Saturday, April 26, 2014

BARAZANI....

HEBU TUNZA YA LEO YAKUSITIRI KESHO EBO!!

Ni kitambo kweli hatujakutana barazani hapa… kuzungumza hiki na kile lakini leo kwa kudra za Mwenyezi Mungu tuko pamoja tena. Alhamdullilah!

Basi hivi juzi kati hapo katika mishughuliko ya hapa na pale nikakutana na kijana mmoja ambaye nilipata tu kufahamiana naye kipindi cha nyuma. Kwanza nilisikitika si tu kwa ile hali aliyokuwa nayo bali pia ulinganisho niliofanya kipindi cha nyuma nilichomuona na sasa hivi alivyo. Tunasema maisha yanapanda na kushuka ni kweli! ile sasa kuna wanaopandishiwa kisha wanayashusha wenyewe...!


Miaka miwili iliyopita huyu kaka alikuwa mmoja wa wale vijana waliokuwa na maisha ambayo kijana yoyote wa rika lake angetamani kuwa nayo. Sehemu ya kuishi, gari la kutembelea na pesa ya kubadili mboga.

Ingawa ndio kwanza alikuwa ameyaanza maisha lakini kwa kipindi kifupi hicho alikuwa ameyapatia. Sasa juzi kati nilipokutana naye ndio mdomo ulinishuka kama kidevu cha punda! Kama ilivyo hulka ya binadamu kuuliza kulinikamata nikianzia kujiuliza mwenyewe mpaka kuuliza wengine! Kulikoni?

Ndio sasa nikaambiwa jamaa aliyapatia maisha lakini ndio vile akili zingine aliwaachia marafiki wamshikie na wakamshikia kwelikweli wakamuachia ya kuvukia barabara. Hakuna baa ambayo hakutoa ofa, hakuna binti ambaye alimvutia na akampita tu… hakuna starehe iliyokuja na ikampita… akawa mwema kwa kila mtu aliyetaka kukopa laki na asilipe sawaa.. aliyetaka elfu hamsini akahonge hayaaa…aliyataka yote kwa pupa!

Si akiba,… wala vitega uchumi… alijua kesho ipo ingemletea ya kula kesho kutwa akisahau kutunza ya leo imsitiri kesho na keshokutwa. Jambwe! Kwisha habari yake! Sasa jiulize wale aliokuwa akitanga njia nao wako wapi?... unaambiwa hakuna hata nusuru ya kusema huyu alimlia vyake leo kamsitiri. Hakuna!

Ndugu yangu, kijana mwenzangu!.... hawa watu tunaowaita marafiki tunapokuwa kileleni ndio hawa hawa wanageuka wageni tunaposhuka sakafuni. Hawa hawa wanakusifia kwelikweli ndio hawa hawa watakusimanga utakaposhuka… maisha ni wewe, wema tuufanye kwa kadiri tukikumbuka kuna kesho sio kwa kutegemea wema unaoufanya leo basi utakuletea malipo utakapoanguka. Sahau!

Tenda wema kwa kiasi ndugu marafiki wanafirisi…huamini?... ishi kwa malengo jua kuna kuporomoka kesho!... kijana starehe haziiishi duniani kila uchao kuna mapya kama matoleo ya simu!... utayaweza? Utayamaliza?...

Sijasema usisaidie ndugu na marafiki!...angalia uwezo wako kwanza ndugu yangu…usitake kumfurahisha kila mtu mbele yako… wakati hali yako mwenyewe ukunga ukijikuna watoka unga….utalia kilio cha mbwa mdomo juu.

Nimemaliza!

Wasalaam

LAURA

1 comment:



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger