyokuwa akiitegemea ingempeleka hata shule binafsi ilipotea kabisa, na Mzee Nalela alijikaba alivyoweza ili angalau amsomeshe hata Sega.

Pamoja kukomea darasa la saba, Sindi alitamani kusoma zaidi, alikuwa na ndoto ya kuwa nesi. Aliipenda kazi hii sana akivutiwa na mama yake Alma ambaye alikuwa nesi wa zahanati ya kijiji. Alipenda mavazi yake na kile kitambaa cheupe alichovaa kama taji kichwani. Alipenda alivyokuwa mkarimu na namna watu walivyomkimbilia palipotokea tatizo. Ndoto yake ya kuwa nesi ilipotea taratibu na baba yake aliponyang’anywa shamba bila fidia ndio kabisa ndoto ile ilipotea na kutoweka, hatimaye akakubali kuwa majaaliwa yake yalikuwa yanaishia pale.

Tatizo la Sega kukosa ada ya chuo ndio lililozaa shida kubwa kwake. Baba yake aliamua kumuoza kama mke wa tatu kwa Mzee mfanya biashara kijijini hapo, Mzee Dunia Hatia. pamoja na kuhitai ada mzee Nalela alikuwa na madeni mengi kwa Mzee Dunia hivyo kuyakamilisha yote walikubaliana kuwa amuoze binti yake kwa Mzee Dunia kwa mahari ya kusamehewa deni na shilingi milioni moja na laki mbili taslimu.

Kwa Mzee Nalela ambaye sasa alikuwa na kijishamba kidogo tu cha kulima mazao ya chakula, shilingi milioni moja ilikuwa pesa kubwa sana kwake. Angetoa laki sita za Sega na laki nne zingekuwa zake. Tayari alishapokea laki mbili na milioni moja ilikuwa ikimsubiri Mzee Dunia arejee toka safari na kumchukua mkewe na kisha kumalizia mahari nzima.

Sindi alitaka sana kaka yake arejee shule, alitaka sana kaka yake atimize ndoto zake lakini ukweli kwamba alipaswa kuliweka rehani penzi lake na kijana mwenzake Nyanzambe ulimuumiza sana. Alimpenda Nyanzambe mno. Uhusiano wao ulikuwa unatimiza mwaka sasa, wakipeana ahadi za kuoana na Sindi akuutunza uanawali wake kwa ajili ya Nyanzambe. Akimuahidi Nyanzam kuwa mwanaume wa kwanza na wa mwisho maishani mwake.

Ahadi hiyo ilishaanza kwenda mrama, furaha kati yao ilianza kupungua taratibu, Sindi aliumia sana kila alipotaka kumwambia Nyanza ukweli wa mambo ulivyo sasa si kama ulivyokuwa mwanzo. Alishindwa hata kumwambia kuwa mzazi wake alikuwa amemtafutia mchumba sembuse kumwambia kuwa sehemu ya mahari ilishalipwa.

Miezi michache iliyopita alikuwa ameanza kujitolea kufundisha watoto wadogo kusoma na kuandika. Wazazi wa watoto hao walimpati chochote walichokuwa nacho kama shukrani. Kiasi kidogo alichopata alikitunza kwa bidii na sasa alikuwa amemnunulia Nyanza shati zuri la mikono mirefu alilovaa kanisani na kiasi kilichobaki alikifunga katika bahasha na kuamua kumpatia mpenzi wake. Alimpenda sana Nyanza kama ambavyo Nyanza alimpenda Sindi. Walikuwa vijana wadogo tu waliopendana na kuwekeana ahadi ya kuwa pamoja, wakiwa wametoka katika familia za kimaskini na wote wakiwa wamekwama kuendelea na masomo sababu ya umaskini.

Baada ya Sindi kulikuwa na mabinti wawili Danze na Denzi waliokuwa mapacha na kisha kitinda mimba Peter. Hawa ndio walikuwa watoto wa Mzee Nalela. Mzee maskini aliyeweza kujenga nyumba ya matofali ya kuchoma iliyoezekwa kwa mabati mabovu yaliyositiriwa na nyasi pia. Mzee aliyepambana na maisha kwa kadiri alivyoweza mpaka hapo alipofikia. Akianza na kilimo, kuchoma mkaa na hatimaye kurejea katika kilimo sasa akilima mashamba makubwa ya watu kwa malipo ya mapatano.
8888888888888888888888888

Nyanzambe Festo Mugilagila alikuwa mtoto wa mjane, mtoto wa kwanza kati ya wawili wa mwanamke mjane ambaye mumewe aliuawa kijijini hapo na polisi akituhumiwa kuficha nyara za serikali. Pamoja kutumia akiba yake yote na kuuza sehemu ya mali zake kutafuta haki. Mama Nyanza aliishia kukubali kuwa haki ipo mbinguni tu si duniani!

Ndugu wa mumewe walimalizia sehemu ya mali zilizobaki na akajikuta akianza vibarua vya kulima huku akifanya biashara ya ndizi mpaka alipopata ajali ya kugongwa na pikipiki ndipo alipoachana na shughuli hizo na kupata kazi ya kufanya usafi nyumbani kwa mzungu mwekezaji aliyekuja kijijini hapo na kununua sehemu kubwa ya ardhi ambayo sasa ilikuwa inakodishwa kwa wanakijiji kwa malipo.

Hellena Mama yake Nyanza aliifanya kazi yake ya kuhudumia nyumbani kwa  Mzungu kwa juhudi zote na ndio kwanza alikuwa natimiza mwezi wa pili tangu aajiriwe. Kipato kidogo alichopata hakikutosha kumsaidia kijana wake hata mtaji mdogo hivyo Nyanza kama vijana wengine walikuwa wakilima mashamba yaliyokodishwa kwa pesa ndogo au nyakato zingine alivua samaki na nyavu za kukodi pia na kuwakaanga.


nyanza alitamani kupata pesa za kununulia nyavu au hata pesa ndogo ya kununulia ardhi ili alime au naye akodishe lakini kipato kilimpiga chenga. Alitamani sana kumtunza Sindi Nalela msichana aliyyeotwa na robo tatu ya vijana pale kijijini, msichana aliyesemekana kuwa mzuri zaidi kuliko wote kijijini, msichana aliyesemwa kuwa na nidhamu na utulivu kuliko wenzake lakini zaidi msichana aliyeonekana kuhangaika na maisha, mwenye kujiamini na mcheshi.

Wanaume wengi walimtamani Sindi, walimpenda, walimuota, walimfuata kwa mitego mbalimbali lakini Sindi aliweka wazi kuwa  alikuwa msichana wa mwanaume mmoja tu, na mwanaume mwenyewe alikuwa Nyanza, kijana masikini kabisa.

Kashikashi ya wanaume kumkimbizia Sindi, Nyanza aliiona na ilimuumiza kwa vile alihofu Sindi angemuacha na kukubali kuwa na mtu mwenye hali bora. Alijitahidi sana kutunza pesa aizopata ilia angalau amnunulie Sindi hata mafuta ya kujipaka lakini pesa haikukaa.

Mdogo wake alikuwa sekondari ya kutwa, nyumba waliyoishi lilikuwa kama banda na walikuwa wamepanga baada ya kutimuliwa na ndugu wa baba yake. kodi ya banda ilimtazama, mambo mengine yote yalimtazama. alimhurumia mama yake mno hasa kutokana na maumivu ya kifua aliyokuwa akilalamikia kila mara kutokana na ajali. Pesa za kwenda kufanya uchunguzi zaidi hakuwa nazo. Nyanza alipambana kiume na maisha lakini hakuwahi kuyashinda!

Jioni hii Nyanza alikuwa ameketi kwenye jiwe kubwa lililokuwa kwenye muinuko, akitazama mashamba na mapori madogo madogo yaliyokuwa yakionekana mbele yake. Alizitazama zile pesa zilizokuwa kwenye bahasha  na kutikisa kichwa. Alizihitaji sana lakini si kutoka kwa Sindi. Yeye ndio alipaswa kumpatia Sindi pesa kama ile na si kuipokea toka kwa mwanamke. Alihisi unyonge zaidi. Wakati Sindi alipomtumia ujumbe kuwa alikuwa na zawadi yake ambayo angempatia kanisani, hakuwazia hata kidogo kuwa zawadi ile ingekuwa pesa. Alitulia katika lile jiwe kwenye mlima mdogo  akiwa ameketi na kukunja miguu yake, akifanya mikono yake iliyoshika bahasha ililale juu ya magoti yake na kunyooka kwenda mbele.

Aliyatuiza macho yake akitazama mbele, mawazo yakimchota na kumletea uso wa huzuni zaidi. Alikuwa akimsubiri Sindi eneo lile na mara kadhaa aligeuka nyuma na kuchungulia kama Sindi angetokea.

jua lilishasogea na kujenga kivuli kilichoanza kulikaribisha giza, wakati akitabasamu kwa huzuni na kuanza kukiteremsga kile kilima akamuona Sindi akija kwa mbali akiwa anakimbia. Akakunja uso kwa mashaka ana yeye akiteremka kwa haraka na kuelekea kule alikokuwa akitokea Sindi. Sindi akamfikia, akihema na kutokwa na jasho jepesi na hapo hapo akinyoosha kidole kuonyesha upande wa kulia na kule kuhema kukimzuia kuzungumza.

‘Kuna nini Sindi…?’
Nyanza aliuliza kwa wasiwasi akimchunguza Sindi
Sindi akameza mate kwa nguvu na kushusha pumzi kwa mkupuo
‘Kuna mtu…kuna mtu sijui amekufa sijui amekutw ana nini…yuko kule tunakokutania wakati mwingine…’ Sindi aliongea akihema na hapo hapo akionyesha woga

‘Mtu!....unamjua?’ mamcho yalimtoka Nyanza
‘Simjui….sijawahi kumuona maeneo haya….nilidhani uko kule ikaamua kuanzia kule ili nikikukosa nije huku…wakati natoka pale ndio nikaona nyasi kama zimeingia ndani hivi…’ Sindi akaonyesha namna alivyoona nyazi zimelala katikati ya eneo lenye nyasi ndefu
‘…hebu twende’ nyanza akasema haraka bila kungoja maelezo mengine ya Sindi. Wakaondoka wakikimbia kuelekea eneo la tukio. Walipofika Sindi akamuonyesha mahali mwili wa mwanaume wa rika lao tu ukiwa umelala kiubavu ubavu katika nyasi. Nyanza akanyata na kumchunguza kwa mbali na nyuma yake Sindi akichungulia.

Nyanza akaokota kipande cha mti na kukinyoosha kumgusa nacho yule mwanaume. Akaligusa bega na kumsukuma kwa nguvu kidogo akitumia kile kipande cha mti ili apate kuuona uso wa yule mtu. Yule mtu akateleza kidogo na uso wake ukaonekana, Macho yake yakifumbuka taabu na kuwatazama akina Nyanza.
‘uwiiii….’ Sindi akaruka kwa woga kama mtu aliyetambaliwa na nyoka huku Nyanza akitupa kile kipande cha mti na kumvuta Sindi mbali na eneo lile. Wote walitembelewa na wahaka, wakapatwa na kiwewe kwa dakika nzima walisimama wakitetemeka na kutazama sehemu aliyolala kijana yule kwa wasiwasi na woga.

Aliyelala pale chini alikuwa Jerry Kristus Agapela. Mtoto wa balozi mstaafu na Mkurugenz wa kampuni ya mafuta. Agape Oil!


NI NINI KILITOKEA MPAKA JERRY KUWA KATIKA HALI ILE?….

JE SINDI ATAMUACHA NYANZA ILI AOLEWE NA HATIMAYE KAKA YAKE ASOME?

USIKOSE SEHEMU IJAYO!.....NIACHIE MAONI

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger