Friday, January 10, 2014

SINDI .....NA LAURA PETTIE (52)

52

Fiona Agapella akaweka ndita kadhaa usoni na akili yake ikilikumbuka tukio moja lililotokea hivi karibuni, ingawa hakulipa uzito tukio hilo kwa wakati ule lakini kwa sekunde hizi mbili tatu tukio lile lilikuja na uzito wa tani za kutosha kutikisi mbuyu.!


Akaikumbuka barabara siku hiyo aliyomtembelea Iloma kazini kwake, na wakati wakiongea hili na lile akaingia kijana aliyekuwa amevalia t-shirt yenye maandishi ya kampuni moja ya usafirishaji vifurushi. Akamuulizia Iloma na alipoelekezwa alipo akamkabindhi kifurushi kilichokuwa kimefungwa kiustadi. Iloma akasaini na kukipokea.

Alionekana kukifurahia kifurushi kile lakini hakuonyesha shauku ya kutaka kukifungua pale muda ule na Fiona hakuwa na wazo la kutaka kujua ni kitu gani na kilitoka wapi, ila kwa muda huu akili ya Fiona ilijaa shauku ya kukiona tena kile kifurushi. Akanyanyuka kwa mwendo wa haraka na kuanza kupekua huku na kule. Alihama droo moja hadi nyingine, kisha akaingia kabatini ambako pia aliambulia patupu.

Akasimama akiwa amejishika kiuno, akili yake ikiendelea kumshawishi azidi kukitafuta hicho alichokuwa anakitafuta. Akaiongoza miguu yake mpaka kwenye kordo moja chumbani hapo kulikokuwa na boksi kubwa lililobeba sanduku moja juu yake. Akalishusha sanduku lile na kulifungua lile boksi. Shabash! alichokuwa anakitafuta kilikuwa ndani ya lile boksi.

Akakitoa na kurudi nacho kitandani, akiharakisha kukifungua kwa shauku ya kutosha. Akaachama mdomo na kutoa macho. kulikuwa na hereni zilizofanana na mkufu vyote kwa pamoja vikiwa rangi ya fedha na kunakshiwa kwa kito cha almasi. Fiona akaweweseka sasa akitoka tena mbio na kulifuata sanduku lake dogo na kulifungua. Akatoa mkebe mwingine uliofanana vile vile na ule aliokuwa ameutoa katika boksi na vidani vilivyokuwa ndani vilikuwa vya kufanana.

Akahisi kitu kama kichomi kikimgonga moyoni, hakikuwa kiyu cha kawaida vitu kufanana namna hii. Akapata akili ya kurudisha kila kitu mahala pake na kisha kusimama mbele ya ile dressing table akijitazama na akili yake isitambue kwanini alisimama pale akijitazama. Hata ile dhamira yake ya kusafisha kucha ilipotelea mbali na kumuacha akiwa haelewi ni kipi alipaswa kufanya muda ule.

Akiwa amezama mawazoni, mlango ukafunguliwa na Iloma akaingia akitabasamu
‘Nilijua umeshatoka’ akamsemesha Fiona akikifuata kitanda na kuutua mkoba wake. Pengine alitarajia Fiona angelijibu chochote kuendeleza mazungumzo lakini haikuwa hivyo. Fiona alikuw anamtazama  tu kana kwamba alikuwa akigeuka kuwa kiumbe cha ajabu taratibu.

Iloma akakunja uso kidogo na kumtazama Fiona kwa mshangao
‘Fifi!...’ akamuita kwa upole akianza kumsogelea. Fiona hakujibu kitu ni kama vile akili yake haikuwa pale muda ule

‘nin kimetokea?’ Iloma akauliza tena akiwa ameshamkaribia rafiki yake na kuendelea kumdadisi. Kama mtu aliyerudiwa na akili alishusha pumzi na kumtazama Iloma usoni
‘Unawasiliana na Kristus?’ akamuuliza Iloma ambaye alitanua macho yake kwanza na kurudisha kichwa nyuma huku kuguna katika namna na kushangaa kidogo

‘Kristus?’ iloma akauliza akiwa bado anashangaa
‘Agapella!’ Fiona akarahisisha swali lake akiwa bado amemkazia macho Iloma
‘No!... sijaongea naye tangu siku ile uliponituma’ Iloma akajibu naye akimtazama Fiona kwa udadisi
‘Una uhakika?’ Fiona akawa kama haamini ile kauli ya Iloma
‘Sasa nikufiche ili iweje au itanisaidia nini mimi… wait!...’ iloma akageuka kwanza akimpa kisogo Fiona na kufumb amacho kwa nguvu mno kana kwamba alitaka kujiweka sawa kabla ya kumgeukia tena Fiona.

Alipogeuka akamtazama Fiona na kumrushia swali kali sana
‘unadhani nawasiliana na Agapella kisirisiri?’ Iloma akagonga mfupa wa swali na kumnyong’onyeza Fiona
‘Simaanishi hivyo’ Fiona akababaika kwa vile nia yake ilikuwa imewekwa wazi ghafla na yule yule aliyetaka kumtuhumu

‘Sasa una maana gani kuniuliza kama nawasiliana na Agapella?... Fifi kama umefikia hatua ya kuniwazia hivyo ni bora urudi kwa mumeo kabla hatujakorofishana vibaya’ Iloma akaja juu kidogo

‘Sijakutuhumu Iloma… nimeuliza tu’ Fiona akajitetea akimpita Iloma na kwenda kusimama nyuma ya Iloma naye iloma akapiga hatua moja mbele na kumgeukia Fiona wakawa wamebadilishana nafasi za kusimama
‘hakuna swali lisilo na sababu Fiona…. ndio maana tangu mwanzo nilikataa kujihusisha na huu usuluhishi’ Iloma akajitetea

‘What about vidani ulivyonavyo kuwa sawa na nilivyonavyo?’ Fiona akaona aweke wasiwasi wake kweupe.
Iloma akamtazama Fiona kwa sekunde kadhaa pasipo kuwa na jibu. Akili yake ilichemka maradufu na kumtafutia jibu la kujitetea. Akalipata!

‘Una nguo ngapi zinazofanana na zangu?... au ni wewe tu unayestahili kuwa vidani?... what if nimemwambia mpenzi wangu aninunulie vidani vilivyonivutia toka kwako… hilo ni kosa?’ Iloma akauliza akianza kuona ujinga wa mazungumzo yale na hatari iliyo mbele yake.

Fiona akakubali kushindwa
‘Okay!... samahani kwa kukufikiria vibaya’ akajibu akiifuata pochi yake na kutoka. Iloma akashusha pumzi kama mtu apigaye mluzi na kukifuata kitanda kwa unyonge. akaketi hapo akipepesa macho kama mtu aliyenusurika kufumaniwa katika hatari. Akahema kwa nguvu, mabega ayakipanda na kushuka. Mpaka dakikaile tayari alishakutana kimwili na Kristus Agapella na akakiri moyo ulishafunguka kwa mzee huyu!
Fiona alichomtendea Marehemu Sophia mama wa Jerry na Jenifa, mke mkubwa wa Mzee Agapella ndio kilichokuwa njiani kumkuta yeye mwenyewe kupitia rafiki yake kipenzi Iloma! Je ataujua ukweli na akijua atafanya nini?
888888888888888888888

Dennis Mazimbwe ana mkewe Daniella walitoka ofisini na kuanza kuifuata kordo iliyokuwa inaelekea mapokezi. Dennis alikuwa ametangulia hivyo ilikuwa rahisi kwake kumuona Rebecca Okello aliyekuwa mapokezi pale mbele ya meza ya sekretari. Meza ya sekretari alikuwa upanze wa kushoto mara tu umalizapo kordo na kuingia mapokezi na vile Dennis alitangulia hamaniko alilolionyesha usoni lilimfahamisha Rebecca moja kwa moja kuwa hali haikuwa shwari.

Akazunguka ule upande wa sekretari ghafla na kuingia miguuni pa sekretari akiusahau mfuko mdogo aliokuwa ameuweka miguuni pake wakati akiongea na sekretari yule ambaye alikuwa bado hajaelewa kilichokuwa kinaendelea.

Dennis akafika mapokezi pale na mkewe Daniella akawa wa kwanza kuongea na yule  sekretari akimtania na kumuuliza hiki na kile. Daniella alisimama pale alipokuwa amesimama Rebecca hivyo mfuko ule aliouacha Rebecca pale chini ulikuwa kando yake.

Rebecca kule chini akahisi ule mfuko ungeleta balaa akanyoosha mkono na kutambaza taratibu sakafuni akiufuata ule mfuko ili aufiche kule chini alikokuwa amejificha na bahati mbaya mkono wake hakufikia kile kimfuko zaidi ya kuishia kukanyagwa na Daniella aliyekuwa  anasogea mbele ili achukue kikaratasi kilichoonekana kumvutia pale mezani.

Daniella alihisi kukanyaga kitu. Akatazama kule chini na kuuona ule mfuko na asijue kulikuwa na mtu kule chini akiugulia maumivu ya kukanyagwa na ko ko ko yake.



‘Naona kuna mteka amesahau mfuko wake hapa chini’ Daniella alisema akitaka kuinama ili auokote. Rebecca akapiga ishara ya msalaba huku akipuliza vidole vyake na Dennis akamuwahi mkewe na kuuokota ule mfuko kwa vile alijua kuinama kule kungemfanya amuone Rebecca.

Akafanya jitihada zote za kumuondoa Daniella pale na kwenda naye nje. Rebecca aliposikia mlango umefungwa akajitoa kule chini na wakati akimalizia kutoka akajigonga kichwani kwenye ile meza ya sekretari.

Akalaani, akapuliza vidole na kusugua alipojigonga na Sekretari yule akajizuia kucheka akinyanyuka na kumuomba asubiri akamtafutia barafu akande vidole. Kule nje Daniella na Dennis waliingia garini na Dennis akadai amesahau funguo za gari ofisini. Akamuomba Daniella amsubiri nay eye akatoka mbio na kurudi ofisini, pale mapokezi.

Alimkuta Rebecca akifungwa na sekretari kitambaa kilichokuwa na barafu. Dennis hakujali pengine kwa kutojua ni nini kilikuwa kimemkuta Rebecca. Aliukwanyua mkono wa kushoto wa Rebecca ile sehemu karibu na kwapa na kumburuza kama mtoto. Akafungua mlango wa ofisi na kumtupia ndani Rebecca kabla ya yeye kuingia na kufunga mlango.

‘nitaongea hili kwa mara ya kwanza na ya mwisho Becca’ Dennis alifoka sasa
‘…. usikanyage ofisini kwangu bila kunipigia simu Rebecca’ akaotoa onyo
‘umeanza kuniwekea masharti Dennis?!’ Rebecca hakuamini kauli ile kauli
‘kuna wakati  utumie akili kufikiri… Daniella ni mke wangu na anafika hapa wakati wowote… wakati huu si sawa na wakati alipokuwa hayupo… huelewi nini?’ Dennis aliongea kwa haraka na msisitizo kuonyesha kukerwa na Rebecca

‘Kwanini yeye usimzuie kufika hapa kama unavyonizuia?’ Rebecca naye akauliza na kumfanya Dennis atamani kumnasa kibao ili angalau aone hatari anayoiona yeye kwa kufika kwake pale bila taarifa.

‘… hebu kuwa busara Becca... Daniella amekusheshimu sana kwa kujua kinachoendelea bila kumfikishia mumeo… angalau mpe heshima yake kama mke wangu wa ndoa… sipendi upumbavu’ Dennis sasa aliangalia nyuma kwa wasiwasi akirudi nyuma kukishia kitasa tayari kwa kutoka. Alihisi Daniella angemfuata nyuma

‘Lakini ulisema utamtaliki hivi karibuni…’ Rebecca alikuwa bado na hali ya kutoamini Dennis alikuwa anamgombeza vile kama mtoto
‘ni mpaka hapo hiyo karibuni itakapofika kwa sasa usikanyage ofisini kwangu bila taarifa vinginevyo utanipoteza’ akatishia Dennis na kushika kitasa cha mlango

Sekretari alikuwa akisikiliza mazungumzo yao mlangoni na alipoona kitasa kinacheza akageuza miguu haraka kurudi mapokezi lakini hakupiga hatua nyingi Dennis alishatoka na akamshangaa kumuona sekretari wake pale kordoni. Yule dada akavunga kuulizia hiki na kile lakini Dennis hakumsikiliza akampita na kuishia zake.

Binti akabaki kordoni akitazama ule mlango wa ofisi ya Dennis, pengine alitarajia Rebecca angetoka, kinyume chake akasikia kitu kikipasuliwa kwa nguvu zote. Akaharakia kwenda kule ofisini kwa Dennis, fremu yenye picha ya Daniella iliyokuwa mezani pa Dennis ilikuwa imesambaa kila kona. Wanawake hawa wawili wakatazamana tu mmoja akiwa na mshangao na mwingine akiwa na hamaniko!
88888888888888888888

Sindi Nalela alikuwa akibubujikwa na machozi wakati Tima alipokuwa anangoja jibu la swali lake kwa mara ya pili tangu aliulize.
‘Upo tayari?’ akarudia tena lile swali kwa mara ya tatu na Sindi akaitikia kwa haraka kama mtu aliyekata shauri ya liwalo na liwe.

‘Nimeshakwambia inataka uvumilivu na narudia tena kama kweli unataka huyu mtoto azaliwe itakupasa kuvumilia yote kwa kipindi cha miezi mitano iliyobaki… uko unakoenda hakuna raha wala starehe yoyote… na sitaki kukuficha kuwa kuna maisha ya unafuu… ni vile tu unahitaji kumuokoa huyo mtoto… ila kama huwezi ni bora ukubali tu kuiondoa hiyo mimba na maisha yaendelee’ Tima aliongea taratibu, akitaka Sindi amuelewe na akiweke akilini kile alichokuwa akiambiwa kwa wakati ule

Sindi aliitikia tu na mara kadhaa akigeuza uso wake na kumtazama Nadina aliyekuwa ameketi kando yake akijaribu kumfariji na kumpa nguvu.

‘Nani atakuwa anaenda kumuona sasa?’ Nadina akamuuliza Tima
‘nitaenda usiwe na hofu… mradi tu Sindi aniahidi atavumilia na kamwe hatachukua uamuzi kinyume na huu tuliokubaliana’ Tima akatoa maelezo ambayo kwa kiasi Fulani yalimpa Nadina matumaini ingawa moyo wake ulijaa mashaka mengi mno. Kuna maswali alijiuliza pasipo kupata majibu lakini hakutaka kuyauliza kwa uwazi akichelea kuonekana mjuaji.

Jioni ilipoingia, Sehemu kubwa ya jengo la danguro ilikuwa kimya. Vijakazi vilikuwa vikitumikia mabwana ndani ya vile vyumba. pur
ukushani chache zilikuwa kule kwenye casino ambako kwa siku kama hii ya mwisho wa wiki kulikuwa kunajaa watu wenye fedha zao. Sindi na Nadina walitazamana kwa sekunde kadhaa na kukumbatiana, kila mmoja akilia. kuna kitu mioyoni mwao kiliwaumiza ni kama vile ilikuwa mara ya mwisho kwao kuonana na kamwe wasionana tena baa da siku ile.

Wakalia kwa uchungu, kwa muda mfupi waliokaa pamoja walikuwa kama ndugu, walipita dhoruba pamoja na walipofarijika walicheka pamoja lakini sasa iliwapasa kutengana na mmoja wao alikuwa akielekea kusikojulikana. Waliumia!

Nadina akavua rozari yake na kumvalisha Sindi
‘utakapohisi upweke itazame rozari hii… itakufariji’ akaongea akiushika ule msalaba wa rozari na kumtazama Sindi usoni.
‘Sijui ninakokwenda…’ Sindi alisema kwa kwikwi na kuongea kwa mara ya kwanza jioni ile. Alikuwa kimya kwa muda mrefu sana akionekana mwenye mawazo na mara kadhaa akilia kimya kimya.

‘imetosha sasa… twende sindi’ Tima aliwaachanisha na kumshika mkono sindi akimuongoza sehemu iliyokuwa na nyasi nyingi. Sindi alitembea kichwa kikiwa kinatazama nyuma kule alikosimama Nadina ambaye naye alitembea kumfuata Sindi huku akilia, akamfuata mpaka alipopotelea kwenye zile nyasi na kusikia geti dogo likifunguliwa. akafumba macho na kuruhusu machozi zaidi

akalia, akalia peke yake, kwa dakika alizosimama pale alihisi dunia ilikuwa imemgeuzia mgongo tena kwa mara nyingine. Mtu aliyemuona kama ndugu alikuwa ameondoka maishani mwake na hakuwa na hakika ya kumuona tena.

Sindi na Tima walipotoka nje ya geti lile dogo lililokuwa limejengwa nyuma ya nyumba ile kwenye eneo ambalo hakuna mtu aliyepata kuwaza kuwa kulikuwa na geti walitokezea kwenye pori.

Jua lilikuwa linaelekea ukingoni na kufanya rangi za kuvutia kwenye angala wadidu. Vivuli vyao vilikuwa virefu wakati jua lilipokuwa likizama taratibu. umbali mfupi toka pale walipotokea. Walikutana na vijana wawili ambao walionekana kuwa pale wakiwasubiri wao.

‘Utaondoka na watu hawa… umesikia?’ Tima alimpa sindi maelezo akimkabidhi mkoba mdogo aliokuwa nao. Sindi akaachia mdomo wazi. Aliwatazama vijana wake kwa awamu, kwa uso uliojaa wasiwasi na hofu kubwa. Moyo ulimuenda mbio mno.

Ilikuwa ni afadhali kuongozana na Tima mpaka mwisho kuliko kuongozana na wanaume pekee asiojua ni watu wa aina gani na bora angejua alikokuwa akielekea. Sindi aliogopa, aliogopa mno!

‘ Usihofu… sawa?... utafika salama… na nitakuja kesho kutwa kukuona… be strong…sawa?’ Tima akazungumza naye akimshika mabega na kumtikisa kumtoa katika ile hali ya taharuki iliyomkuta ghafla.
‘Kambaulaya binti mwenyewe ndio huyu… naomba mfanye kama tulivyoongea’ Timakaongea na wale vijana
‘usijali dada… hamna shida’  kijana mmoja aliyeonekana kuwa na sura ngumu na misuli ya kutisha alimvuta Tima pembeni na kuzungumza naye kwa muda. Tima akatoa kitu kama karatasi na kumpatia kwa haraka sana yule kijana ambaye naye alikipokea kwa haraka na kukihifadhi mfukoni.

Sindi aliyaona yote haya na hofu ilimzidi lakini hakuwa na jinsi. Wakati huu giza lilishaanza kuingia na Tima aliporejea kwake alimkumbatia kwa nguvu na kumnpng’oneza
‘Be strong!’ kisha akamuachia na kuanza kuondoka pasipo kugeuka nyuma wala kumpungia mkono. Wale vijana wakaanza mwendo na Sindi akajikuta akiaza kuchapua hatua kuwafuata nyuma. Moyo wake ulikuwa mzito sana hasa alipowatazama wanaume hawa ambao kimuonekano tu ilitosha kumfahamisha kuwa hawakuwa watu wema lakini kwa muda ule angefanyaje? akaishika rozari ile kifuani akiwa amekumbatia vifurushi vyake na kuendelea kuwafuata watu hawa waliogeuka mara kadhaa na kumtazama kwa macho yao makali.
888888888888888888888888

Ufukwe wa bahari ya hindi ulikuwa ukileta upepo mwanana eneo zima la hotel ya Sunrise muda huu wa saa tatu usiku. Meddy aliyekuwa ametoka eneo la bahari na kuja kuketi kwenye kiti chake alimtazama Jerry na kusikitika kwa kutikisa kichwa, Jerry alionekana kuzama mbali kimawazo wakati akiyatazama mawimbi ya bahari yaliyopambana na upepo na kuleta mvumo wa kuvutia ufukweni hapo.

‘Jerry!’ Meddy akamshtua Jerry kwa kumuita
taratibu Jerry akaondoa macho yake toka kule baharini na kumtazama  Meddy. Walikuwa wameketi kwenye vile vitanda vya kupumzikia beach. Jerry alikuwa amelala chali mikono yake ikiwa imekutana nyuma ya kisogo. meddy alikuwa ameketi akimtazama Jerry na wakati huo akijifuta maji mwilini.

‘unawaza nini?’ Meddy akamuuliza
‘Mtoto wangu..’ akajibu Jerry akirudisha macho kule baharini
‘Mtoto?’ Meddy hakumuelewa haraka

‘…sidhani kama ni rahisi kuondoa mawazo kuwa kuna mtoto wangu kwenye tumbo la mwanamke ninayempenda sana…na sijui mtoto huyo yu hai au mfu… sijui mwanamke huyo anaishi maisha gani… unadhani amani ya moyo itatoka wapi?’ Jerry akaongea kwa uchungu

‘Come on Jerry!... kwanini unazungusha mambo namna hii?’ Meddy aliongea kwa jazba kidogo
‘Kivipi?’ Jerry naye aliuliza akimtazmaa tena Meddy
‘Sio wewe uliyeapa kuwa hutoleta tena inshu za Sindi katika maisha yenu na Pamella?.... kama hutaweza kuhimili haya mambo ni bora umwambie pamella ukweli… I cant stand kuona Pamella anaingia mahali ambako ataishi maisha ya kuumizwa kila siku sababu tu akili yako iko kwa mtu mwingine’ Meddy aliongea kwa hasira

‘… Pamella anaingiaje hapa?’ Jerry naye akaja juu akinyanyuka na kuketi akitazamana na Meddy
‘Pamella ni rafiki yangu… maumivu yake yote hunishirikisha… siwezi kusubiri awe anakuja kunililia kila siku kwa sababu ambazo ningeweza kuzizuia… be a  man Jerry!... damn! be a real man… face her na umwambie ukweli au meza kila kitu na uanze maisha upya’ Meddy alimgombeza mwenzake na asijue hali aliyokuwa nayo Jerry ilikuwa ni mtihani tosha

‘… kirahisi hivyo?... kama ungewahi hata kumpa mimba msichana na akaitoa angalau ukausikia uchungu ninaousikia hapa labda ungeongea kitu kingine… sio rahisi kama unavyodhani..angalau ningekuwa na uhakika mimba yangu ameitoa… sijui binti wa watu yuko wapi?... sijui anaishi maisha gani… sijui mimba niliyompa inamtesa kiasi gani…unaniambia be a man?... how? niipuuuze hii inshu nzima na kufanya kama vile sindi hakuwahi kutokea maishani mwangu?... sina roho mbaya kiasi hicho… na infact nampenda Sindi… nampenda sana…I’m a man enough to confess this ….now be a man enough to let Pamella know this’ akanyanyuka na kuondoka pale alipokuwa ameketi. akatembea kuelekea baharini akimuacha Meddy amenywea, akimuhurumia mwenzake na akishindwa kujua alipaswa kufanya nini sasa. akamshuhudia kwa mbali rafiki yake akifuta machozi.

Akakiri Jerry alikuwa na maumivu ambayo hakuna mwingine aliyeyaona isipokuwa yeye. ilikuwa imesalia wiki moja na siku kadhaa ndoa yake na pamella ifungwe, wakati watu wote wakiwa katika shamra shamra za kuandaa harusi ni Jerry tu hakuwa na amani ya moyo.
88888888888888888888

Ofisi ya Adella ilikuwa na dirisha lililoelekea kule casino. Mara kadhaa alisimama katika dirisha hilo na kuangalia yale yaliyokuwa yakiendelea ndani ya casino yake. Mlango wa ofisi yake ukafunguliwa na Tima akaingia akitabasamu.
‘Done!’ akatamka kwa furaha na Adella akaachia kicheko na kukimbilia kwenye friji ndogo iliyokuwa hapo. Akatoa mvinyo na kuzifuata glasi mbili zilizokuwa kwenye kabati jembamba lililokuwa kwenye kona.

akampatia Tima glasi moja na kummiminia ule mvinyo
‘cheeeers!’ wakasema kwa pamoja na kucheka
‘Wamemchukua kama ng’ombe anayekwenda machinjioni’ Tima akatamka akisogea kule dirishani

‘Wala hakuwa na wasiwasi?’ Adella akauliza kwa furaha
‘aliokuwa nao ila imani yake kwangu nadhani ilimfanya asiogope kufuatana nao’ Tima akasema akitabasamu
‘uliwaambia wahakikishe hakuna kinachopatikana?’ Adella akauliza kwa furaha akirejea kuketi kwenye kiti chake cha kazi
‘Wale vijana si umewatafuta mwenyewe… kazi yao zi unaijua na pesa juu nimeongeza yaani wahakikishe watakapomzika wanapanda mti kabisaa!’ Tima akamfurahisha bosi wake aliyekuwa naandika cheki ya pesa muda ule

‘chukua hii… shopping ya maana inakuhusu… now sina mtu wa kuniweka roho juu… yule binti alikuwa msumbufu mno…na angezidi kukaa hapa si ajabu kuna mambo yangeharibika vibaya mno… aisee! umetumia usanii wa hali ya juu kuwatenganisha mbwa wale…’ Adella aliongea kwa furaha akimkabidhi cheki ile Tima ambaye aliipokea na kuibusu kwa furaha kubwa.

Mirindimo ya wimbo wa Nadina ulisikika na wakajikuta wakikata kicheko chao na kumsikiliza Nadina. Adella alisimama na kulifuata dirisha. Kwa pamoja wakawa wanamtazama Nadina pale kwenye jukwaa la Casino

Ukumbi ulikuwa umezizima kwa ile mirindimo ya taratibu, lakini mzizimo ule uliletwa na muimbaji mwenyewe. Alikuwa anatokwa na machozi na kuimba kwa hisia mno. Ni kama vile alitaka aliyekuwa anamuimbia amsikie. Sauti yake kali ilipaa hewani na kutetemesha nyoyo za watu pale alipokifikia kibwagizo ambacho wengi walimsaidia kukiimba
‘….Nenda nenda nenda na wala usiangalie nyuma…na wala usinitafute tena na wala usinikumbuke… nimekubali kwa moyo mmoja tuuu… kuwa sitokuwa nawe …mileleee… nenda nenda nenda na wala usiangalie nyuma…’ akakirudia kiitikio kile safari hii sauti ikififia na kwikwi za kilio zikimzidia mwisho akaacha kuimba na kuinamia kipaza sauti huku akilia. watu wakabaki wanamshangaa.

ITAENDELEA

NIACHIE MAONI YAKO!

No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger