Sunday, October 20, 2013

BARAZANI... TUNAPASWA KUSHUKURU KWA DHATI



Katika safu yetu ya leo ya barazani… ninayo machache tu ya kusema na wewe ndugu msomaji…

Yawezekana wewe ni mwanamke…. una kazi nzuri yenye kukuingizia kipato… una afya njema tu inayokupa nafasi ya kuzunguka huku na kule…. una marafiki wanaoifanya siku yako iishe katika namna ya kupendeza…. lakini huna mume pengine huna hata boyfriend ama unaye lakini maumivu anayokupatia katika uhusiano uliopo unajihisi kama mtu mpweke sana. Pengine unavyo vyote hivi lakini huna mtoto na unaona kama dunia inakuonea, Mungu amekutupa!


Yawezekana wewe ni mwanaume… kazi uliyonayo si sawa na elimu uliyoisotea… pengine maisha yako ni ya chini sana kulinganisha na maisha ya rafiki zako… unafanya hiki na kile katika kuongeza kipato lakini bado maisha yako hayako katika hali unayoitaka… matatizo ya kimaisha yanakuandama kila uchao… unajihisi mpweke hujui hata ufanye nini kuboresha hali yako… mwanamke umpendaye anaelekea kushindwa kukuvumilia… heshima yako kama mwanaume inatetereka kwa vile maisha yako ni duni… unahisi kuonewa, Mungu amekutupa!

Huna furaha ya kweli ndani ya moyo wako…. unasema I’m blessed huku ndani ya moyo wako unajua unaudanganya ulimwengu kwa vile unachokitamka si kile unachokihisi… unasema nina furaha huku uso wako umekosa nuru ya kweli

Rafiki unapaswa kushukuru kwa dhati!
Wakati ukijiona mwenye bahati mbaya na mikosi…. wakati ukishindwa kufurahia kile kidogo ulichobarikiwa kama afya njema kumbuka kuwa kuna watu wako kitandani kwa miaka kadhaa wakiugulia maumivu yasiyopoa… wako hospitalini kwa miaka kadhaa kwa kukosa kiasi Fulani cha fedha kurejesha afya zao…. kumbuka kuna watu wenye ulemavu wa maisha unaowazuia hata kuifikia elimu uliyonao, hata kuzunguka huku na kule unakozunguka wewe… hata kuwa na marafiki wanaoipendezesha siku yao…. hata kuwa na kazi hiyo hiyo ndogo unayoona haikufai…

Kwanini usimshukuru Mungu kwa yale aliyokubarikia?.... kwanini usiwe na furaha ya kweli kwa yale uliyonayo?... kwanini uudanganye ulimwengu uko sawa wakati moyo wako umejaa Simanzi?... kwanini ulitunze sononeko moyoni wakati una kila sababu ya kuamka kila asubuhi na kumshukuru Mungu kwa hali uliyonayo!

Mungu wetu ni Mungu wa rehema… Anasikia, anasikiliza na anajibu sawasawa na mapenzi yake! Mshukuru kwa yale aliyokupatia kwanza, furahia yale uliyobarikiwa kwanza, utavuta hali chanya katika maisha yako. Mungu atakupatia mengine mengi zaidi. Lakini unaponung’unika moyoni ukidhani binadamu hawatokusikia jua Mungu anakusikia, unaposhindwa kuyafurahia maisha yenye unafuu aliyokupatia sasa kwa jambo moja dogo tu katika maisha yako… UNAKUFURU!

kuna watu waliopata kubarikiwa kila unalotamani na wakavipoteza ndani ya muda mfupi tu!... Jifunze sasa kushukuru kwa dhati toka moyoni  na si kumpatia Mungu sifa ya uongo mbele za watu kuwa amekubariki huku ndani ya moyo wako una fundo moja kubwa la huzuni kuhusu maisha yako!

USIACHE KUMUOMBA MUNGU NA USIACHE KUMSHUKURU PIA!


Wasalaam, Laura Pettie!!

2 comments:



Snowfall Widget for Blogger


Snowfall Widget for Blogger