Tuesday, December 1, 2015

HAPPY NEW MONTH…MAMBO 6 NINAYOKUKUMBUSHA!


Mpenzi msomaji!

Tunauanza mwezi mpya… mwezi wa mwisho wa mwaka…mwezi wa  likizo kwa wengi na mwezi unaojulikana kama mwezi wa sikukuu. Christmas na Mwaka mpya  ni wiki chache zijazo. Ni jambo la kumshukuru Mungu sana kuwa mimi na wewe mpaka dakika hii tupo hai na kwamba pamoja na changamoto zote za kidunia na kiimani bado tungali hai tukipewa nafasi nyingine ya kunyoosha njia zetu na kurekebisha hapa na pale. Tunasema Asante Mungu!

Kama ilivyo ada tunapouanza mwaka, wengi wetu huwa tuna zile New Year’s  Resolutions!.... mipango ya mwaka  mpya kwa mwaka mzima. Na sasa tunapoelekea kuumaliza mwaka tunapaswa kukaa chini na kutazama ni yapi tumeweza kuyatimiza na yapi yamekwama na kwa sababu zipi. Kwa ujumla ni wakati wa kujitathmini kwa kina na kujiandaa kumalizia yaliyokwama na pengine kupanga mengine mapya.

Yawezekana yapo tuliyoyapanga  lakini kutokana na sababu za maana na zisizo za maana kama uzembe na kukata tamaa basi tumeshindwa kuyatimiza. Si busara kuyatupa mbali na kutafuta mapya, ni vema tujitathmini ni kwa vipi mambo haya hayakutimia ili kuyajua kwa undani madhaifu yetu na kuyafanyia kazi.

Kwa kuuanza mwezi nina neno kwako msomaji! Mambo haya SITA  nimeona ni mazuri tukiyafanyia kazi wakati tunapoelekea kuumaliza mwaka.


1. ONDOA VINYONGO, MINUNO,  HASIRA NA VISASI:
 ….. katika safari yetu ya maisha hapa duniani yapo mambo na wapo watu ambao hutukwaza kwa kiasi cha kuacha makovu mioyoni mwetu… tunaapa kutowasamehe…. Tunaapa kuwachukia kila tunapowaona…. 
Mpendwa msomaji!
Kwa imani yangu ya kikristo tumeagizwa kusamehe duniani ili Baba Mungu apate kutusamehe pia dhambi zetu…. Wakati tunapoelekea kuumaliza mwaka ni vema tuitue mizigo hasi chini na kujaza mioyo yetu amani na utulivu wa nafsi….

Samehe hata kama hujaombwa msamaha! Msamehe na jisamehe! Na uanze mwezi mpya wa mwisho wa mwaka ukiwa na roho safi isiyo na chochote hasi dhidi ya mtu mwingine! Kukaa na vinyongo, hasira na visasi moyoni dhidi ya mtu hakukusaidii kitu zaidi ya kukufungia mibaraka kwako na kizazi chako!

2. OMBA MSAMAHA WA DHATI:
…. Waombe radhi uliowakosea. Wahenga walisema Kiburi si maungwana. Inakufaidia nini kujaa kiburi kiasi cha kushindwa kuomba radhi kwa mtu uliyemuumiza na unajua fika kuwa umemuumiza? Jishushe na umpe mwenzio amani ya moyo! Hakika hata wewe utajisikia amani kupatana na mtu uliyemkosea hata kama hatokusamehe hapo hapo lakini utakuwa umejitoa lawamani.

3. ANZA KUANDAA MIPANGO YAKO
…. Binadamu huwa  tunapanga ila Mungu huwa ana mipango yake inayompendeza yeye. Pamoja na hili, haituzii kuanza kujipanga. Usisubiri kesho, usisubiri mwakani. Nafasi ya kurekebisha uliyokosa kuyafanya kwa wakati uliopita anza leo kurekebisha japo hata kwa kukaa chini na kupanga ni namna gani utarekebisha…. Usiogope kujikosoa na kuyaona madhaifu yako kwa uwazi. Itakusaidia kupambana na changamoto zijazo…. Yawezekana ulipanga kuwa na biashara yako…. Usingoje krismasi ipite anza leo hii tar 1 kuweka mawazo yako ya wapi uanzie!

4. SAIDIA WENGINE WAFANYE WATABASAMU
…. Wasaidie watu wengine kufikia malengo yao hata kwa kuwapa moyo na mawazo chanya. Usishiriki katika kumdidimiza mwenzio…  kuna mema mengi Mungu amekufanyia kwa mwaka huu. Hata kama unayapima mema hayo kwa kulinganisha na ya mtu mwingine… bado kuwa na afya njema, kuwa na kama ulivyo, kuwa  na watu wako, kuwa hai ni kati ya mema unayopaswa kuyashukuru kwa Mungu na kuyarejesha kwa njia ya kufariji wengine….

Mnunulize mtu zawadi na umpatie pasipo sababu yoyote…. Mpe chakula masikini ili uone tabasamu lake usoni… zungumza na mtu aliyekwama mpe matumaini ya maisha… msaidie mzee kwa furaha uone shukrani yake usoni…. Mpishe njia mwenzio kwa nidhamu… mfungulie mlango mwenzio kistaarabu… msalimie mtu ambaye siku zote huwa humsalimii…mpe bonus mtumishi wako wa ndani….  Mpigie simu ndugu yako aliye mbali ambaye ni ndugu yako wa karibu lakini huwa huna mawasiliano naye...mtu kama bibi, shangazi, babu , baba mkubwa...baba mdogo au ndugu yako wako wa damu nk...
unaweza hata ukamwambia rafiki yako.... mpenzi wako...mwenzi wako namna anavyogusa maisha yako...ukamshukuru akiwa hai kuliko kungoja siku yake ikifika ndio maneno yakutoke akiwa ameshatangulia!
Na mengine mengi! Yote kwa yote  fanya jambo lolote lililo ndani ya uwezo wako kumfanya mtu mwingine atabasamu!

5. JIPONGEZE
Wengi tunaishi tukiyatafuta maisha na kusahau kuyaishi maisha yenyewe
Jipongeze hata kwa kitu kidogo ulichofanikiwa kukifanya.... Jipe muda ukafanye massage.... toka nenda mahali mbali ukapumzike wewe na wmenza wako au peke yako.
Jinunulie kitu cha kukufurahisha.... jiambie maneno mazuri ya kujenga nafsi .... usikae ukajiambia maskini mimi... kwanini mimi.... sina bahati hiyo na kadhalika. maneno mabaya huumba haraka!


5. KIKUBWA TATHMINI UHUSIANO WAKO NA MUNGU!
.... wengi tunajisahau sana katika hili. Tunadhani siku pekee ya kuongea na Mungu ni siku ya kumuabudu… ni wakati unapokwamba tu ndio umkumbuke Mungu…. Jiulize ni Mara ngapi pasipo sababu yoyote umetabasamu ukamshukuru Mungu wako…. Pengine baada ya chakula cha mchana… pengine baada ya kuitazama meza ya ofisi yako…pengine baada ya kutazama watoto wako…pengine baada ya kulitazama gari lako ama tu kwa kujihisi mwenye bahati kuwa hivyo ulivyo, hapo ulipo!.... jiulize ni mara ngapi katika maisha yako umeongea na watu kuhusu Mungu katika namna ya kuwakumbusha uwepo wake?
Kuna watu wanadhani mambo ya Mungu hayawahusu…. Au ni ujanja f’lani kutokuzungumzia kuhusu imani na Mungu hadharani lakini Shetani anapokutandika na majanga haraka sana watu husema Mungu nisaidie…maombi yenu wapendwa nk!
Tunapoelekea mwishoni mwa Mwaka tunapaswa kujipongeza na kujirekebisha pia!

Kwa siku ya leo naishia hapa!
Niwatakie mwezi mpya mwema! Panapo majaaliwa basi tukutane tena wakati mwingine


Laura Pettie

2 comments:



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger