Friday, March 15, 2013

SINDI.....NA LAURA PETTIE (1)

1


 Giza jepesi lilikuwa limegubika sehemu kubwa ya kijiji cha Mzimbuni, miale ya moto, taa za kandili, mishumaa pamoja na vibatari ilikuwa ikionekana hapana pale huku ikichagizwa na mwanga hafifu wa mbalamwezi. Hali hii iliashiria kuwepo kwa pilika pilika huku na kule.

Watoto walikimbizana na kupigizana kelele za kimichezo, Wanaume wa kila rika wakiwa wamejikusanya mahali wakizungumza na wengine wakipata pombe za kienyeji huku wanawake na mabinti wakiwa makini na shughuli za upishi katika nyumba zao. Ndege wa usiku hawakuacha kupiga miluzi na kuleta hali ya kuvutia, hali ya kijiji, hali ya maisha ya ujamaa.



Umbali mfupi  nje kidogo ya eneo lile la kijiji, kijana wa rika la kati anaonekana akiyumba na kutembea kwa shida. Mikono yake miwili ikiwa imeshikilia ubavuni, ubavu unaovuja damu na kumpatia kijana yule maumivu makali kupindukia. Anaonekana kulowa jasho pamoja hali ya ubaridi iliyokuwepo eneo lile. Anayumba akikwepa matawi ya miti iliyokuwa inaning’inia hali kadhalika akijaribu kulifikia eneo lenye miale ya moto aliyokuwa anaiona kwa mbali  toka pale alipokuwa.

Akasimama kwanza akihema kwa sauti na kwa kutumia mdomo, hali kadhalika akiinama na kusikilizia maumivu aliyokuwa nayo ubavuni. Alionekana wazi kutoweza kushindana na ile hali zaidi. akagugumia uchungu akitoa mkono mmoja toka pale ubavuni na kuutazama akiwa amepinda mgongo vile vile. Aliutazama mkono wake uliokuwa umejaa damu tupu ukitetemeka mbele yake, akafumba macho kwa uchungu na kuurudisha kushikilia  ubavu ule uliokuwa na jeraha

Akajiinua kidogo ili aweze kusonga mbele lakini lakini maumivu yalimzidia na akajikuta akiserereka kidogo na kuishia kushikilia tawi la mti ili asidondoke. Kishindo cha kuserereka kiliwafikiwa mabinti watatu waliokuwa karibu na eneo lile. Mmoja akivaa nguo zake baada ya kujisaidia haja ndogo na mwingine ndio akiwa amechuchumaa. Kishindo cha kuanguka kwa kijana yule kilimfanya yule aliyechuchumaa aruke sambamba na wale wenzake ambao walikuwa akimsubiri yeye.

‘Ni nini?’ yule aliyekuwa akivaa nguo ya ndani aliuliza huku yule aliyekuwa anajisaidia akikazana kupandisha nguo yake na kujibu ‘Sijui….’ wakati huo mwenzao akikaza shingo kuangalia upande mwingine kabisa

‘Mi narudi bwana….kama unamngoja Nyanzambe wako we mngoje…’ yule binti wa kwanza alimsemesha binti aliyekuwa akiangaza upande mwingine
‘Jamani msiondoke….atafika sasa hivi?’ aliwasihi wenzake
‘hicho kishindo umekisikia lakini?.... tuje kuliwa na simba vichochoroni kisa mchumba’ako kha!’ akaanza kugeuka na binti aliyekuwa akimsubiri mpenzi wake akamuwahi na kumshikilia huku yule mwingine akicheka, naye akiwa amemshikilia yule aliyetaka kuondoka.

‘Sasa akija akanikosa je?’ akauliza kwa wasiwasi shingo ikiwa imegeukia kule alikotarajia Nyanzambe angetokea
‘bora kipi…akukose hapa akuone kesho au akukose hapa akute umeliwa na simba’ aliuliza yule msichana aliyekuwa ameshikiliwa na wenzake na yule binti akakosa jibu. Uso wake ulionyesha wazi alitaka kumsubiri huyo aliyekuwa akimsubiri lakini pia hofu ya kubaki pale peke yake ilimsumbua.

Ukimya mfupi tu uliopita kati yao ulifanya kishindo cha pili cha kuanguka kwa yule kijana kiwafikie barabara na hapakuwa na mjadala tena. Walitoka mbio kila mtu akitafuta nafasi ya kuchanja mbuga kuliko mwenzake. Wakakimbia na kukutana nyuma ya nyumba na kusimama hapo wakihema na kucheka kimya kimya, mikono ikiwa kifuani.
‘Hivi ni nini?’ mmoja akauliza akiwa ameinama na kushika magoti huku akihema
‘Sijui…’ akajibu mwingine akitikisa kichwa hali kadhalika yule mwingine akitoa macho kwa woga na kutazama kule walikotokea

‘Sindi ingia basi tuondoke wenzio…’ yule aliyekuwa ameinama akamharakisha yule aliyekuwa na hofu, Akimtaka afungue dirisha la mbao la ile nyumba. Sindi akalifungua na wenzake wakamsaidia kumnyanyua na kumsukumizia ndani. Puh! akaaanguka kama mzigo na wenzake huku nje wakatazamana na kucheka huku wakifunika midomo kwa viganja vyao. Wakaondoka eneo lile kwa kunyata.

Sindi aliokota vitu alivyogonga na kuangusha wakati aliposukumiwa ndani na wenzake. Mwanga wa kibatari uliokuwa juu ya stuli ndogo chakavu ulimtosha kuweka sawa eneo lile. Akajifunga khanga yake vizuri na kurekebisha kilemba. Akatoka mule chumbani na kutokezea sebuleni kulikokuwa na wadogo zake waliokuwa wakifanya kazi za shule wakiwa wameketi chini na kuizunguka meza ndogo katikati yao. Akapita kwa mwendo wa haraka na baba yake aliyekuwa anasoma kitabu akamtazama juu ya miwani aliyokuwa akisomea kisha akaendelea kusoma kitabu chake.

Sindi akaingia jikoni na kumkuta mama yake akisonga ugali kwa juhudi zote kwa kutumia mikono miwili. ugali ulikuwa mkubwa na jiko lilikuwa la kuni. Ilimpasa kukanyaga sufuria la ugali kwa utumia miguu yake yenye ndala ili aweze kusonga kwa ufanisi.

Sindi alipoingia jikoni mama yake akasonga kidogo na kuachia mwiko, akivuta uoande wa khanga na kufuta jasho. akashusha pumzi kwa nguvu zote na kumtazama binti yake aliyetembea kinyonge na kwenda kuketi kwenye kigoda mbele ya yale mafiga aliyokuwa akitumia mama yake.

‘haya nini…’ Mama yake akamuuliza, akijua wazi kulikuwa na linalomtatiza mtoto wake
‘sitaki kuolewa…’ akajibu na kutazama pembeni na mama yake akatabasamu na kuirudia shughuli ya kusonga ungali uliokuwa umeanza kuungulia. Akasonga kidogo na kuipua sufuria la ugali
‘nipe hilo sufuria la samaki hapo chini’ mama yake akamsemesha akimuelekeza lilipo hilo sufuria. Sindi akanyanyuka na kulifuata, akalileta na kulibandika. mfuniko ulikuwa juu ya sufuria la samaki ukafunika ugali. Mama yake akamtulizia macho

‘husomi…umri wako unaruhusu…kwanini usifurahie ngekewa iliyombele yako Sindi?’
‘Mama….’ Sindi akaita kwa msisitizo akinyanyua mabega yake na kuyashusha chini
‘….basi angekuwa mtu ninayempenda’ Sindi akalalamika na mama yake aliyekuwa akitazama samaki kwenye lile sufuria, akanyanyua uso ukiwa na ndita kadhaa na kumtazama binti yake

‘Nyanzambe!?’ mama yake akatamka katika namna iliyomshinda Sindi kung’amua kama lilikuwa swali au mashangao. Akabaki kumtazama mama yake kwa uso uliojaa masikitiko. Mama akatikisa kichwa kulia na kushoto akisonya kidogo na kutazama nyuma yake kulikokuwa na kishindo cha kiguu. Akatokezea Peter mdogo wake Sindi. Akiwa anatafua kalamu yake mdomoni

‘…Mama baba anauliza mbona chakula hakifiki mezani?’
‘Baba au wewe ndio una njaa….kamuamshe bibi…naleta chakula sasa hivi’ Sindi akamjibu mdogo wake ambaye aliukusanya mdomo wake na kuupindisha kando akidhamiria kumdhihaki Sindi

‘Peter!...nikikushika ntakuchapa’ Sindi alikarahishwa na ile dhihaka, akavua ndala yake na kumtupia Peter aliyekuwa ameanza kukimbia kurudi sebuleni. Mama yao aliwatazama na kucheka. Shughuli ya kupakua chakula ikaanza na nusu saa baadaye walikuwa wakipata chakula cha usiku. Baba akiwa na ameketi kwenye kiti cha mbao na meza mbele yake ikiwa na sahani ya ugali na bakuli la samaki na samaki mzima ndani yake.

Kulia kwake, Mkewe mama Sindi, mama mkwe wake mama Sindi, Sindi na wadogo zake wa kike wawili na mmoja wa kike walikuwa wameketi kwenye mkeka wakishea ugali kwenye sinia na vipande vya samaki kwenye bakuli. Kushoto kwake kulikuwa na kijana wa makamo naye akiwa ametengewa chakula kama baba yake Sindi. Alikuwa Sega kaka yake Sindi.

Chakula kililika kimya kimya huku redio iliyokuwa imenyanyunyiwa mkonga wake katika kutafuta stesheni ikisoma taarifa ya habari.
‘Peter baba mate hayo jamani….unakula samaki mbona hugusi ugali’ Mama Sindi alimsema mwanawe wa kiume na kufanya waliokaa mkekani kucheka kichinichini kana kwamba hawakutaka kuonekana wakicheka wakati kula.
88888888888888888888888

Kulipambazuka, anga likitakata kwa mawingu machache na ugavu wa bluu wenye kupendeza. Ndani ya jiji la Dar es Salaam katika moja ya maghorofa Masaki kulikuwa na hali ya kukosa utulivu. Mwanamke aliyekuwa ameketi sofani alionekana kutoka kulia muda si mrefu na bado alikuwa akipangusa machozi na kujaribu kutulia kama vile mumewe alivyokuwa akimuasa akishirikiana na binti yao aliyekuwa kando yake.

Mlango wa sebuleni ukafunguliwa na polisi watatu wakaingia mmoja akiwa amevalia kiraia na wengine wakiwa na sare. Yule aliyevaa kiraia alikuwa na radio call mkononi pamoja na faili dogo. Mzee Kritus Agapela akasimama haraka na kusabahiana na yule polisi aliyevaa kiraia, akiwapuuza wale wengine.

Mke wa Kritus na binti yake nao wakisimama na kumsogelea yule polisi
‘aah..mmm…bado hatujapata fununu zozote za aliko kijana wako ila…tumepata kiellezo ambacho nadhani kinaweza kutupa mwanga wa kujua anaweza kuwa sehemu gani…’ Polisi yule aliongea taratibu na wasikilizaje wake wakimtolea macho kwa hamu kubwa ya kusikia alichotaka kusema

‘….tumefuatilia kule alikoanzia safari na inaonekana itakuwa amjeruhiwa kidogo….mpaka sasa tuna kiatu ambacho kinakuja na kikifika tutawataka mkitambue kama ni chake…naaa…’ wakati akivuta sentensi yake ili kupata neno la kumalizia sentensi yake Mzee Kristus alionyesha hali ya kukereka zaidi
‘Stupid!....nimeshindwa kufanya shughuli zangu…..kila kitu kimesimama kwangu….. familia hailali usingizi sababu ya suala hili na wewe unaniletea habari ya kutambua kiatu?....kiatu?...Inspekta?’ Mzee Kristus alifoka kwa ukali

‘Mzee tuna…’ alikatishwa tena
‘Sijali mnaleta kiatu ama bukta….i need my Son! ….my son!...sio habari za viatu….sikuja kufungua jalada la kupotelewa na kiatu polisi…. it is Jerry!...aliyepotea ni Jerry Kristus Agapela sio ndala wala raba…’ akaondoka kwa mwendo wa jazba akiishia ndani na kuiacha familia yake ikimtazama Inspekta kwa huzuni.

Yule polisi akaaga kwa unyonge kidogo, akiwa amefadhaishwa na majibu ya Mzee  Kristus. Alikuwa akifanya kazi usiku na mchana akimtafuta kijana huyu aliyepotea katika mazingira ya kutatanisha. Mzee Kristus alihitaji taarifa za kila hatua na kila alipopewa taarifa hizo hakuonyesha kuridhishwa na nguvu iliyotumika kumsaka kijana wake.

Akaondoka na kumuacha yule mama na binti wake wakifarijiana kwa huzuni…..

…..SAFARI IMEANZA UNGANA NAMI KATIKA  SIMULIZI HII…..





1 comment:

  1. Siwezi kusema lolote kwa sababu ndiokwanza mwanzo ila inaonesha mwanzo mzuri nategemea itakua nzuri kuliko karata tatu nitafurahi sana ikiwa hivo

    ReplyDelete



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger