Wednesday, November 6, 2013

SINDI.... na LAURA PETTIE (45)

45
Sindi Nalela alikuwa sakafuni ndani ya chumba kile kile alicholazwa usiku uliopita, uso wake uliovilia damu hapa na pale ulilalia shavu la kushoto sababu ya kule kulala kiubavu huku mikono yake ikiwa imefungwa nyuma kwa kamba. Miguu yake ilikuwa imeunganishwa kwa kamba nzito ambayo haikumruhusu kutanua miguu yake hata kwa sentimeta moja. Alilala vile akimtazama Nadina aliyekuwa amelala mbele yake!


Alimtazama kwa huzuni na uchungu, akimhurumia kwa ile hali aliyokuwa nayo. Naye alikuwa amelala kiubavu akiwa amefungwa mikono kwa nyuma pamoja na miguu yake. hakuonekana kuwa na fahamu kwa wakati ule. Uso wake ulikuwa umejeruhiwa na mwili wake ulikuwa umevimba na kuvilia damu achilia mbali sehemu zilizojaa michubuko ya kusisimua. Sindi alifumba macho na kuruhusu machozi yamtiririke, aliyafumbua alimtazama Nadina na kujaribu kumuita kwa sauti ya chini.

‘Nadina…Nadina… Nadina…’ aliita kwa sauti yenye kitetemeshi akijaribu kujisotesha kumkaribia Nadina na ikamuwia vigumu mno kusogea. Midomo ikamchezacheza wakati akiruhusu kijito kingine cha machozi kifanye njia usoni pake. Akalia kwa kupepesa macho na uchungu ukamfanya agugumie kilio na hatimaye kukitoa kwa kwikwi huku akifumba macho na taswira ya kilichotokea na kuwafikisha ndani ya chumba kile ikipita kichwani mwake kama kipande cha sinema.

Baada ya kuokotwa kule njiani, aliletwa kwenye chumba ambacho aliishia kufungwa mikono kwenye kiti  huku miguu yake pia ikifungwa kwenye miguu ya kiti. akapokea suluba ya kutosha na kutisha huku akilazimishwa kumtaja aliyemsaidia kutoroka. Kipigo kilikuwa kimekolea mno wakati Adella alipohisi suluba alizokuwa anampatia zilikuwa si mali kitu!

Jasho lilikuwa linamchuruzika, nywele zake zilizokuwa zimefungwa kifagio nyuma zilikuwa hazikueleweka, alikuwa amelegea mno na maumivu aliyokuwa anayapata yalimfanya sasa ahisi kama vile mwili ulikuwa unaelekea kufa ganzi. Alitamani kufa tu na kupumzika ila ndio vile kifo nacho kilisimama pembeni na kumsikitikia!

‘Niletee waya wa moto…’ Adella aliutupa chini mkanda aliokuwa akitumia kumpigia Sindi na kuagiza silaha nyingine ya kumuadhibia. Sindi akajitutumua kuinua uso na kumtazama Adella ambaye alitabasamu kana kwamba alichoagiza kilikuwa kitu chenye kumletea faraja Sindi.

Yule mlinzi aliyekuwa nyuma ya Adella aliduwaa kwanza na asiamini alichosikia akiagizwa
‘hujanisikia au?’ adella akageuka na kumuuliza
‘Lakini yawezekana alikuwa mwenyewe..’ Mlinzi akajaribu kumtetea kwani hata yeye aliguswa na kile kipigo alichokuwa ameshapewa Sindi.
‘…nina uhakika na ninachokiamini… niletee waya… naona ana moyo wa mshumaa kukubali kuungua kwa ajili ya kumulika wengine… tutaenda sambamba tu…tuone mwisho wako bitch!’ lle tusi la mwisho likaenda sambamba na kofi kali la shavuni lililomfanya Sindi akaribie kuanguka na kile kiti. Mlinzi mwingine aliyekuwa nyuma ya Sindi alimpa mwenzake ishara ya kutii amri ya bosi wao.

Kule kuduwaa hakukumpata mlinzi peke yake, bali pia baadhi ya wasichana waliokuwa nje ya kile chumba wakisikiliza kilichokuwa kinaendelea mule ndani. Nadina alirusha rusha miguu kama mtu aliyebanwa na haja ndogo huku akikung’uta viganja vya mikono yake kwa kiwewe. Mlinzi alipotoka wale mabinti walitazamana  kwanza na Nadina akahisi alipaswa kujitokeza kabla ya waya uliogizwa haujamfikia Adella. Akawatoka wenzake na kuufuata mlango kwa kasi lakini wenzake wakamuwahi na kumshika

‘Nadina!... hivi unajua kitakachofuata?....’ Mwenzake akamtisha kwa kumtahadharisha
‘lakini ni mimi ndio nilimsaidia’ Nadina akatetea uamuzi wake na wakati akibishana na wenzake yule mlinzi akawapita akiwa na waya pamoja na chetezo kilichokuwa na vipande vya mkaa wa moto. Nadina akaweweseka na ile hali ya kushauriwa akaiona kama ilikuwa ikimuweka Sindi hatarini zaidi lakini ndio vile wenzake walimshikilia kwa nguvu zote.

Mlinzi akazama ndani na kufanya wale wasichana watulie na kusikilizia. hakukuwa na maongezi yoyote lakini dakika mbili mbele Sindi alipiga yowe kali la maumivu akimuita mama yake… akimuita Mungu wake… yowe lile lilibeba ujumbe wa maumivu makali yasiyovumilika na Nadina ambaye sasa alikuwa akilengwa na machozi aliwaponyoka wenzake na kuuvamia ule mlango wa kile chumba. Akaingia kwa pupa na kumkuta Adella akiinua tena ule waya uliobadilika rangi na kuwa mwekundu akiufuata mgongo wa Sindi.

Nadina akamvamia Adella na kumuangukia miguuni, akilia kwa uchungu na kiwewe.
‘Ni mimi… ni mimi…’ akakitegua kitendawili cha Adella ambaye aliurudisha ule waya kwenye chetezo na kumtazama Nadina kwa ghahabu kubwa!


‘Pumbavu!’ akaachia tusi lililokwenda sambamba na makofi mfululizo kwa Nadina. Akaokota ule mkanda na kumcharaza nao Nadina kwa hasira zote huku Nadina akiwa ameushikilia mguu wa Adella akimuomba msamaha. Akanyanyua ule mguu uliokuwa umeng’ang’aniwa na Nadina na kumsukuma katika mtindo wa kumpiga teke. Nadina akaangukia miguuni pa Sindi na kujitutumua kuketi, haraka akasotesha matako kinyumenyume akimkimbia adella aliyekuwa anamfuata. Maumivu yalimtembelea mwilini kama jeshi la siafu!

Masikini akagotea kwenye ukuta na kujikunyata, Adella ambaye alishamfikia alinyanyua mguu wake wa kulia uliokuwa na kiatu kirefu kiasi na kumkanyaga Nadina shavuni, akambana kwenye ukuta na ule mguu wake mpaka alipohisi kutosheka. Akauteremsha mguu na kuchuchumaa mbele ya Nadina aliyekuwa anatetemeka kupitiliza. Alitarajia kipigo baada ya kujitokeza ila si kipigo kama kile!

mkong’oto aliompa ulikuwa wa haraka na wa uhakika. Ndani ya dakika zile alikuwa amemchakaza mno Nadina ambaye maumivu yalimfanya asielewe hata kile alichokuwa akiambiwa na Adella. Alichachatika nusu akili zikimruka!
‘Sikuwaleta hapa kucheza kombolela na mimi… na nyie sio wa kwanza kuja hapa na hamtakuwa wa mwisho… ukiwa mstaarabu nakuwa mstaarabu ukiwa mshenzi nakuwa mshenzi mara mbili… hapa sijakupiga binti… nimekupapasa kwa upendo sana…’ Adella aliongea taratibu lakini kwa sauti iliyojaa hasira ndani yake

Akanyanyuka na kuachana na Nadina na kurejea kwa Sindi aliyekuwa amelegea pale kwenye kiti. Akakishika kidevu chake na kukitumia kuinua kichwa cha Sindi. Wakatazamana!
‘Hatujamalizana bado… nataka ili liwe funzo la kwanza na la mwisho kwako’ akakiachia kichwa cha sindi na kukifuata chetezo. Kitendo kile kikamfanya Nadina ajue Adella alitaka kuendelea kumchoma Sindi na ule waya wa moto.

Akajikuta tu akinyanyuka kidogo na kutembelea magoti kumfuata Adella, akimuomba msamaha na kuahidi kila alichoona kingewaokoa toka katika kile chumba. Adella akageuka na kumuamrisha yule mlinzi aliyekuwa nyuma ya Sindi kumtandika Nadina. Kilio cha Nadina kilimfanya hata Sindi aliyekuwa hana nguvu naye ajitutumue kuomba msamaha ili tu Adella asiendelee kumuadhibu Nadina.

Mlinzi akampiga Nadina kiasi cha kupoteza fahamu pale sakafuni huku yeye Adella akitabasamu. Aliporidhika akamuamrisha yule mlinzi kusimamisha kipigo. Akaagiza wawekwe kwenye kile chumba alichokiita kuzimu na kuishia zake. Sindi akalia akimtazama Nadina aliyekuwa anavuja damu puani na sehemu mbalimbali za mwili. akajivuta kwa nguvu na kusababisha aanguke na kile kiti na kulala kando ya Nadina.

Akalia, akalia mno na alilia kwa mengi lakini hakuwa na jinsi na hata baada ya kuingizwa ndani ya chumba kile bado Nadina alikuwa hana fahamu na ndio alikuwa akimtazama kwa uchungu, akitamani yote yale yanayotokea katika maisha yake yawe ndoto! Ulikuwa usiku mwingine mrefu kupindukia!
8888888888888888888888888

Ala ya muziki wa taratibu ilisikika toka katika redio iliyokuwa mita chache toka kilipo kitanda chake. Jerry Agapella aliisikiliza ala ile ya forever in love ya Kenny G, ala itumiwayo katika kipindi cha chombeza time cha redio moja nchini. Ala ya muziki aliyopenda kuiskiliza kila alipohisi upweke, ala ile ilimkumbusha mbali mno, ilimkumbusha mtu aliyezunguka kichwani mwake karibu ila robo tatu ya siku yake iendayo kwa Mungu. Alimkumbuka Sindi Nalela!

Glasi ya mvinyo iliyokuwa mkononi mwake iliganda mkononi pasipo kuelekea kinywani wala kutua chini. Aliitazama ile glasi wakati akili yake ikipotelea mbali na upeo wa macho yake. Ilimjia kichwani siku ile ambayo Sindi alikuwa akigombana na Peter mdogo wake na yeye kuwa katikati yao … akaikumbuka siku aliyomtembelea Sindi kule kwenye lile darasa alilokuwa akifundisha na kusababisha watoto kupoteza umakini na kumtazama yeye Jerry wakati akimchungulia Sindi… akatabasamu zaidi wakati alipoikumbuka siku ile aliyomletea Sindi zawadi ya khanga iliyoandikwa ‘nikikosa nirekebishe’, akalikumbuka tabasamu la binti huyu, kicheko chake na zaidi uzuri wake!

Tabasamu la Jerry likatoweka taratibu kichwa chake kilipoamua kuirejesha siku ile ya mwisho aliyokuwa na Sindi….‘Wewe ni naniiii?.... wewe sio Jerry John….wewe ni nani?....unataka nini kwangu?’ sauti ya sindi na taswira yake akiwa amehamanika vibaya mno vilimjia moja kwa moja na kumfanya afumbe macho na kuweweseka.
Akaiweka ile glasi ya mvinyo kwenye kabati dogo lililokuwa kando ya kitanda na kukikamata kichwa chake kwa nguvu kana kwamba kuna mtu alitaka kuking’oa.
‘Oh God please!..’ akarai huku akiligeukia lile kabati dogo na kuitazam chupa ya mvinyo iliyokuwa kando ya glasi. Akaivamia na kuipeleka mdomoni, akipiga funda kadhaa kwa pupa na kuitua ikiwa tupu.

Mwili ukamsisimka, wakati akikiinua kichwa na kuitazama picha ya kuchora iliyoandikwa maneno matamu kuhusu Sindi, picha ile  ilikuwa imebandikwa mbele yake. Akaitazama kwa huruma mno wakati midomo yake ikimchezacheza na asijue la kutamka.

Haya ndio yalikuwa maisha yake, upande wa pili wa maisha yake ambao ni Meddy tu ndio aliyeujua kwa undani. alijitahidi mno kuwa sawa mbele za watu lakini kila usiku uliopita akiwa peke yake Jerry aliuweka uanaume kando na kulia peke yake, akasononeka na kujiliwaza kwa pombe kali kutuliza mawazo na maumivu.

Ala ile iliyokuwa imechachamaa sasa na vyombo kusikika vikiomboleza katika namna ya kuvuta hisia ilizidi kumtia wehu Jerry. Akainuka na kusimama kando ya kitanda akipepesuka  kidogo na kujitahidi kupiga hatua kuelekea kabatini. Akalifungua kabati na kutulia kwanza akiwa ameshikilia milango ya kabati kwa pamoja. kisha taratibu mkono wake wa kulia ukakiachia kitasa na kuzama ndani ya kabati. Akatoa bastola ndogo na kuishikilia mkononi. Taratibu akatoka kabatini na kurudi kuketi kitandani. Akiendelea kuitazama ile bastola huku machozi yakimtiririka…
88888888888888888888888888

Usiku huu haukuwa mgumu kwa Jerry peke yake bali pia Fiona Agapella. wakiwa wameketi kitandani kwa Iloma. Fiona alikuwa anamtazama iloma na kutikisa kichwa kulia na kushoto kuonyesha hali ya kukata tama
‘he won’t call… nimeondoka muda mrefu sana Iloma… alitakiwa awe amepanic na kuanza kunitafuta… ona…’ akanyooshea saa iliyokuwa ukutani
‘Saa saba kasoro… na hajapiga simu yangu wala yako… hii inamaanisha nini sasa?’ Fiona aliongea akitaka kushuka toka kitandani na Iloma akamuwahi.

‘Wakati unaondoka alikuona?’ Iloma akamuuliza haraka na hivyo kumfanya Iloma asitishe uamuzi wa kutoka kitandani pale
‘aliniona sana… hata wakati naweka nguo sandukuni he was there..’ Fiona alijibu kwa hamaki kidogo
‘hakusema kitu?’ Iloma akauliza tena na Fiona akatikisa kichwa kulia na kushoto mara kadhaa

‘okay Fifi…listen…’ Ilom akamkaribia rafiki yake na kumshika mikono akitafuta maneno ya kumfanya pengine atulie na kulala japo kwa masaa machache yaliyobaki.
‘ni masaa machache tu yamepita tangu uondoke… subiri kesho asipokutafuta ndio tujue cha kufanya…’ Iloma akamshauri huku moyoni akimlaumu rafiki yake huyu kwa kutikisa kiberiti kipindi kama hiki.

Fiona akatazama pembeni akiashiria kutokuukubali uamuzi ule ila ndio vile hakuwa na jinsi
‘What is asiponitafuta si ndio nitakuwa nimeachika?’ Fiona akauliza akionyesha dalili zote za maumivu ya moyo
‘atakutafuta Fiona!...trust me! na asipofanya hivyo tutajua cha kufanya… come on Fiona where is the iron lady I used to know!...’ Iloma alijaribu kumuweka Fiona sawa pamoja na kujua ukweli kuwa mwenzake alikuwa katika hamaniko kubwa mno!

ukimya ukapita kati yao wakitazama chini kama watu wanaofikiria kisha Iloma akainua uso na kumtupia Fiona swali.
‘dada yako Adella yuko wapi?’

Fiona akainua uso na kujitutumua kutabasamu lakini tabasamu lile halikudumu usoni pake. machozi yalimlengalenga na akajikuta akiyawahi kabla ya kuteremka mashavuni
‘Sijui kama yu hai au mfu… sijui… I just don’t know na sitaki hata kujua’ Fiona akajibu akilazimisha tena lile tabasamu
‘Why?...’ Iloma akadadisi kwa shauku mno akijisogeza karibu na Fiona. Kuna mengi mno alikuwa hayafahamu kuhusu huyu rafiki yake.

‘…ni long story but nilipotoroka kwa mjomba nilimuacha akitumikishwa kama mkewe… miaka miwili baadaye nilimtafuta na nikamkuta mjamzito…’ Fiona akasita kwanza akivuta kamasi nyepesi
‘… nikamtorosha na kwenda kuishi naye… alikuw kama mwehu… nadhani sababu ya mateso na kubakwa… akajifungua mtoto wa kike na siku aliyojifungua sikuwepo… akamtelekeza mtoto kwangu na kutokomea… sikumuona tena… sikumuona tena adella… sikumuona tena dada yangu’ Fiona alitiririkwa na machozi na kujiinamia.

Iloma akamsugua sugua mgongoni kumtuliza mpaka Fiona alipoinua kichwa na kujaribu kufuta machozi.
‘sasa mtoto aliyemzaa yuko wapi?’ iloma akajikuta tu akiuliza
‘…Nilimuita Nadina… niliishi naye kwa kinyongo sana sababu alikuwa damu ya mjomba… sikuwahi kumjali wala kumpenda… aliishi akijua mimi ni mama yake na siku zote alishangaa namna nilivyokuwa nikimchukia… usiku mmoja alipoteza pesa ya chakula… sikuwa hata na senti iliyobaki… nikampiga mno… nikamuadhibu vibaya mno na kumfukuza… Nadina akaondoka… ni miaka mingi sijamuona… sijui alipo… sijui’ Fiona aliongea taratibu safari hii akilitazama shuka na kutiririkwa na machozi.

Iloma naye akafuta machozi na kutikisa kichwa kwa huzuni.
‘…nimeishi maisha yote mabaya duniani… then I met Sophia Agapella… akanitoa mitaani na kunipa makazi na kazi, akanifanya ndugu yake wa pekee kwa vile alikuwa yatima aliyelelewa katika kituo… akaniamini mno and see what I did to her… nikamuua… nikamuua Sophy…’ akashindwa kuendelea na kulia zaidi sasa kwa sauti kubwa ya kuombolez na Iloma akafanya kazi ya ziada kumbembeleza.

ITAENDELEA….

2 comments:

  1. kuna mengi nyuma ya pazia kuhusiana na fiona!!! good story laura!!!!

    ReplyDelete
  2. mwisho wa ubaya aibu!!! fiona mwisho wake umefika

    ReplyDelete



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger