Saturday, September 12, 2015

UREMBO NA LAURA: .....J4 - JIPENDE, JITHAMINI, JIAMINI, JIVUNIE WEUSI WAKO!!!!


Haya jamani mpo wana kona ya urembo na Laura?

Kama umepata nafasi ya kujumuika nasi hapa, ukaisoma makala hii,  basi tuna kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu!

Leo nataka kuongea na akina dada weusi… weusi tiiii kama mimi ambao bado hawajajikwangua au ndio wanafikiria kujikwangua. Anti wewe ni mzuri tu, …..na weusi wako huo ulionao…..unaweza kuendelea kuwa mzuri hivyo hivyo ulivyo!

Kuna watu wanadhani kuwa mweupe ndio kuwa mzuri, ndio kuwa mrembo, ndio kuwa mlimbwende! HAPANA!!.... si kweli! Hata ukiwa na weusi wako huo huo ulionao bado unaweza kuamua kujiweka katika namna ya kuvutia na ukavutia. Siku zote vile utakavyosimama mbele za watu ndivyo watu watakavyokuchukulia…. Ukijiamini watu  nao watakuamini pia!!

Nimepaka wanja na Lip Balm tu!.... 
usoni hata poda ya kawaida  haijapita

Katika pitapita zangu mitandaoni, hivi karibuni nimegundua kumekuwa na ongezeko la bidhaa za kujichubua. Tena wauzaji wakisifia kabisa kuwa unakuwa mweupee, unatakata, unakuwa na rangi f’lani amazing n.k kana kwamba kuwa mweusi ni laana au uchafu!

Huwa nasikitika sana ninapoona feedback ya bidhaa hizi kwenye picha ambapo  mtu aliyekuwa na weusi wake mzuri tu amekuwa mweupe na ndio anasifiwa kuwa amependeza na amekuwa mzuri.

Uzuri ni vile unavyowaza wewe na unavyojichukulia! Miaka  fulani nikiwa mtoto  mdogo nilikuwa na rafiki yangu aliyekuwa mweupe sana……. Namna alivyojipenda na kujisifia kila mara  kuhusu rangi yake alikaribia kunifanya niamini mimi sikuwa na rangi nzuri hata kidogo hata hivyo kila nilipojitazama niliipenda rangi yangu pia.
Ni mweusi lakini mzuri tu!!

Nilitaka kuanza kuamini weupe ni uzuri mpaka siku moja tukiwa wawili mbele ya watu fulani, mtu mmoja akasema kwa sauti…Laura usije ukajichubua baadaye baki hivyo hivyo una rangi nzuri sana! Rangi adimu! Mweusi anaweza kuwa mweupe lakini mweupe hawezi kuwa mweusi!

Kumsikia mtu akiisifia ngozi yangu kulinipa kujiamini sana, na sasa ndio nikagundua watu wengi wanasikia watu wakisifia weupe wanadhani weupe ndio uzuri  (kama mimi nilivyokuwa nasikia rafiki yangu akijisifia sana)…..kwa kuwa ni nadra kwao kusikia mtu akiwasifia kwa ngozi zao nyeusi (kama mimi nilivyosifiwa)….


Wakati naingia usichana, mama yangu aliniambia kila mara usije ukajichubua baki hivyo hivyo huoni mimi nilivyo mzuri tu (mama yangu ni mweusi pia)… kumsikia mama akisema hivi kulinijaza ujasiri zaidi na leo naweza kumwambia mtu yoyote mweusi BAKI HIVYO HIVYO ULIVYO HUONI MIMI NILIVYO MZURI TU HAHAHAHAAAAA!!
Ni mweusi Ti! na bado ni mzuri tu
na anajikubali mpaka weupe tumemkubali!

Yaani unakuta mtu kajichubua ana sugu balaaa, mwingine mashavu yameungua….mwingine mpaka ndevu zimemtoka… mkorogo umembabua miguu yaani unamtazama unamhurumia maana badala ya kuwa mrembo anakuwa kituko kwelikweli…. Mwingine mweupe kama karatasi yaani mpaka unajiuliza yote haya juu ya nini jamani?

Anyway, unawezaje kutunza  ngozi yako nyeusi na ikavutia?
MAMBO 10 YA KUZINGATIA


1. KUNYWA MAJI MENGI…. Kunywa maji kadiri uwezavyo, Uvivu wa kunywa maji unachakaza ngozi na badala ya kuitibu watu hukimbilia makemikali kuing’arisha kinguvu wakati kumbe maji ni dawa nzuri sana!.... najitahidi lita 1 hadi mbili kila siku! ukiona hayana ladha weka vionjo kama limao kwa mbali au ndimu.

2. Safisha ngozi yako kwa vitu visivyo na kemikali, pendelea vitu natural hata kama ni vya kizungu ila vyenye ingredients natural…. Mfano usoni napenda sabuni ya Liwa, zile natural kabisa au zile zinazofungwa kwenye cover ya kahawia zimeandikwa sandwool soap bee and flower!

3. Tumia vipodozi vinavyoendana na ngozi yako…. Poda, foundation etc viwe vya ngozi yako vitakupa muonekano mzuri sana.

4. Kula chakula bora hususani matunda na mbogamboga usisubiri uandikiwe na daktari


5. Fanya mazoezi- mazoezi mepesi tu ambayo yatakutoa jasho kidogo. Ukiwa mvivu wa mazoezi kama mimi, weka hata muziki wa bolingo ucheze mpaka jasho likutoke. Jasho linapokutoka unapunguza uchafu mwili na ufungua vitundu vya kwenye ngozi hivyo ngozi hupumua

6. Kuwa na furaha…. Stress kuleta makunyanzi! Haijalishi una msukosuko kiasi gani katika maisha, Jifunze kujipa nafasi ya kutabasamu na kushukuru japo hata kwa uhai ulionao. Usiweke vitu moyoni au kichwani kiasi cha kukunyima furaha kwa muda mrefu. Unapokosa amani ya moyo unakosa usingizi ambao ni chanzo cha ngozi kuharibika

7. Jipende, Jithamini, Jiamini…. Jifanyie mambo ya kupendeza, jisikie wewe ni wa kipekee, jizawadie, jipambe, jitunze, jiheshimu. Usikubali mtu akuaminishe wewe ni mbaya kwa kuwa ni mweusi.... unapojipenda utagundua staili ya nywele inayokufaa...staili ya wanja inayokufaa... rangi ya lipstick inayokupendeza...yote haya utayagundua ukijipenda kwanza!

8. Ielewe ngozi yako- Je una ngozi kavu, una ngozi ya mafuta sana au ya kawaida. Ukiijulia ngozi yako itakusaidia uepuke vipodozi vyenye mafuta ambavyo vinaweza kukuletea chunusi… au kutumia vipodozi vikavu huku ngozi yako ni kavu

9. Usibadili badili vipodozi kufuata mkumbo- kwa kuwa umesikia kipodozi fulani kinatangazwa sana basi unakitafuta na kujaribu… vipodozi au vifaa vya kusafishia ngozi unavyotumia vikikukubali tulia navyo tu usihangaike kubadilibadili vitu.

10. Jifanyie Scrub za asili, massage, steaming nk kuondoa cell zilizokufa kwenye ngozi na kuipa uhai zaidi. Scub husaidia sana kuondoa cell zilizokufa na vijimakovu na alama nyeusi.

Wewe dada uliye mweusi tulia na weusi wako!

Usirubunike kuchubua ngozi yako ukiamini ndio utaupata urembo

Hivyo hivyo ulivyo unaweza kuamua kuwa mrembo

Najivunia kuwa mweusi kwa kuwa sasa naweza pita mahali nikajikuta ni mweusi peke yangu na nikaonekana na mvuto kuliko hata hao weupe hihihiiii
ADIOS!!!




































No comments:

Post a Comment



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger